METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, May 12, 2020

DKT MABULA AZINDUA KAMPENI YA UVAAJI BARAKOA KWA MAKONDAKTA NA MADEREVA MWANZA



Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula amezindua kampeni ya uhamasishaji wa uvaaji wa barakoa, unawaji mikono wa mara kwa mara na uchukuaji wa tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Covid-19 unaoenezwa na kirusi cha Corona kwa madereva wa daladala, makondakta na abiria katika mkoa wa Mwanza.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo katika ofisi za chama cha madereva mkoa wa Mwanza (MWAREDDA) Mhe Dkt Mabula amekipongeza chama hicho kwa kuunga mkono jitihada za Serikali inayoongozwa na Rais Mhe Dkt John Magufuli katika kupambana na ugonjwa wa Covid-19 unaosumbua dunia kwa sasa, Na kuongeza kuwa Serikali inatambua changamoto wanazokutana nazo na itaendelea kuzitafutia ufumbuzi moja baada ya nyengine huku akiwataka madereva na makondakta  hao kuendelea kuwa wamoja 

‘.. Siku zote unapopigania haki mkiwa wengi mnakuwa na nguvu tofauti na mnapokuwa mmoja mmoja, Tutumie vyama vyetu kuiomba Serikali na taasisi zake mfano idara ya kazi kutukutanisha na waajiri wetu kumaliza kero zinazotukabili ..’ Alisema 

Aidha Mhe Dkt Mabula akaunga mkono juhudi za chama hicho katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Covid-19 kwa kukabidhi barakoa 400 zitakazovaliwa na madereva na makondakta ili kujikinga na ugonjwa wa Covid-19, Pamoja  kutoa  kompyuta moja kwaajili ya utekelezaji wa shughuli za kila siku za chama hicho.

Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha madereva (MWAREDDA) mkoa wa Mwanza Ndugu  Mjalifu Kezilaabi Manyasi amemshukuru mbunge huyo kwa kujitoa kwake katika kutekeleza shughuli za maendeleo na utatuzi wa kero za wananchi huku akimuomba kuendelea kufanya hivyo, Wakati katibu wa chama hicho Ndugu Samson Matayo akitaja changamoto mbalimbali zinazokabili chama chao ikiwemo ukosefu wa bima ya afya, mshahara mdogo, kuachishwa kazi bila kufuata taratibu za kisheria, ukosefu wa mikataba ya kazi na upungufu wa vitendea kazi kama kompyuta na shajara.

Uzinduzi wa kampeni ya uvaaji barakoa kwa wasafirishaji na wasafiri mkoa wa Mwanza ulipambwa na shughuli ya ugawaji bure barakoa zaidi ya 1,200 kwa wananchi na wasafirishaji zoezi lililoongozwa na mbunge huyo wa jimbo la Ilemela akishirikiana na wauzaji wa mafuta kutoka kituo cha mafuta Munuo.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com