METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, February 6, 2026

BALOZI MWAMWETA NA MHE. MTAKA WASAKA SOKO LA PARACHICHI UJERUMANI

 

 Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani, Mhe. Hassani Iddi Mwamweta anaongoza ujumbe wa wakulima na wafanyabiashara kutoka Tanzania unaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Matunda na Mbogamboga ya Fruit Logistica 2026 yanayofanyika Berlin kuanzia Februari 03 hadi 06, 2026.

Ujumbe huo unajumuisha Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Bw. Saleh Saad Mohamed unatumia maenesho hayo kupata fursa ya kutanua masoko kwa kuongeza masoko mapya, kuongeza mtandao wa wafanyabiashara na kujifunza maarifa mapya kuhusu kilimo-biashara.

Kampuni zaidi ya 40 kutoka Tanzania kwa kushirikiana na Taasisi za TAHA, Mamlaka ya Udhibiti Nafaka na Mazao mchanganyika (COPRA) na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) wameshiriki Maonesho hayo ambayo yamehudhuriwa na kampuni zaidi ya 2600 kutoka nchi 151 duniani.

Fruits Logistica ni Maonesho ya Kimataifa ya Matunda na Mbogamboga ambayo huwaleta pamoja wakulima, wasambazaji, wanunuzi, wasafirishaji na wadau mbalimbali katika mnyororo wa usambazaji wa matunda na mbogamboga kutoka duniani kote.









Share:

Tuesday, January 6, 2026

VYUO VIKUU VYAZINDUA MRADI WA KIMKAKATI KUKABILI MSONGO WA MAWAZO KWA VIJANA

 

‎Na. Meleka Kulwa- Dodoma.

‎Katika hatua inayotajwa kuwa mwanga mpya kwa vijana wanaokabiliwa na changamoto za afya ya akili, Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kimezindua rasmi mradi wa u’GOOD TevuAfya, unaolenga kushughulikia kwa vitendo matatizo ya afya ya akili kwa vijana, hususan wanaoishi mijini na pembezoni mwa miji.

‎Uzinduzi wa mradi huo umefanyika Januari 6, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Afrika Mashariki, ukihusisha viongozi wa chuo, watafiti, wadau wa maendeleo pamoja na wanafunzi.

‎Akizungumza katika hafla hiyo, Makamu Mkuu wa UDOM, Profesa Lughano Kusiluka, amesema mradi wa u’GOOD TevuAfya ni miongoni mwa miradi 23 ya kimataifa inayotekelezwa chini ya programu ya Good Life, huku miradi minane ikitekelezwa Tanzania.

‎“Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa Tanzania inaendelea kujijengea heshima na nafasi muhimu katika ramani ya utafiti wa kisayansi duniani,” amesema Profesa Kusiluka.

‎Ameeleza kuwa ushindani wa kupata ufadhili wa miradi ya utafiti ni mkali, hivyo mafanikio ya watafiti wa Tanzania kupata miradi hiyo yanaonesha ubora wa kazi na umuhimu wa tafiti zinazolenga kutatua matatizo halisi ya jamii.

‎Kwa mujibu wa Profesa Kusiluka, changamoto za afya ya akili kwa vijana zimeongezeka kwa kasi kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo hali ngumu za kiuchumi, mabadiliko ya mifumo ya kifamilia, msongo wa mawazo, matumizi makubwa ya mitandao ya kijamii pamoja na kasi ya maendeleo ya teknolojia za kidijitali.

‎“Afya ya akili si tatizo la vijana pekee, ni suala la jamii nzima. Familia, wazazi na mazingira yanayowazunguka vijana vina mchango mkubwa,” amesema, akisisitiza umuhimu wa tafiti shirikishi zitakazosaidia kupata suluhisho endelevu.

‎Aidha, ametoa wito wa kuimarishwa kwa elimu ya uraia kwa vijana ili kuwajengea uzalendo, kujiamini na kuiona Tanzania kama nchi ya fursa na matumaini, akibainisha kuwa misingi ya maadili na utambulisho wa kitaifa ina mchango mkubwa katika ustawi wa afya ya akili.

‎Kwa upande wa wanafunzi, Akley Omary wa UDOM amesema afya ya akili ni uwezo wa mtu kukabiliana na mawazo chanya na hasi yanayotokana na changamoto za maisha na mazingira ya kijamii.

‎Amesema wanafunzi wengi hukumbwa na msongo wa mawazo unaotokana na changamoto za kifedha, matatizo ya kifamilia na mazingira magumu ya masomo, huku kukosa mahitaji muhimu kama chakula, vifaa vya masomo na fedha za matumizi vikizidi kuathiri ustawi wao wa kisaikolojia.

‎Naye David Julius, mwanafunzi wa Shahada ya Business Information System, amesema dhana potofu kwamba afya ya akili ni sawa na wazimu imekuwa kikwazo kikubwa kwa vijana kutafuta msaada.

‎“Afya ya akili ni uwezo wa mtu kufanya maamuzi sahihi na kuchanganua mambo kwa ufanisi, kufeli masomo na kushindwa kufanya maamuzi sahihi mara nyingi hutokana na msongo wa mawazo,” amesema.

‎Kwa upande wake, Rebeca Omari Kabanda, mwanafunzi wa Information Security Engineering, amesema ukosefu wa ajira ni moja ya changamoto kubwa zinazowaathiri vijana kisaikolojia, hasa pale matarajio ya maisha baada ya kuhitimu yanapogonga mwamba.

‎Ameongeza kuwa matumizi sahihi ya TEHAMA na mitandao ya kijamii yanaweza kuwa nyenzo muhimu ya kutoa elimu na msaada wa kisaikolojia kwa vijana, akisisitiza umuhimu wa kujiepusha na tabia hatarishi na mahusiano yasiyo rasmi yanayoweza kuathiri afya ya akili na maendeleo ya kielimu.

‎Mradi wa u’GOOD TevuAfya unatarajiwa kutoa mapendekezo ya kisera pamoja na mbinu za vitendo zitakazosaidia kuboresha afya ya akili kwa vijana na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla hatua inayotajwa kuwa muhimu katika kujenga taifa lenye vijana wenye afya njema ya mwili na akili.

Share:

Friday, January 2, 2026

Wednesday, December 31, 2025

EWURA YAWANOA WAANDISHI WA HABARI KUHUSU ELIMU YA UDHIBITI WA HUDUMA

 

Na Mwandishi Wetu- Dodoma 

Wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Dodoma, leo 31 Desemba 2025, wameishukuru Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kuwapa mafunzo kuhusu udhibiti wa huduma za nishati na maji.

‎Mwenyekiti wa klabu hiyo, Musa Yusuf, ameipongeza EWURA kwa hatua ya kutoa mafunzo hayo, akibainisha umuhimu wa mkataba wa huduma kwa wateja, uvunaji wa maji ya mvua, na utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesisitiza kuwa elimu waliyoipata wataitumia kwa kuelimisha umma.

‎“Asanteni sana EWURA kwa elimu hii, hakika imetufungua macho. Wenzangu wote ni mashahidi. Tunaomba mafunzo kama haya yaendelee,” amesema Bw. Yusuf.

‎Kwa upande wake Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuelewa masuala yanayodhibitiwa na EWURA, kwani yanagusa huduma ambazo kila mwananchi kwa namna moja au nyingine anazitumia.

‎“Ninyi waandishi wa habari ni daraja kati ya EWURA na wananchi, tuendelee kushirikiana katika kuelimisha umma ili kila mtumiaji wa huduma tunazodhibiti ajue haki na wajibu wake”. Amesisitiza Mwakalosi.


Share:

MAKAMU WA RAIS ATOA POLE MSIBA WA BI LAURENCIA MABELLA

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amefika nyumbani kwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ndugu. Leonard Qwihaya, Mbezi Beach Jijini Dar es Salaam, kutoa pole kufuatia kifo cha Mama mzazi wa Qwihaya Bi. Laurencia Shija Mabella.



Share:

DKT. NATU APONGEZA UBUNIFU NA UBORA WA JARIDA LA HAZINA YETU

 

Na. Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, amepongeza ubunifu na ubora wa Jarida la Hazina Yetu Toleo la Tano ambalo limeandaliwa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini cha Wizara ya Fedha.

Ametoa pongezi hizo wakati akipokea Jarida hilo kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mwamba alisema Jarida hilo ambalo limeendela kuwa bora na kufika kila mahali duniani kwa njia ya kidigitali ni nyenzo muhimu katika kuwasilisha taarifa sahihi, za wazi na kwa lugha inayoeleweka kuhusu shughuli, mafanikio na mipango ya Wizara ya Fedha.

Dkt. Mwamba alipongeza jitihada za Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kwa kuendelea kuboresha mawasiliano na uelimishaji kwa umma pamoja na ubunifu na weledi unaooneshwa katika uandaaji wa Jarida hilo, akibainisha kuwa limeendelea kuwa chombo muhimu cha kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya fedha na uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Bw. Benny Mwaipaja alisema kuwa Jarida la Hazina Yetu linalenga kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Fedha pamoja na mchango wake katika maendeleo ya Taifa, akiahidi kuendelea kuliboresha ili liwe chombo chenye tija zaidi katika mawasiliano ya serikali.

Jarida la “Hazina Yetu Toleo la Tano” limesheheni maarifa mbalimbali kupitia Makala bora kabisa, habari, matukio ya picha na matangazo mbalimbali na linapatikana kwa njia ya nakala ngumu (hard copies) na nakala tete (soft copies) kupitia mitandao ya kijamii ya Wizara na wadau wengine wa habari pamoja na Tovuti ya Wizara ya Fedha www.mof.go.tz 


Share:

Saturday, December 20, 2025

DKT. MWIGULU AKAGUA HALI YA BANDARI YA BARAZANI MKOANI LINDI

 

Na Mwandishi Wetu- Lindi

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Mchemba leo Desemba 21, 2025 amekagua hali ya bandari ya Barazani mkoani Lindi na kuiagiza Mamlaka ya Bandari Tanzania kukamlisha kwa haraka michakato ya awali ya kitaalam ya ujenzi wa mradi wa Bandari ya Ngongo wilayani Lindi mkoani Lindi.‎

‎Amesema kukamilika kwa bandari ya Ngongo kutasaidia kuwaondolea adha watumiaji wa bandari inayotumika sasa ya Barazani ambayo hali yake haiendani na mahitaji ya sasa.‎

‎Dkt. Mwigulu ameongeza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa bandari ya Ngongo kutaleta chachu ya maendeleo mkoani humo kwani bandari ya Lindi imeanza kuchangamkiwa na wafanyabiashara, wakiwemo wa nchi jirani.

Share:

Tuesday, December 16, 2025

MRADI WA SHILINGI MILIONI 120 WA VYOO VYA KISASA KUBORESHA USAFI NA AFYA MINADA YA BAHI NA KIGWE

 

 Na Meleka Kulwa – Dodoma

‎Mkurugenzi wa Miradi wa Habitat for Humanity Tanzania, John Massenza, amesema ujenzi wa vyumba vya vyoo vya kisasa katika minada ya Bahi na Kigwe utakapokamilika, utaimarisha mazingira ya biashara, afya, na usafi kwa wafanyabiashara pamoja na wananchi wanaotumia minada hiyo wilayani Bahi, jijini Dodoma.

‎Ziara ya kukagua na kukabidhi maeneo ya ujenzi ilifanyika Desemba 16, 2025, ambapo John Massenza amekabidhi rasmi maeneo ya miradi hiyo kwa wahandisi watakaotekeleza ujenzi wa vyumba vya vyoo katika minada ya Bahi na Kigwe.

‎Amesema kuwa katika mradi huo, kutajengwa majengo ya vyoo pamoja na miundombinu rafiki kwa wanawake, ikiwemo jengo maalumu litakalowawezesha wakina mama kujisitiri wanapokuwa na mahitaji maalumu.

‎Aidha, amesema kuwa katika minada ya Bahi na Kigwe kutajengwa jumla ya vyumba 26 vya vyoo, vikiwemo vyumba 10 kwa wanaume na 16 kwa wanawake, pamoja na tanki la maji kwa kila mradi. Miradi hiyo pia itajumuisha chumba maalumu cha mahitaji ya wanawake, bafu, chumba cha wakina mama wanaonyonyesha, pamoja na ofisi ya wasimamizi wa huduma.

‎Amebainisha pia kuwa vyumba viwili kwa kila mradi vitajengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu katika minada ya Bahi na Kigwe.

‎Aidha, amebainisha kuwa mradi wa ujenzi wa vyumba vya vyoo katika Mnada wa Bahi utagharimu shilingi milioni 60, huku mradi wa Mnada wa Kigwe ukigharimu shilingi milioni 60 pia. Miradi hiyo inatarajiwa kunufaisha zaidi ya watu 4,000 pindi itakapokamilika.

‎Katika mpango wa uendeshaji wa huduma hizo, amesema kuwa watumiaji wa vyoo watalipia huduma hiyo kwa lengo la kugharamia matengenezo, uendeshaji wa mradi pamoja na kuboresha makazi ya wananchi na kuinua vipato vyao.

‎Amebainisha kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuboresha afya na ustawi wa jamii, kuongeza kipato, na kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja kupitia mazingira bora ya biashara na huduma.‎

‎Habitat for Humanity inafanya kazi katika nchi 70 duniani, huku makao makuu yake yakiwa nchini Marekani. Aidha, Massenza amesema kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada za taasisi hiyo katika kuboresha huduma za vyoo na usafi wa mazingira katika maeneo ya minada na jamii kwa ujumla.

‎Katika ziara hiyo, Mkurugenzi wa Habitat for Humanity Tanzania, John Massenza, aliambatana na viongozi wa serikali ya kijiji na mtaa pamoja na maafisa mazingira kutoka Wilaya ya Bahi.

‎Awali, mhandisi wa mradi alisema kuwa tanki la maji litakuwa na ujazo wa lita 3,000, kwa Kila tank litakalokuwepo kwenye miradi hio, huku akibainisha kuwa ujenzi wa majengo hayo ukitarajiwa kuchukua wiki 8 hadi 10, na kwamba mradi mzima unatarajiwa kukamilika ndani ya siku 90.


















Share:

Sunday, December 14, 2025

WAZIRI MKUU: WATANZANIA TUNZENI AKIBA YA CHAKULA

 


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania watunze akiba ya chakula walichonacho na waepuke matumizi yasiyofaa kutokana na hali ya kuchelewa kwa msimu wa mvua.

Waziri Mkuu ametoa wito huo leo jioni (Jumapili, Desemba 14, 2025) wakati akizungumza na baadhi ya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma.

Amewaeleza viongozi hao kutoka mikoa ya Dodoma na Singida kwamba Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitoa utabiri wa mwelekeo wa msimu wa mvua za vuli na mvua za msimu kwa kipindi cha Oktoba 2025 hadi Desemba 2025 na kipindi cha mwezi Novemba, 2025 hadi Aprili 2026 mtawalia.

“Kutokana na utabiri huo, baadhi ya mikoa nchini inatarajiwa kuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na kutawaliwa na vipindi virefu vya ukavu na mtawanyiko wa mvua usioridhisha,” amesema.

Amesema tathmini hiyo ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaonesha hali ya kuchelewa kwa mvua inatarajiwa katika maeneo ya mikoa ya Dodoma, Katavi, Kigoma, Singida, Tabora, Iringa, Mbeya, Mtwara, Njombe, Songwe, Rukwa, Ruvuma pamoja na Kusini mwa Mkoa wa Morogoro.

“Pamoja na kuwa hakuna tishio la uhaba wa chakula kutokana na hifadhi ya chakula iliyopo nchini, lakini ni vema, wananchi waendelee kuzingatia matumizi sahihi ya chakula. Tuna akiba ya chakula ya kutosha lakini ninawasihi wananchi waweke akiba na kuepuka matumizi yasiyo ya lazima,” amesema.

Ametumia fursa hiyo kuwakumbusha wakulima waandae mashamba kwa wakati na watumie pembejeo zinazoendana na upatikanaji wa mvua chache sambamba na kuzingatia ushauri wa wataalamu wa kilimo ambao kwa sasa wanazunguka nchi nzima kukutana na wakulima na kutoa elimu.

Vilevile, Dkt. Mwigulu amewataka wafugaji wote waweke mipango mizuri ya matumizi na uhifadhi wa maji na vyakula vya mifugo ili kukabiliana na hali hiyo.

Waziri Mkuu amewasisitiza Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wahakikishe maafisa ugani wanawatembelea wakulima na kutoa ushauri ikiwemo matumizi sahihi ya mbegu kulingana na hali ya hewa badala ya kukaa ofisini muda wote.

“Vilevile, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri endeleeni kuhamasisha wakulima wajisajili kwenye daftari la mkulima na kuhakikisha wanapata namba za usajili,” amesisitiza

Amewataka viongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) zihakikishe kuwa shehena za pembejeo zinahudumiwa kwa wakati ili usambazaji ufanyike kwa ufanisi.

Share:
Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com