Na Mathias Canal, WAZOHURU MEDIA
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa– TAMISEMI inatekeleza Mradi wa Kuboresha Elimu ya Sekondari - SEQUIP) Tanzania Bara. Lengo kuu la mradi ni kuhakikisha mazingira ya kufundishia na kujifunzia yanaboreshwa katika shule za Sekondari kuanzia Kidato cha Kwanza hadi cha Sita kwa kipindi cha miaka mitano (5) kuanzia Mwaka wa fedha 2020/2021 hadi 2025/2026.
Mradi huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia kwa mkopo wa masharti nafuu wa kiasi cha Dola ZA Kimarekani milioni 500 sawa na takribani kiasi cha Shilingi Trilioni 1.2.
Utekelezaji wa mradi huu umejikita katika Malengo mahususi ambayo ni pamoja na Kuongeza fursa ya upatikanaji wa Elimu ya Sekondari; Kuweka mazingira salama ya Elimu kwa wasichana waliopo katika Shule za Sekondari; na Kuhakikisha wanafunzi wote wanaoanza masomo ya sekondari wanamaliza Elimu ya Sekondari.
Hata hivyo utekelezaji wa shughuli za mradi umejikita katika maeneo makuu manne ambayo ni: Kujenga uwezo wa wanafunzi wote hususani wanafunzi wa kike kupata Elimu ya Sekondari na stadi za Maisha; Kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji na matumizi ya teknolojia ya kidijitali (TEHAMA); Kuongeza upatikanaji wa Elimu ya Sekondari na kupunguza vikwazo kwa wanafunzi wa kike; na Ufuatiliaji, tathmini na uendeshaji wa mradi.
Serikali katika ya mwaka wa fedha wa 2021/22 hadi 2024/2025 Kupitia Mradi wa SEQUIP imewekeza katika shughuli mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya shule za Sekondari ili kuboresha mazingira ya Kujifunzia na kufundishia. Hadi kufikia Machi, 2025, Jumla ya shilingi Bilioni 767.23 zimetumwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za ujenzi wa miundombinu ya shule za sekondari.
Shughuli zinazotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa shule mpya za sekondari 830 zikiwemo shule mpya ngazi ya Kata 694 ,shule mpya za sekondari za bweni za wasichana za Mikoa 26, shule mpya za Amali 103 na shule za bweni za Wavulana 7.
Aidha, fedha hizo zimetumika katika ujenzi wa mabweni ya wanafunzi 625, vyumba vya madarasa 1,499, matundu ya vyoo 4,836, Umaliziaji wa Maabara za sayansi 132, ujenzi nyumba za walimu 459, ujenzi wa mabwalo 3, samani zinazohusisha viti na meza 60, vitanda 123 na ukarabati wa shule chakavu 5.
UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA KATA JENZI wa shule Mpya za
Ujenzi wa shule mpya za sekondari za Kata umefanyika kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha wa 2021/22 hadi 2024/25. Miundombinu iliyojengwa katika shule za sekondari za Kata ni pamoja na madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 3, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA na Matundu ya vyoo.
Jumla ya shilingi Bilioni 394,790,160,363.08 zimetumika katika ujenzi wa shule mpya 694 za sekondari za Kata ambapo kati ya hizo shilingi Bilioni 375,096,425,878.00 ni kutoka kwenye mradi wa SEQUIP na Shilingi Bilioni 19,693,734,485.08 zinatokana na mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa miradi ya awamu ya kwanza na ya pili. Shule hizi zimejengwa katika Halmashauri zote Tanzania Bara.
UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA AMALI
Kufuatia maboresho ya Mitaala ya Elimu Toleo la 2023, imeelekezwa kuanzishwa kwa shule za sekondari za amali zinazolenga kutoa masomo ya ujuzi kwa wanafunzi. Kutokana na maboresho hayo, shule mpya za Sekondari za Amali kwa ajili ya kutoa masomo ya ujuzi zinajengwa katika mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia mradi wa SEQUIP.
Jumla ya shilingi Bilioni 88,849,305,125.00 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya 103 za sekondari za Amali. Ujenzi wa shule hizi unafanyika kupitia utaratibu wa aina mbili ambazo ni ujenzi wa shule 29 za amali za kihandisi zinazojengewa miundombinu yote ikiwemo madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 2, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA, karakana, mabweni 4 na Matundu ya vyoo kwa gharama ya shilingi 46,400,000,000.00 ambayo ni sawa na shilingi Bilioni 1.6 kwa kila shule.
Ujenzi wa Shule 74 za sekondari za amali zisizo za kihandisi zinajengwa kwa gharama ya shilingi Bilioni 42,449,305,125.00 Shule hizi zinajengewa miundombinu ya awamu ya kwanza inayohusisha madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 2, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA na Matundu ya vyoo.
UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA BWENI ZA WAVULANA
Serikali iliamua kujenga shule mpya za Bweni za Wavulana katika Kanda saba nchini ambazo ni kanda ya Mashariki (Dar es Salaam, Pwani na Morogoro), Magharibi( Tabora, Kigoma, Katavi na Shinyanga), Kanda ya ziwa (Kagera, Mwanza, Simiyu, Geita na Mara), Kanda ya Kusini (Lindi, Mtwara na Ruvuma), Nyanda za juu Kusini (Iringa,Njombe, Mbeya, Songwe na Rukwa), Kanda ya kati (Dodoma na Singida) na kanda ya Kaskazini (Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga).
Jumla ya shilingi Bilioni 28,700,000,000.00 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa shule hizo mpya za wavulana za bweni ambapo kila shule imejengwa kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 4,100,000,000.
UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA BWENI ZA WASICHANA ZA MIKOA
Ujenzi wa shule za bweni za Wasichana za Mikoa umefanyika katika mikoa yote Tanzania Bara. Kila shule imejengwa kwa kiasi cha fedha cha shilingi Bilioni 4,100,000,000.00 ambapo shule moja imejengewa miundombinu ikiwemo vyumba vya madarasa 22, jengo moja la utawala, maabara 4, matundu 16 ya vyoo, chumba kimoja cha jenereta, bwalo moja, mabweni 9 ambapo mabweni 5 yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 120 kila moja na mabweni 4 yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 80.
UJENZI WA MIUNDOMBINU MINGINE YA SHULE ZA SEKONDARI
Pamoja na kujenga shule mpya za sekondari katika Mamlaka za Serikari za Mitaa, Mradi wa SEQUIP umefanikisha ujenzi wa miundombinu mingine ya shule. Miundombinu iliyojengwa ni pamoja na mabweni ya wanafunzi 625, vyumba vya madarasa 1,499, matundu ya vyoo 4,836, Umaliziaji maboma ya vyumba vya Maabara za sayansi 132, ujenzi nyumba za walimu 459, ujenzi wa mabwalo 3, samani zinazohusisha viti na meza 60, vitanda 123 na ukarabati wa shule chakavu 5. Jumla ya shilingi Bilioni 167,987,845,884.00 zimetumika.
SHULE SALAMA
Serikali ya Tanzania kupitia Mradi wa kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP) inatekeleza Mpango wa Shule Salama katika shule 3,303. Lengo ni kujenga uwezo wa walimu wa malezi, ushauri nasaha na wanafunzi kuhusu dhana ya Shule Salama na kuwezesha uundaji wa mazingira rafiki na salama kwa ajili ya ufundishaji na ujifunzaji, Kuimarisha mazingira ya ujifunzaji shuleni na kutoa fursa ya elimu bora, salama na jumuishi kwa kila mtoto bila ubaguzi na kusaidia wanafunzi kuwa katika mazingira salama ya kujifunza na kupambana na changamoto zinazoweza kusababisha kuacha masomo, Ujenzi wa shule za bweni za wasichana 26, ambao unachangia kupunguza changamoto za umbali na usalama kwa wanafunzi wa kike.
Wanafunzi 10,239 wa kike waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito wameweza kuendelea na shule kupitia elimu kwa njia mbadala (Altenative Education Pathway) na 4,706 waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali wameweza kurejea shuleni kupitia mifumo rasmi.
Kufuatia ujenzi wa miondombinu hii ambayo ni rafiki kwa wanafunzi imepelekea Kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wa kike wanaojiunga na Kidato cha Tano kutoka 24,637 mwaka 2020 hadi kufikia wananfunzi 67,304 mwaka 2024.
MAFUNZO YA TEHAMA, SAYANSI NA HISABATI
Katika Kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji kwa shule za sekondari za Serikali, serikali kupitia mradi wa SEQUIP imetoa mafunzo endelevu kazini kwa walimu 40,101 wanaofundisha masomo ya sayansi na hisabati. Mafunzo haya yamekuwa na tija kubwa sana katika maeneo makuu yafuatayo:
• Kuboresha kwa kiasi kikubwa ubora wa ufundishaji na ujifunzaji
• Kuongeza ufaulu na kuboresha matokeo ya wanafunzi
• Kuimarisha uelewa wa mtaala na mbinu za tathmini
• Kujenga uwezo wa kitaaluma na kitaalamu wa walimu
Vilevile, Jumla ya walimu 4,987 walishiriki katika mafunzo ya matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji, ikiwa ni sehemu ya lengo la jumla la kuwafikia walimu 5000 ndani ya muda wa utekelezaji wa mradi.
Katika kufanikisha utekelezaji wa mitaala, serikali kupitia mradi wa SEQUIP imechapa na kusambaza nakala 11,409,461 ya vitabu vya sekondari kwa masomo ya Sayansi, Hisabati na Amali.
Hatua kubwa zimepigwa katika kuboresha miundombinu ya kidijitali kwenye shule za sekondari Tanzania Bara. Jumla ya kompyuta 1,848 aina ya all-in-one, kompyuta mpakato moja (laptop) 231, projekta 231, skrini 231, na UPS 462 zimenunuliwa na kusambazwa katika shule 231, Pia serikali imenunulia na kusambaza Bao janja (Smart Boards) katika shule 422.
WANAFUNZI WALIORUDI SHULE
Jumla ya Wanafunzi 13,272 wa kike waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito wameweza kuendelea na shule kupitia elimu kwa njia mbadala (Altenative Education Pathway) na 4,706 waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali wameweza kurejea shuleni kupitia mifumo rasmi. Hadi kufikia mwaka 2024 Wanafunzi 721 walifanikiwa kufaulu kidato cha nne na kuchaguliwa kuendelea na masomo ambapo kidato cha tano walichaguliwa wanafunzi 467 na Vyuo vya Kati walichaguliwa wanafunzi 254.
Serikali inajivunia mafanikio mbalimbali katika utekelezaji wa mradi wa SEQUIP ambapo imefanikiwa Kuongeza fursa ya upatikanaji wa Elimu kwa kujenga shule karibu na makazi ya wanachi na katika maeneo ambayo hayakuwa na shule za sekondari, kuogeza nafasi za udahili kwa wanafunzi wa Kidato cha Kwanza kwa wahitimu wa elimu ya msingi na wanafunzi wa kidato cha Tano wanaofanya vizuri katika mitihani ya kidato cha nne, Kuondoa Msongamano wa wanafunzi katika shule za sekondari kutokana na kuongezeka kwa shule mpya, Kupunguza umbali wa wanafunzi wanaotembea kutoka katika makazi yao kufuata shule, Kuwaandaa wataalamu wa baadae katika tasnia ya sayansi na Teknolojia na ujuzi mbalimbali ambao watasoma na kupita katika shule mpya za sekondari, Kuimarisha Ulinzi na usalama wa wanafunzi kwa kuwawekea mazingira mazuri ya kujifunza na kuwaepusha na hatari zinazoweza kuwasababishia kukatisha masomo; na Kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
Ktika tafakuri na uandaaji wa makala hii kwa kina, nimetembelea mikoa yote nchini kujionea hatua zilizofikia za utekelezaji wa miradi kama ambavyo nimeainisha kwenye makala hii, nimezungumza na wananchi katika maeneo yote yanayozunguka mradi na kila mmoja kwa nafasi yake amezungumzia kuhusu manufaa ya mradi wa SEQUIP kama miongoni mwa miradi iliyogusa maisha yao na hususani wananchi wa kawaida kwa sababu umeelekezwa moja kwa moja katika kuboresha huduma za elimu.
Katika maeneo mengi ya vijijini ambako kulikuwa na upungufu wa shule za sekondari, wananchi wameeleza kuwa ujenzi wa shule mpya umepunguza umbali, Nami nakubaliana nao kabisa ni kweli umbali ambao wanafunzi walikuwa wakitembea kila siku kufuata masomo ni wazi sasa umepungua, wapo waliokuwa wanatumia umbali wa zaidi ya kilomita 8 kufuata shule zilipo lakini kwa sasa kwa sehemu kubwa mwanafunzi hawezi kutembea umbali wa kilomita zaidi ya 3 kabla ya kuifikia shule ilipo. Wazazi wengi katika maelezo yao wameonyesha wanaamini kuwa hatua hiyo imeongeza mahudhurio ya wanafunzi na kupunguza vitendo vya utoro vinavyotokana na safari ndefu za kwenda na kurudi shuleni.
Katika mikoa ya Singida, Tabora, Dodoma na Katavi, wananchi wameeleza kuwa ujenzi wa madarasa mapya, mabweni na nyumba za walimu umeimarisha mazingira ya kujifunzia na kufundishia. Baadhi ya wananchi ambao kwa sehemu ni wazazi wa wanafunzi wamewlwza kuwa hapo awali wanafunzi walikuwa wakisoma katika madarasa machache yenye msongamano mkubwa, lakini kupitia SEQUIP hali hiyo imeanza kupungua. Pia wamesema uwepo wa nyumba za walimu umechangia walimu wengi kuishi karibu na shule na hivyo kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu.
Katika mikoa ya Kanda ya ziwa ukimowemo mkoa wa Kagera, Geita, Mwanza na Mara, wananchi wamepongeza jitihada za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuanzisha utekelezaji wa mradi huo kwani umekuwa sehemu ya kuimarisha sekta ya elimu hususani masomo ya Sayansi kwa kuboresha maabara za sayansi na upatikanaji wa vifaa vya kufundishia.
Wazazi na wananchi hao wanaamini kuwa uwekezaji huo utasaidia kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika masomo ya Sayansi na Hisabati ambayo kwa muda mrefu yalikuwa yakikabiliwa na changamoto za vifaa na miundombinu. Wazazi na viongozi wa jamii wameeleza kuwa maendeleo hayo yanaweka msingi mzuri wa kuandaa wataalamu wa baadaye katika sekta mbalimbali za maendeleo.
Kwingineko katika mkoa wa Pwani, Lindi, Mtwara, na Ruvuma wananchi wameeleza kuwa mradi huo utakuwa kichocheo kikubwa kwani umeleta manufaa ya kiuchumi kwa jamii zinazozunguka shule zilizojengwa au kuboreshwa. Wakati wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi, vijana wengi walipata ajira za muda katika shughuli za ujenzi, usafirishaji wa vifaa na huduma nyingine zinazohusiana na miradi hiyo. Hali hiyo imeongeza mzunguko wa fedha katika maeneo husika na kutoa fursa za kipato kwa wananchi wa kawaida. Wapo vijana waliotoa ushuhuda kuhusu mafanikio waliyoyapata ikiwemo kufunga ndoa, ujenzi wa nyumba za kuishi na za biashara, ufunguzi wa miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa Lodge, miradi ya ufugaji nyuki na ufugaji wa Ng’ombe wa maziwa sambamba na miradi ya maduka pamoja na ununuzi wa pikipiki kwa ajili ya kazi za Bodaboda.
Kwa upande wa mikoa ya Kanda ya kaskazini ambayo ni Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga, wananchi wameeleza kwa namna chanya juhudi za mradi wa SEQUIP katika kuongeza fursa za elimu kwa wasichana. Wengi wanaamini kuwa uwekezaji katika mabweni, mazingira salama ya kujifunzia na programu za kuwasaidia wanafunzi waliokatisha masomo kurejea shuleni umeongeza usawa katika upatikanaji wa elimu. Baadhi ya viongozi wa dini na jamii wamekuwa wakihimiza familia kutumia fursa hizo kuhakikisha watoto wa kike wanamaliza elimu yao bila vikwazo.
Hata hivyo, pamoja na mafanikio hayo, wananchi katika baadhi ya maeneo wameeleza matarajio yao ya kuona mradi huo ukiendelea kuimarishwa kwa kuongeza idadi ya walimu, vifaa vya kufundishia na huduma za teknolojia katika shule mpya zilizojengwa. Wanaamini kuwa miundombinu bora pekee haitoshi bila kuwa na rasilimali watu na vifaa vinavyokidhi mahitaji ya wanafunzi. Kwa ujumla, maoni ya wananchi kutoka mikoa mbalimbali yanaonesha kuwa SEQUIP imeleta mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu na imekuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo mengi nchini.
Ama kwa hakika, haya ni mafanikio makubwa ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan inajivunia kwa kutumia njia mbalimbali ikishitrikiana na Wadau wa Maendeleo katika kuimarisha Sekta ya Elimu nchini na kuwaletea wananchi wake maendeleo.
Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan inajivunia Mradi wa SEQUIP kama alama ya maendeleo, urithi wa kizazi kijacho, na nguzo ya uchumi wa viwanda kupitia elimu watakayoipata wanafunzi. Mradi huu ni mfano wa kujitegemea, uzalendo, na dira ya maendeleo ya Taifa kwa kutumia rasilimali za ndani.
Tanzania sasa imeandika historia. Kwa fedha zetu wenyewe, kwa wataalamu wetu, na kwa moyo wetu, Kukamilika kwa Mradi wa SEQUIP si tu itaboresha elimu ya Tanzania na vizazi vijavyo bali ni ushindi wa watanzania wote.
MWISHO
.jpeg)

.jpeg)






