METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, September 12, 2026

TANZANIA NA DRC CONGO WAFUNGUA UKURASA MPYA WA USHIRIKIANO KWENYE MADINI

▪️Waziri Mavunde na Waziri Kabamba wakubaliana msingi wa ushirikiano,

▪️Ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Samia na Rais Tshisekedi ya ushirikiano baina ya nchi hizo mbili,

▪️Ushirikiano walenga kurahisisha usafirishaji na biashara ya madini,

▪️Wakubaliana kuweka mikakati ya pamoja kuimarisha ufuatiliaji wa uzalishaji wa madini (traceability),

TIANJIN, CHINA

Pembezoni mwa Mkutano wa Madini wa China uliofanyika Jijini Tianjin, Waziri wa Madini *Mhe. Anthony Mavunde* amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Madini wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), *Mheshimiwa Louis Watum Kabamba* yaliyolenga kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kwenye sekta ya madini.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika tarehe 11 Septemba, 2026 Waziri Mavunde na mwenzake Mhe. Kabamba walijadiliana kwa kina namna ya kuendeleza sekta ya madini baina ya Nchi zao na hatimaye kuweka msingi ambao utakuwa ni mwanzo wa kuimarisha ushirikiano utakaoleta tija kwa pande zote mbili.

"Leo tumekutana hapa si kwa bahati mbaya, haya ni matokeo ya maelekezo ya viongozi wetu *Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan* na *Mhe. Felix Tshekedi* ya kwamba Nchi zetu ni muda muafaka wa kuimarisha ushirikiano kwenye sekta ya madini kwani tunahitajiana na kutegemeana hususan katika masuala ya usafirishaji wa madini" 

"Viongozi wetu wameshatuwekea msingi, sisi kazi yetu ni kuhakikisha tunayaishi maono yao na kuimarisha ushirikiano ambao utakwenda kuongeza tija na kuboresha sekta zetu za madini kuanzia uzalishaji mpaka biashara na uongezaji thamani madini" alisisitiza Waziri Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa ushirikiano baina ya Kongo DRC na Serikali ya Jamhuri ya Tanzania umelenga kwa kiasi kikubwa kurahisisha ufanyaji wa biashara na usafirishaji wa madini kwa maslahi mapana ya Nchi zetu.

Vilevile, Mavunde alieleza kuwa kwa sasa ni vyema Tanzania na DRC wakaweka mikakati ya pamoja na kuisimamia kwa lengo la kuimarisha ufuatiliaji wa mnyonyoro wa uzalishaji wa madini kuanzia yanapochimbwa mpaka yanapouzwa au kusafirishwa kwenda nje (traceability).

Naye, Waziri wa Madini wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), *Mhe. Louis Kabamba* alishukuru kwa kukutana na mwenzake na kuahidi kuwa, kwa namna yeyote ni vyema kuyaishi maono ya Viongozi wakuu wa Mataifa haya ili kuleta manufaa yanayotarajiwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Aliendelea kusisitiza kuwa ushirikiano baina ya Tanzania na DRC pia utasaidia kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza sekta ya madini hususani katika kuwezesha uchimbaji mdogo na kuongeza mapato ya Serikali, hatua ambayo kwa DRC bado wachimbaji wadogo wanachangia kiasi kidogo. Pia, Mhe. Kabamba alisifu maendeleo ya STAMICO na kuomba uzoefu wao usaidie kuimarisha Shirika la Madini la Kongo ili liweze kuzalisha na kujiendesha kwa faida.




Share:

Sunday, August 16, 2026

TIB YAUNGA MKONO AJENDA YA NISHATI SAFI KUELEKEA DIRA 2050


 Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akimkabidhi Tuzo pamoja na Cheti, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo TIB, Bw. Deogratius Kwiyukwa, kama Ishara ya kutambua mchango wa benki hiyo katika kushiriki kukuza na kuchochea shughuli za uchuki jumuishi na shukrani kwa ushiriki na kuwa tayari kuchochea maono ya Taifa ya kumkomboa mwananchi kwa kumtengenezea mazingira bora ya uwajibikaji kwa Taifa lake, katika Kilele cha Tamasha la Kizimkazi 2026, lililohitimishwa mwishoni wa Juma lililopita.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha, Kizimkazi, Zanzibar)

Na Benny Mwaipaja, Kizimkazi-Zanzibar

Safari ya mageuzi ya kiuchumi kuelekea Dira ya Taifa 2050 imeanza kushika kasi, huku mijadala kuhusu vichocheo vya uchumi ikiendelea kupewa uzito mkubwa nchini.

Miongoni mwa matukio yaliyoibua mjadala huo ni Tamasha la Kizimkazi 2026, lililofanyika kusini mwa Unguja na kukutanisha viongozi wakuu wa serikali, taasisi na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Tamasha hilo lilihudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais Dkt. Emmanuel John Nchimbi, pamoja na Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, sambamba na viongozi wengine wa serikali akiwemo Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), vyama vya siasa, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Mbali na kuwa jukwaa la kukutanisha wadau, tamasha hilo pia lilikuwa sehemu muhimu ya mdahalo wa kitaifa kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, ambapo viongozi waandamizi walitoa maoni yao kuhusu umuhimu wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi kama sehemu ya maendeleo endelevu ya taifa.

Ajenda ya nishati safi inaenda sambamba na nguzo ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, ambayo ni sehemu ya msingi ya Dira 2050.

Kupitia nguzo hiyo, Tanzania inalenga kuwa kinara wa kimataifa katika uhifadhi wa mazingira kwa kusimamia matumizi endelevu ya rasilimali za asili na kuimarisha uwezo wa taifa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Miongoni mwa taasisi zilizojitokeza kwa nguvu katika tamasha hilo ni Benki ya Maendeleo TIB, iliyoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Bw. Deogratius Kwiyukwa. TIB ni benki ya maendeleo ya Serikali iliyoanzishwa mahsusi kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini kupitia utafutaji wa mitaji, uandaaji wa miradi ili iweze kuvutia uwekezaji, pamoja na usimamizi wa mifuko ya maendeleo kwa niaba ya serikali na sekta binafsi.

Akizungumza na waandishi wa habari kando ya tamasha hilo, Bw. Kwiyukwa alisema

Benki ya Maendeleo ya Tanzania TIB, imejipanga kuongeza ufadhili wa miradi ya nishati safi nchini, kama sehemu ya jitihada za Taifa za kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema benki hiyo imetenga fedha maalum za kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa miradi ya nishati mbadala ikiwemo ya jua, upepo, gesi asilia na nishati ya maji.

“Tunafahamu kuwa nishati safi ndio mkombozi wa viwanda, kilimo na nyumba za Watanzania. Kupitia ufadhili huu tunalenga kupunguza utegemezi wa nishati chafu na kuchochea uchumi wa kijani,” amesema Bw. Kwiyukwa.

Kwa mujibu wa TIB, hatua hii pia inalenga kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kushiriki katika miradi mikubwa ya miundombinu ya nishati, ambayo itasaidia kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ajira kwa vijana.

“Benki ya Maendeleo ya TIB imekuwa na mchango mkubwa hapa nchini katika kuleta mabadiliko chanya katika ukuaji wa sekta mbalimbali. Kupitia tamasha hili la Kizimkazi, tunaungana na Mheshimiwa Rais na wadau wengine kupambanua na kuonesha mchango wa sekta zote kufikia malengo ya Dira,” alisema.

Alieleza kuwa benki hiyo imejikita katika sekta mbalimbali muhimu ikiwemo miundombinu, nishati, utalii, uchumi wa buluu, vijana na wanawake, pamoja na utunzaji wa mazingira.

Kwa mujibu wa Bw. Kwiyukwa, TIB pia inasimamia mifuko mbalimbali ya maendeleo kwa niaba ya serikali na taasisi nyingine, ikiwemo mifuko ya maji, umeme vijijini, na nishati safi, katika Tanzania Bara na Zanzibar.

Alisema dhamira kuu ni kufikisha maendeleo kwa wananchi na kupunguza vihatarishi katika maeneo ambayo benki za biashara hushindwa kuyafikia.

Katika hatua nyingine, TIB kupitia kampuni yake tanzu ya TIB Rasilimali, imeendelea kufungua njia mbadala za upatikanaji na ukuzaji wa mitaji. Kampuni hiyo ni miongoni mwa mawakala wakubwa wa soko la hisa la Dar es Salaam, ikiwa na jukumu la kuuza na kununua hisa kwa niaba ya taasisi na watu binafsi. Pia hutoa huduma za elimu ya fedha, uwekezaji, pamoja na uwakala wa bima.

Bw. Kwiyukwa alisema kupitia TIB Rasilimali, taasisi na wananchi wamekuwa wakihamasishwa kutambua njia mbadala za kukuza mitaji yao bila kutegemea fedha za Serikali pekee.

Alibainisha kuwa Ofisi za Dar es Salaam na majukwaa ya mitandaoni zimekuwa zikiendesha madarasa maalumu ya kila wiki, hasa kwa vijana, ili kuwapa uelewa kuhusu njia salama na za uhakika za uwekezaji.

“Jitihada hizo zinaunga mkono malengo makubwa ya Dira 2050, yanayolenga kujenga uchumi wa thamani ya dola trilioni moja, kuongeza wastani wa kipato cha Mtanzania hadi dola 7,000 kwa mwaka, pamoja na kuhakikisha sekta binafsi inachangia kwa kiwango kikubwa zaidi katika ukuaji wa uchumi wa Taifa” alisema Bw. Kwiyukwa.

Sambamba na ushiriki wake katika tamasha hilo, Benki ya Maendeleo TIB pia ilitunukiwa tuzo na cheti kutoka kwa Mheshimiwa Rais kama ishara ya kutambua mchango wake na utayari wake wa kuchochea maono ya Taifa ya kumkomboa mwananchi kiuchumi kupitia maendeleo jumuishi.

Akihitimisha, Bw. Kwiyukwa aliipongeza Mwanamke Initiative Foundation (MIF) kwa kuandaa Tamasha la Kizimkazi, akieleza kuwa limefungua fursa pana kwa Watanzania kujadili masuala muhimu ya maendeleo. Pia aliahidi kuwa TIB itaendelea kushiriki katika matamasha na majukwaa mengine yenye lengo la kuchochea maendeleo ya Taifa.

Sambamba na hayo, katika Tamasha hilo la Kizimkazi 2026, Benki ya Maendeleo TIB ilitunikiwa tuzo pamoja na cheti na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama Ishara ya kutambua mchango wa benki hiyo katika kushiriki kukuza na kuchochea shughuli za uchuki jumuishi na shukrani kwa ushiriki na kuwa tayari kuchochea maono ya Taifa ya kumkomboa mwananchi kwa kumtengenezea mazingira bora ya uwajibikaji kwa taifa lake.

Kwa ujumla, ushiriki wa TIB katika Tamasha la Kizimkazi 2026 umeonesha wazi nafasi ya taasisi za maendeleo katika kusukuma mbele ajenda ya nishati safi, uhifadhi wa mazingira na uwezeshaji wa kiuchumi, yote ikiwa ni sehemu ya safari ya Tanzania kuelekea Dira 2050.


Share:

ULEGA: BARABARA YA KIBAONI–SITALIKE KUFUNGUA FURSA ZA KIUCHUMI KATAVI NA MAENEO JIRANI

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema kuwa ujenzi wa Barabara ya Kibaoni–Sitalike (km 70) ni muhimu katika kuchochea shughuli za kiuchumi na kufungua fursa za biashara katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, pamoja na kuimarisha mahusiano ya kiuchumi na nchi jirani.

Ulega ameyasema hayo mkoani Katavi wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Kibaoni–Sitalike, ambapo amesema Serikali itaendelea kuhakikisha inatenga na kutoa fedha kwa wakati ili kuwezesha utekelezaji wa mradi huo kukamilika kwa mujibu wa viwango na muda uliokusudiwa.

“Niwahakikishieni wananchi kuwa Mkandarasi anayejenga Barabara ya Kibaoni–Sitalike tutamlipa hivi karibuni ili aendelee na kazi. Serikali itaendelea kuhakikisha fedha zinapatikana ili mradi huu ukamilike,” amesema Ulega.

Amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutakuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, kuongeza fursa za biashara na kuunganisha maeneo ya uzalishaji na masoko, hivyo kuchochea maendeleo ya wananchi wa Katavi na mikoa jirani.

Aidha, Ulega amesema Serikali tayari imelipa Shilingi bilioni nne kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Mpanda–Kigoma, huku akimtaka Mkandarasi kuhakikisha anamalizia kwa haraka ujenzi wa Daraja la Mnyamasi ili kurahisisha matumizi ya barabara hiyo na kuzuia changamoto za mawasiliano wakati wa msimu wa mvua.

“Tunataka Daraja la Mnyamasi likamilike kwa haraka ili wananchi na watumiaji wengine wa barabara wasipate usumbufu wakati wa msimu wa mvua. Wasimamizi wa mradi wanapaswa kusimama imara na kuhakikisha kazi zinafanyika kwa kasi na ufanisi,” amesema Ulega.

Waziri huyo amesisitiza kuwa wasimamizi wa miradi wanapaswa kuhakikisha maeneo yote yanayokatisha mawasiliano wakati wa mvua yanapatiwa ufumbuzi wa kudumu, huku akielekeza kazi zifanyike kwa kasi bila kuathiri ubora wa miundombinu inayojengwa.

Awali, akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Kibaoni–Sitalike, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Katavi, Eng. Martin Mwakabende, amesema utekelezaji wa ujenzi wa kipande cha kwanza cha barabara hiyo umegawanywa katika sehemu tatu, huku gharama ya ujenzi ikiwa ni Shilingi bilioni 88.72.

Eng. Mwakabende amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya miundombinu ya barabara, akisema uwekezaji huo una mchango mkubwa katika kuchochea shughuli za kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi wa Mkoa wa Katavi na mikoa jirani.

Ujenzi wa Barabara ya Kibaoni–Sitalike ni miongoni mwa hatua zinazolenga kuimarisha mtandao wa barabara nchini, kurahisisha usafirishaji na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi katika maeneo yanayounganishwa na barabara hiyo.










Share:

GATI JIPYA LA ABIRIA BANDARI YA KIGOMA KUWA CHACHU YA BIASHARA NA USAFIRI KWA NJIA YA MAJI

Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, amesema ujenzi wa Gati Jipya la Abiria katika Bandari ya Kigoma utakuwa chachu ya kukuza biashara na kuimarisha usafiri kwa njka ya maji katika ukanda wa Ziwa Tanganyika

Prof. Mbarawa ameyasema hayo wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa gati hilo, ambalo linajengwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Japan kupitia ruzuku, huku ujenzi wake ukiwa umeanza tangu Juni,2025

Amesema mradi huo wenye thamani ya Shilingi bil. 53, utakapokamilika utaimarisha usafirishaji wa abiria na mizigo, kuongeza usalama wa huduma za usafiri kwa njia ya maji na kuchochea shughuli za kiuchumi katika mikoa ya Kigoma, Katavi, Rukwa, pamoja na nchi jirani

“Tunajenga meli, tunakabati bandari na tunajenga reli ili kuhakikisha mifumo yote ya uchukuzi inaunganishwa na kuleta tija kiuchumi,” amesema Prof. Mbarawa

Gati hilo litakuwa na urefu wa mita 130, upana mita 50, Mradi huo pia utahusisha ujenzi wa barabara yenye urefu wa mita 481 kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma hadi eneo la gati

Prof. Mbarawa amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya uchukuzi ili kuifanya Kigoma kuwa lango muhimu la biashara na shughuli za kiuchumi katika Ukanda wa Ziwa Tanganyika na Ukanda wa Maziwa Makuu

Kwa upande wake, Meneja wa Bandari za Ziwa Tanganyika, Bw. Ernest Mabula, amesema kukamilika kwa gati hilo kutaboresha ufanisi na usalama wa huduma za usafiri kwa njia ya maji, kuongeza usafirishaji wa abiria na mizigo na kukuza biashara katika ukanda huo

Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dkt. Rashid Chuachua, ameishukuru Serikali kwa uwekezaji huo, akisema gati hilo litachochea ukuaji wa uchumi, kuongeza fursa za biashara na kuboresha huduma za usafiri kwa wananchi.








Share:

Friday, June 26, 2026

Ziara ya Eng. Masaka Yatoa Mwelekeo Mpya wa Uzalishaji wa Mbegu ASA


















Na Mwandishi Wetu, Arusha

Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA), Eng. Innocent Masaka, amesema wakala huo umejipanga kuboresha mashamba yake ya uzalishaji wa mbegu yaliyopo katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa na kuyaendesha kwa mtazamo wa kibiashara ili kuongeza ufanisi wa uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora kwa wakulima.

Eng. Masaka ameyasema hayo Juni 26, 2026, alipofanya ziara katika Shamba la Mbegu za Kilimo la ASA Arusha–Ngaramtoni lenye hekta 450 za uzalishaji wa mbegu, kwa lengo la kujionea hali ya uzalishaji wa mbegu pamoja na maendeleo ya uboreshaji wa miundombinu mbalimbali inayotekelezwa katika shamba hilo.

Alisema maboresho hayo yataongeza uwezo wa mashamba ya ASA kuzalisha mbegu bora na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyohitajika, hatua itakayowezesha wakulima kupata mbegu kwa wakati na kwa bei nafuu. Aliongeza kuwa kuimarika kwa uzalishaji wa mbegu kutachochea ongezeko la tija katika sekta ya kilimo, kuinua kipato cha wakulima na kuchangia juhudi za Serikali za kuhakikisha usalama wa chakula nchini.

Aidha, Eng. Masaka alimpongeza Meneja wa Shamba la ASA Arusha–Ngaramtoni pamoja na watumishi wa shamba hilo kwa usimamizi mzuri na juhudi wanazozifanya katika kuendeleza uzalishaji wa mbegu bora. Aliwataka kuendelea kufanya kazi kwa weledi, ubunifu na uwajibikaji ili kuhakikisha ASA inaendelea kutekeleza jukumu lake la kuzalisha na kusambaza mbegu bora zinazokidhi mahitaji ya wakulima na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Share:

Sunday, May 31, 2026

MAPINDUZI YA ELIMU YASHIKA KASI: SERIKALI YAWEKA HISTORIA KUPITIA MRADI WA SEQUIP





Na Mathias Canal, WAZOHURU MEDIA

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa– TAMISEMI inatekeleza Mradi wa Kuboresha Elimu ya Sekondari - SEQUIP) Tanzania Bara. Lengo kuu la mradi ni kuhakikisha mazingira ya kufundishia na kujifunzia yanaboreshwa katika shule za Sekondari kuanzia Kidato cha Kwanza hadi cha Sita kwa kipindi cha miaka mitano (5) kuanzia Mwaka wa fedha 2020/2021 hadi 2025/2026.

Mradi huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia kwa mkopo wa masharti nafuu wa kiasi cha Dola ZA Kimarekani milioni 500 sawa na takribani kiasi cha Shilingi Trilioni 1.2.

Utekelezaji wa mradi huu umejikita katika Malengo mahususi ambayo ni pamoja na Kuongeza fursa ya upatikanaji wa Elimu ya Sekondari; Kuweka mazingira salama ya Elimu kwa wasichana waliopo katika Shule za Sekondari; na Kuhakikisha wanafunzi wote wanaoanza masomo ya sekondari wanamaliza Elimu ya Sekondari.

Hata hivyo utekelezaji wa shughuli za mradi umejikita katika maeneo makuu manne ambayo ni: Kujenga uwezo wa wanafunzi wote hususani wanafunzi wa kike kupata Elimu ya Sekondari na stadi za Maisha; Kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji na matumizi ya teknolojia ya kidijitali (TEHAMA); Kuongeza upatikanaji wa Elimu ya Sekondari na kupunguza vikwazo kwa wanafunzi wa kike; na Ufuatiliaji, tathmini na uendeshaji wa mradi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknlojia Mhe Prof Adolf Mkenda ameeleza kuwa hayo na kusisitiza kuwa Serikali katika ya mwaka wa fedha wa 2021/22 hadi 2024/2025 Kupitia Mradi wa SEQUIP imewekeza katika shughuli mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya shule za Sekondari ili kuboresha mazingira ya Kujifunzia na kufundishia. Hadi kufikia Machi, 2025, Jumla ya shilingi Bilioni 767.23 zimetumwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za ujenzi wa miundombinu ya shule za sekondari.

Shughuli zinazotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa shule mpya za sekondari 830 zikiwemo shule mpya ngazi ya  Kata 694 ,shule mpya za sekondari za bweni za wasichana za Mikoa 26, shule mpya za Amali 103 na shule za bweni za Wavulana 7.

Aidha, Prof Mkenda amesema fedha hizo zimetumika katika ujenzi wa mabweni ya wanafunzi 625, vyumba vya madarasa 1,499, matundu ya vyoo 4,836, Umaliziaji wa Maabara za sayansi 132, ujenzi nyumba za walimu 459, ujenzi wa mabwalo 3, samani zinazohusisha viti na meza 60, vitanda 123 na ukarabati wa shule chakavu 5.

UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA KATA JENZI wa shule Mpya za

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Carolyne Nombo amesema kuwa Ujenzi wa shule mpya za sekondari za Kata umefanyika kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha wa 2021/22 hadi 2024/25. Miundombinu iliyojengwa katika shule za sekondari za Kata ni pamoja na madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 3, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA na Matundu ya vyoo.

Nombo amesema Jumla ya shilingi Bilioni 394,790,160,363.08 zimetumika katika ujenzi wa shule mpya 694 za sekondari za Kata ambapo kati ya hizo shilingi Bilioni 375,096,425,878.00 ni kutoka kwenye mradi wa SEQUIP na  Shilingi Bilioni 19,693,734,485.08  zinatokana na mapato ya ndani ya Mamlaka  za Serikali za Mitaa kwa miradi ya awamu ya kwanza na ya pili. Shule hizi zimejengwa katika Halmashauri zote Tanzania Bara.

UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA AMALI

Kufuatia maboresho ya Mitaala ya Elimu Toleo la 2023, imeelekezwa kuanzishwa kwa shule za sekondari za amali zinazolenga kutoa masomo ya ujuzi kwa wanafunzi. Kutokana na maboresho hayo, shule mpya za Sekondari za Amali kwa ajili ya kutoa masomo ya ujuzi zinajengwa katika mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia mradi wa SEQUIP.

Kwa mujibu wa mratibu wa programu ya Elimu ya Sekondari kwa njia mbadala unaofahamika kama SEQUIP wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na serikali za mitaa-TAMISEMI Bw Richard Makota amebainisha kuwa Jumla ya shilingi Bilioni 88,849,305,125.00 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya 103 za sekondari za Amali. Ujenzi wa shule hizi unafanyika kupitia utaratibu wa aina mbili ambazo ni  ujenzi wa shule 29 za amali za kihandisi zinazojengewa miundombinu yote ikiwemo madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 2, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA, karakana, mabweni 4 na Matundu ya vyoo kwa gharama ya shilingi 46,400,000,000.00 ambayo ni sawa na shilingi Bilioni 1.6 kwa kila shule.

Makota amesema Ujenzi wa Shule 74 za sekondari za amali zisizo za kihandisi zinajengwa kwa gharama ya shilingi  Bilioni 42,449,305,125.00 Shule hizi zinajengewa miundombinu ya awamu ya kwanza inayohusisha madarasa 8, jengo la utawala 1, maabara 2, nyumba ya mwalimu, Maktaba, Chumba cha TEHAMA na Matundu ya vyoo.

UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA BWENI ZA WAVULANA

Mratibu wa programu ya Elimu ya Sekondari kwa njia mbadala SEQUIP Dkt Nicholaus Gati amesema Serikali iliamua kujenga shule mpya za Bweni za Wavulana katika Kanda saba nchini ambazo ni kanda ya Mashariki (Dar es Salaam, Pwani na Morogoro), Magharibi( Tabora, Kigoma, Katavi na Shinyanga), Kanda ya ziwa (Kagera, Mwanza, Simiyu, Geita na Mara), Kanda ya Kusini (Lindi, Mtwara na Ruvuma), Nyanda za juu Kusini (Iringa,Njombe, Mbeya, Songwe na Rukwa), Kanda ya kati (Dodoma na Singida) na kanda ya Kaskazini (Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga).

Dkt Gati ameeleza kuwa Jumla ya shilingi Bilioni 28,700,000,000.00 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa shule hizo mpya za wavulana za bweni ambapo kila shule imejengwa kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 4,100,000,000.

UJENZI WA SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZA BWENI ZA WASICHANA ZA MIKOA

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia Mhe Wanu Hafidh Ameir amezungumzia kuhusu Ujenzi wa shule za bweni ambapo amesema Ujenzi wa shule za bweni za Wasichana za Mikoa umefanyika katika mikoa yote Tanzania Bara. Kila shule imejengwa kwa kiasi cha fedha cha shilingi Bilioni 4,100,000,000.00 ambapo shule moja imejengewa miundombinu ikiwemo vyumba vya madarasa 22, jengo moja la utawala, maabara 4, matundu 16 ya vyoo, chumba kimoja cha jenereta, bwalo moja, mabweni 9 ambapo mabweni 5 yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 120 kila moja na mabweni 4 yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 80.

UJENZI WA MIUNDOMBINU MINGINE YA SHULE ZA SEKONDARI

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI) Adolf Ndunguru amesema pamoja na kujenga shule mpya za sekondari katika Mamlaka za Serikari za Mitaa, Mradi wa SEQUIP umefanikisha ujenzi wa miundombinu mingine ya shule. Miundombinu iliyojengwa ni pamoja na mabweni ya wanafunzi 625, vyumba vya madarasa 1,499, matundu ya vyoo 4,836, Umaliziaji  maboma ya vyumba vya Maabara za sayansi 132, ujenzi nyumba za walimu 459, ujenzi wa mabwalo 3, samani zinazohusisha viti na meza 60, vitanda 123 na ukarabati wa shule chakavu 5. Jumla ya shilingi Bilioni 167,987,845,884.00  zimetumika.

SHULE SALAMA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI) Mhe Prof Riziki Shemdoe anasema Serikali ya Tanzania kupitia Mradi wa kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP) inatekeleza Mpango wa Shule Salama katika shule 3,303. Lengo ni kujenga uwezo wa walimu wa malezi, ushauri nasaha na wanafunzi kuhusu dhana ya Shule Salama na kuwezesha uundaji wa mazingira rafiki na salama kwa ajili ya ufundishaji na ujifunzaji, Kuimarisha mazingira ya ujifunzaji shuleni na kutoa fursa ya elimu bora, salama na jumuishi kwa kila mtoto bila ubaguzi na kusaidia wanafunzi kuwa katika mazingira salama ya kujifunza na kupambana na changamoto zinazoweza kusababisha kuacha masomo, Ujenzi wa shule za bweni za wasichana 26, ambao unachangia kupunguza changamoto za umbali na usalama kwa wanafunzi wa kike.

Wanafunzi 10,239 wa kike waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito wameweza kuendelea na shule kupitia elimu kwa njia mbadala (Altenative Education Pathway) na 4,706 waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali wameweza kurejea shuleni kupitia mifumo rasmi.

Prof Shemsoe amebainisha kuwa kufuatia ujenzi wa miondombinu hii ambayo ni rafiki kwa wanafunzi imepelekea Kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wa kike wanaojiunga na Kidato cha Tano kutoka 24,637 mwaka 2020 hadi kufikia wananfunzi 67,304 mwaka 2024.

MAFUNZO YA TEHAMA, SAYANSI NA HISABATI

Mratibu wa programu ya Elimu ya Sekondari kwa njia mbadala SEQUIP Dkt Nicholaus Gati anasema katika Kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji kwa shule za sekondari za Serikali, serikali kupitia mradi wa SEQUIP imetoa mafunzo endelevu kazini kwa walimu 40,101 wanaofundisha masomo ya sayansi na hisabati. Mafunzo haya yamekuwa na tija kubwa sana katika maeneo makuu yafuatayo:

  Kuboresha kwa kiasi kikubwa ubora wa ufundishaji na ujifunzaji

  Kuongeza ufaulu na kuboresha matokeo ya wanafunzi

  Kuimarisha uelewa wa mtaala na mbinu za tathmini

  Kujenga uwezo wa kitaaluma na kitaalamu wa walimu

Vilevile, Jumla ya walimu 4,987 walishiriki katika mafunzo ya matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji, ikiwa ni sehemu ya lengo la jumla la kuwafikia walimu 5000 ndani ya muda wa utekelezaji wa mradi.

Katika kufanikisha utekelezaji wa mitaala, serikali kupitia mradi wa SEQUIP imechapa na kusambaza nakala 11,409,461 ya vitabu vya sekondari kwa masomo ya Sayansi, Hisabati na Amali.

Dkt Gati anaeleza kuwa hatua kubwa zimepigwa katika kuboresha miundombinu ya kidijitali kwenye shule za sekondari Tanzania Bara. Jumla ya kompyuta 1,848 aina ya all-in-one, kompyuta mpakato moja (laptop) 231, projekta 231, skrini 231, na UPS 462 zimenunuliwa na kusambazwa katika shule 231, Pia serikali imenunulia na kusambaza Bao janja (Smart Boards) katika shule 422.

WANAFUNZI WALIORUDI SHULE

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknlojia Mhe Prof Adolf Mkenda amebainisha kuwa jumla ya Wanafunzi 13,272 wa kike waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito wameweza kuendelea na shule kupitia elimu kwa njia mbadala (Altenative Education Pathway) na 4,706 waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali wameweza kurejea shuleni kupitia mifumo rasmi. Hadi kufikia mwaka 2024 Wanafunzi 721 walifanikiwa kufaulu kidato cha nne na kuchaguliwa kuendelea na masomo ambapo kidato cha tano walichaguliwa wanafunzi 467 na Vyuo vya Kati walichaguliwa wanafunzi 254.

Prof Mkenda anasema Serikali inajivunia mafanikio mbalimbali katika utekelezaji wa mradi wa SEQUIP ambapo imefanikiwa Kuongeza fursa ya upatikanaji wa Elimu kwa kujenga shule karibu na makazi ya wanachi na katika maeneo ambayo hayakuwa na shule za sekondari, kuogeza nafasi za udahili kwa wanafunzi wa Kidato cha Kwanza kwa wahitimu wa elimu ya msingi na wanafunzi wa kidato cha Tano  wanaofanya vizuri katika mitihani ya kidato cha nne, Kuondoa Msongamano wa wanafunzi katika shule za sekondari kutokana na kuongezeka kwa shule mpya, Kupunguza umbali wa wanafunzi wanaotembea kutoka katika makazi yao kufuata shule, Kuwaandaa wataalamu wa baadae katika tasnia ya sayansi na Teknolojia na ujuzi mbalimbali ambao watasoma na kupita katika shule mpya za sekondari, Kuimarisha Ulinzi na usalama wa wanafunzi kwa kuwawekea mazingira mazuri ya kujifunza na kuwaepusha na hatari zinazoweza kuwasababishia kukatisha masomo; na Kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

Katika tafakuri na uandaaji wa makala hii kwa kina, nimetembelea mikoa yote nchini kujionea hatua zilizofikia za utekelezaji wa miradi kama ambavyo nimeainisha kwenye makala hii, nimezungumza na wananchi katika maeneo yote yanayozunguka mradi na kila mmoja kwa nafasi yake amezungumzia kuhusu manufaa ya mradi wa SEQUIP kama miongoni mwa miradi iliyogusa maisha yao na hususani wananchi wa kawaida kwa sababu umeelekezwa moja kwa moja katika kuboresha huduma za elimu.

Katika maeneo mengi ya vijijini ambako kulikuwa na upungufu wa shule za sekondari, wananchi wameeleza kuwa ujenzi wa shule mpya umepunguza umbali, Nami nakubaliana nao kabisa ni kweli umbali ambao wanafunzi walikuwa wakitembea kila siku kufuata masomo ni wazi sasa umepungua, wapo waliokuwa wanatumia umbali wa zaidi ya kilomita 8 kufuata shule zilipo lakini kwa sasa kwa sehemu kubwa mwanafunzi hawezi kutembea umbali wa kilomita zaidi ya 3 kabla ya kuifikia shule ilipo. Wazazi wengi katika maelezo yao wameonyesha wanaamini kuwa hatua hiyo imeongeza mahudhurio ya wanafunzi na kupunguza vitendo vya utoro vinavyotokana na safari ndefu za kwenda na kurudi shuleni.

Katika mikoa ya Singida, Tabora, Dodoma na Katavi, wananchi wameeleza kuwa ujenzi wa madarasa mapya, mabweni na nyumba za walimu umeimarisha mazingira ya kujifunzia na kufundishia. Baadhi ya wananchi ambao kwa sehemu ni wazazi wa wanafunzi wamewlwza kuwa hapo awali wanafunzi walikuwa wakisoma katika madarasa machache yenye msongamano mkubwa, lakini kupitia SEQUIP hali hiyo imeanza kupungua. Pia wamesema uwepo wa nyumba za walimu umechangia walimu wengi kuishi karibu na shule na hivyo kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu.

Katika mikoa ya Kanda ya ziwa ukimowemo mkoa wa Kagera, Geita, Mwanza na Mara, wananchi wamepongeza jitihada za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuanzisha utekelezaji wa mradi huo kwani umekuwa sehemu ya kuimarisha sekta ya elimu hususani masomo ya Sayansi kwa kuboresha maabara za sayansi na upatikanaji wa vifaa vya kufundishia.

Wazazi na wananchi hao wanaamini kuwa uwekezaji huo utasaidia kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika masomo ya Sayansi na Hisabati ambayo kwa muda mrefu yalikuwa yakikabiliwa na changamoto za vifaa na miundombinu. Wazazi na viongozi wa jamii wameeleza kuwa maendeleo hayo yanaweka msingi mzuri wa kuandaa wataalamu wa baadaye katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Kwingineko katika mkoa wa Pwani, Lindi, Mtwara, na Ruvuma wananchi wameeleza kuwa mradi huo utakuwa kichocheo kikubwa kwani umeleta manufaa ya kiuchumi kwa jamii zinazozunguka shule zilizojengwa au kuboreshwa. Wakati wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi, vijana wengi walipata ajira za muda katika shughuli za ujenzi, usafirishaji wa vifaa na huduma nyingine zinazohusiana na miradi hiyo. Hali hiyo imeongeza mzunguko wa fedha katika maeneo husika na kutoa fursa za kipato kwa wananchi wa kawaida. Wapo vijana waliotoa ushuhuda kuhusu mafanikio waliyoyapata ikiwemo kufunga ndoa, ujenzi wa nyumba za kuishi na za biashara, ufunguzi wa miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa Lodge, miradi ya ufugaji nyuki na ufugaji wa Ng’ombe wa maziwa sambamba na miradi ya maduka pamoja na ununuzi wa pikipiki kwa ajili ya kazi za Bodaboda.

Kwa upande wa mikoa ya Kanda ya kaskazini ambayo ni Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga, wananchi wameeleza kwa namna chanya juhudi za mradi wa SEQUIP katika kuongeza fursa za elimu kwa wasichana. Wengi wanaamini kuwa uwekezaji katika mabweni, mazingira salama ya kujifunzia na programu za kuwasaidia wanafunzi waliokatisha masomo kurejea shuleni umeongeza usawa katika upatikanaji wa elimu. Baadhi ya viongozi wa dini na jamii wamekuwa wakihimiza familia kutumia fursa hizo kuhakikisha watoto wa kike wanamaliza elimu yao bila vikwazo.

Hata hivyo, pamoja na mafanikio hayo, wananchi katika baadhi ya maeneo wameeleza matarajio yao ya kuona mradi huo ukiendelea kuimarishwa kwa kuongeza idadi ya walimu, vifaa vya kufundishia na huduma za teknolojia katika shule mpya zilizojengwa. Wanaamini kuwa miundombinu bora pekee haitoshi bila kuwa na rasilimali watu na vifaa vinavyokidhi mahitaji ya wanafunzi. Kwa ujumla, maoni ya wananchi kutoka mikoa mbalimbali yanaonesha kuwa SEQUIP imeleta mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu na imekuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo mengi nchini.

Ama kwa hakika, haya ni mafanikio makubwa ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan inajivunia kwa kutumia njia mbalimbali ikishitrikiana na Wadau wa Maendeleo katika kuimarisha Sekta ya Elimu nchini na kuwaletea wananchi wake maendeleo.

Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan inajivunia Mradi wa SEQUIP kama alama ya maendeleo, urithi wa kizazi kijacho, na nguzo ya uchumi wa viwanda kupitia elimu watakayoipata wanafunzi. Mradi huu ni mfano wa kujitegemea, uzalendo, na dira ya maendeleo ya Taifa kwa kutumia rasilimali za ndani.

Tanzania sasa imeandika historia. Kwa fedha zetu wenyewe, kwa wataalamu wetu, na kwa moyo wetu, Kukamilika kwa Mradi wa SEQUIP si tu itaboresha elimu ya Tanzania na vizazi vijavyo bali ni ushindi wa watanzania wote.

MWISHO

Share:
Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com