METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, April 13, 2017

DIASPORA WATAKIWA KUSHIRIKI KUWATAFUTIA KAZI WATANZANIA KATIKA MASHIRIKA YA NDEGE

Picha ya Mjengwa Blog

Na Nuru Juma na Jacquiline Mrisho – MAELEZO

Shirika la usafiri wa Anga Tanzania (ATCL) limetoa fursa kwa Watanzania wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) kuzungumza na mashirika ya ndege ya nchi wanazoishi ili kuunganisha watanzania kufanya kazi na nchi hizo.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Mhandisi Ladislaus Matindi alipokuwa akizungumza na wajasiriamali na wananchi katika mdahalo wa Diaspora uliofanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa.

Mhandisi Matindi alisema kuwa Diaspora wanatakiwa kuanza kutumia fursa zinazopatikana katika usafiri wa anga ili kusaidia watanzania kufaidika na shirika hilo kwani ni sekta inayotoa ajira kwa Watanzania wengi.

“Shirika la ndege linahitaji wauza tiketi, wauza chakula, wasafirishaji na wapokeaji wa mizigo pamoja na wauzaji wa spea za ndege, hivyo Watanzania walioko nchini pamoja na  DIASPORA wanatakiwa kushirikiana ili kupata watu wenye taaluma mbalimbali watakaofanya kazi na shirika hilo,” alisema Matindi.

Mhandisi Matindi ameongeza kuwa ATCL ipo tayari kushirikiana na Diaspora katika kujenga uchumi wa nchi kwa kuangalia fursa ambazo wengi hawafahamu kama zipo nchini Tanzania.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo aliwataka Watanzania wanaomaliza masomo ya masuala ya ndege nje ya nchi kurudi nyumbani ili waweze kuajiriwa na shirika hilo kwa ajili ya kuongeza wataalamu nchini na kukuza uchumi wa Nchi.

Vile vile amewataka watanzania kuelewa kuwa ununuzi wa ndege ni kwa ajili ya kukuza uchumi wa nchi na si ufujaji wa fedha kama Watanzania wengi wanavyodhani  pia ametoa rai kwa Watanzania kutumia usafiri wa shirika hilo kwani unatoa huduma sawa na mashirika mengine tena kwa gharama zinazokidhi mahitaji ya Mtanzania.

Mnamo mwaka 2016, Serikali ilianza kuwekeza katika kufufua Shirika la Usafiri wa Anga Tanzania kwa kuanza kununua ndege mbili mpya. Aidha  Serikali ina mpango wa kuongeza ndege mbili za saizi ya kati zenye uwezo wa kubeba abiria 132 na moja kubwa yenye uwezo wa kubeba abiria zaidi ya 264 ifikapo mwaka 2018.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com