METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, December 22, 2021

ACT WAZALENDO KUKUSANYA MAONI TUME HURU YA UCHAGUZI

 





Na ACT- WAZALENDO, RUVUMA

CHAMA cha ACT wazalendo  kupitia kwa katibu wake  Ado Shaibu  kimedhamilia kufanya mchakato wa kukusanya maoni ya wananchama wake kuhusu tume huru ya uchaguzi  ikiwa ni maelekezo ya  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Chama hicho .

Akizungumza na viongozi wa ACT Wazalendo katika Jimbo la Nyasa Mkoani Ruvuma katika mwendelezo wa ziara yake kwenye mikoa ya Ruvuma, Selous, Mtwara, Lindi, Pwani na Tanga yenye lengo la ujenzi wa Chama, kuhamasisha na kufanya harambee ya michango ya wanachama ya kugharamia Mkutano Mkuu wa Chama wa tarehe 29 Januari 2022 na kufafanua mageuzi ya uendeshaji Chama kisayansi   Ado shaibu amesema kuwa ofisi ya mwanansheria mkuu wa chama imeagiza kukusanya maoni kwa wanachama wake.

"Kwenye kikao cha Wadau wa Siasa Juu ya Hali ya Demokrasia nchini kilichofanyika Dodoma, suala la Tume Huru ya Uchaguzi liliafikiwa na pande zote. Kwetu sisi ACT Wazalendo, hatua inayofuata ni mjadala wa kitaifa kuhusu aina ya Tume Huru tunayoihitaji" alisema Katibu Mkuu, Ado Shaibu.

Katibu Mkuu  huyo wa ACT wazalendo amesema vikao vya  chama (ACT Wazalendo Kamati Kuu ya mwezi Juni na Halmashauri Kuu ya mwezi Oktoba 2021) vimeagiza Chama kulipa kipaumbele suala la Tume Huru ya Uchaguzi.

Ameongeza kuwa mbali na maoni ya wanachama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa ACT Wazalendo imeagizwa kufanya rejea ya uzoefu wa nchi nyingine zenye mifano ya Tume za Uchaguzi zinazopigiwa mfano pamoja na Ripoti na Taarifa mbalimbali ikiwemo Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba.

Ndugu Ado amewaeleza viongozi wa Chama jimboni Nyasa kuwa Chama kitaendelea kulipa kipaumbele suala la Tume Huru ya Uchaguzi ili chaguzi za mwaka 2024 (Serikali za Mitaa) na 2025 (Uchaguzi Mkuu) ziwe huru, za haki na zenye kuaminika.

Katibu Mkuu anaendelea na ziara yake mkoani Ruvuma na leo atakuwa jimbo la Songea Mjini.

 

 

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com