METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, May 1, 2020

TATHMINI YA UNUNUZI WA PAMBA KUFANYIKA KABLA MSIMU


Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akikagua mbegu ya pamba inayofanyiwa utafiti kuangalia uwezo wa kuhimili viuatilifu vya ugonjwa wa Mnyauko Fuzari katika shamba la majaribio la kituo cha utafiti TARI Ukiriguru kituo cha Bwanga wilaya ya Chato  leo

Katibu Mkuu wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akiwa ameshika mbegu ya pamba katika shamba la majaribio ya mbegu kijiji cha Bwanga wilaya ya Chato.Kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa TARI Dkt.Geofrey Mkamilo.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya (aliyevaa koti la blu) akiongea na watumishi wa chama Kikuu cha Ushirika Chato alipotembelea kukagua kiwanda cha kuchambua pamba.Kushoto kwake ni Katibu Tawala Mkoa wa Geita Bw.Claudio Bandisa
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akiwa ameshika cherehani inayotumika kuchambua na kutenganisha pamba mbegu na pamba sufi alipotembela kiwanda cha kuchambua pamba cha Chato .
Katibu Mkuu wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akitazama shamba la pamba la majaribio ya viuatilifu vya pamba chini ya TARI  toka kwa watu binafsi kuona endapo vinauwezo wa kudhibiti ugonjwa wa Mnyauko Fuzari lililopo kijiji cha Bwanga Chato.

Serikali imesema inafanya tathmini ya hali ya ununuzi wa zao la pamba msimu wa mwaka 2019 ili kuondoa changamoto zilizojitokeza kabla msimu mpya wa ununuzi kuanza mwaka huu.

Akizungumza na viongozi wa wilaya ya Chato mara baada ya kutembelea viwanda vya kuchambua pamba, Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya amesema msimu mpya wa ununuzi utatangazwa mara baada ya tathmini ya msimu uliopita kufanyika.

“ Wizara imegundua kuwa hali ya mazao shambani kwa pamba bado ,kwani hata vitumba bado havijapasuka kutokana na uwepo mvua nyingi ,hivyo baada ya ziara hii kwenye mikoa ya kanda ya ziwa serikali itakaa na watalaam ili kuamua lini wakulima wataanza kuuza pamba yao kupitia Vyama Vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) “ alisema Kusaya

Aliongeza kusema kabla msimu haujafunguliwa serikali itahakikisha madeni ya wakulima,wanunuzi na ushuru wa AMCOS, halmashauri pamoja na mfuko wa pembejeo yanalipwa.

“Kila mwananchi atalipwa madai yake na jitihada za serikali ni kuona madeni haya yanalipwa kabla ya msimu mpya wa ununuzi wa pamba kuanza” alisitiza Katibu mkuu
Katika hatua nyingine Chama Kikuu cha Ushirika Chato( CCU) kimetakiwa kuhamasisha wakulima wengi zaidi kuzalisha zao la pamba ili ipate malighafi za kutosha kutumika kwenye kiwanda chake cha kuchambua pamba.

Kusaya alitoa wito huo kufuatia taarifa ya Meneja Mkuu wa Chama hicho Joseph Masingiri kusema kiwanda kimeshindwa kuendelea na uchakataji marobota kutokana na uhaba wa pamba ambapo msimu wa 2019 ni  kilo milioni 13.6 ,000 tu zilinunuliwa wakati uwezo wake ni kilo milioni 30.

Ili kukabiliana na changamoto za zao hilo,Katibu Mkuu Kusaya amewataka wataalam wa halmashauri na wa chama kikuu  kuhamasisha wakulima kuzalisha mazao ya mkonge na korosho ili kuwa na uhakika wa kipato pale zao la  pamba linapoyumba.

“ Tulime pamba na mazao mengine ya biashara kama mkonge na korosho yanayostawi vizuri kwenye mkoa huu wa Geita na kanda ya ziwa yote .Wizara ya kilimo ipo tayari kuleta mbegu bora za mkonge na korosho toka taasisi za utafiti ili zigawiwe kwa wakulima “ Kusaya.

Kusaya alitaja faida za zao la mkonge kuwa katika kipindi cha miaka mitatu  baada ya kupanda mkulima ataanza kuvuna na kuendelea hadi miaka kumi na tano huku akiendelea na kilimo cha mazao mengine .

Katika kuhakikisha mkoa wa Geita unaongeza uzalishaji wa mazao nchini,Katibu Mkuu huyo ameelekeza mkoa uwasilishe wizarani maandiko ya miradi ya kipaumbele ya umwagiliaji ili serikali itafute wadau wa kuitekeleza.

Nae Katibu Tawala Mkoa wa Geita Dennis Bandisa aliyeshiriki ziara hiyo aliishukuru wizara ya kilimo kwa kuonesha nia ya kusaidia kukuza kilimo cha umwagiliaji na kuwa kuahidi kuwa maandiko atayawasilisha wizarani ndani ya kipindi kifupi.

Taarifa ya  Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Eliurd Mwaiteleke kuhusu sekta ya kilimo ilisema wilaya hiyo ina eneo la hekta 10,810 zinazofaa kwa umwagiliaj lakini ni hekta 3,416 tu sawa na asilimia 31.6 zinamwagiliwa.

Katika msimu wa mwaka 2019 jumla ya kilo milioni 10.8 za pamba mbegu zilinunuliwa wilayani Chato kupitia AMCOS zenye thamni ya shilingi Bilioni 13.06 ililipwa kwa wakulima.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com