METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, March 4, 2020

TRA SONGWE YAGAWA BIDHAA ZILIZOINGIZWA KWA NJIA ZA MAGENDO

Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela (aliyevaa miwani) akikagua orodha ya bidhaa ambazo zimetolewa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kutokana na kuwa zimekamatwa kwa njia za njia za magendo na wamiliki hawakujitokeza.
Simenti iliyokamatwa kwa kuingizwa nchini kwa njia za Magendo katika Mpaka wa Tunduma ikitolewa kwa ajili ya kupelekwa katika shule za sekondari za Mkoa wa Songwe.


Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) Mkoa wa Songwe imegawa baadhi ya bidhaa zilizo kamatwa kwa kuingizwa Nchini kupitia mpaka wa Tunduma kwa njia za Magendo ili kukwepa ushuru.
Akipokea bidhaa hizo kutoka Kwa Kaimu Meneja TRA Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela amesema bidhaa hizo zinapelekwa katika shule za Sekondari za Mkoa wa Songwe ili ziweze kuwasaidia wanafunzi.
“Nimepokea simenti mifuko 192, mafuta ya kupikia ndoo 37 na sukari katoni 70 ambavyo vyote navielekeza katika shule za Sekondari  ili vikasaidie huko.” , amesema Brig. Jen. Mwangela.
Amesema mifuko 100 ya simenti ameelekza ipelekwe Wilaya ya Momba ambapo kuna ujenzi wa shule ya sekondari ya Wasichana kwa kidato cha tano na sita na sukari imetolewa kipaumbele Wilaya ya Mbozi ambayo watakuwa wenyeji wa wanafunzi wa Michezo ya Umiseta.
Brig. Jen. Mwangela amewataka Wakuu wa Wilaya kuhakikisha wanafuatilia bidhaa hizo ili zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa na si vinginevyo.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Momba Juma Said Irando ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara waliozoea kutumia njia zisizo halali kuingiza bidhaa nchini Kupitia Mpaka wa Tunduma waache maramoja kwani kamati ya Usalama ya Wilaya yake imeimarisha doria ili kumaliza tatizo la wakwepa kodi.
Irando amewata wafanyabiashara kutumia njia halali pia wazingatie sheria na taratibu za forodha ili waweze kufanya bishara halali na kuepuka hasara kwakuwa watakamatwa.
Amesema kuwa wafanyabiashara watambue kuwa wakikamatwa na bidhaa ambazo zimeingizwa Nchini isivyo halali sio tu watataifishwa mali hizo bali sheria zinawataka walipe kodi na faini ili wachangie pato la Nchi.
Irando ameongeza kuwa Wilaya yake imepokea mifuko 100 ya simenti ambayo itasaidia katika ujenzi wa Sekondari ya Wasichana ambayo itakuwa sekondari ya A level kwa wasichaa pekee Mkoa wa Songwe.
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TRA Mkoa wa Songwe Farensi Mniko amesema walifanikiwa kukamata bidhaa hizo kutokana na kuimarisha kaguzi mbalimbali katika Mpaka wa Tunduma pia kwa kupata taarifa kutoka kwa wananchi mbalimbali.
Mniko ameongeza kuwa bidhaa zilizo kamatwa zikikaa muda mrefu bila mhusika kuzichukua Kamishna wa TRA anayo mamlaka ya kuzigawa kwa taasisi za serikali kama alivyo fanya kwa bidhaa za simenti, sukari na mafuta alizozitoa.
Ameongeza kuwa bidhaa hizo hukaguliwa ubora wake kabla hazijagawiwa kwa taasisi za serikali hivyo zinakuwa salama, huku akiwasisitiza wafanyabiashara waache kupita njia zisizo halali kwakuwa TRA imejipanga kukomesha magendo.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com