METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, November 10, 2019

WAZIRI NDALICHAKO AFUNGUA OFISI MPYA ZA UTHIBITI UBORA WA SHULE MISUNGWI NA SHINYANGA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikata utepe kuashiria ufunguzi wa ofisi mpya ya Uthibiti Ubora wa Shule ya Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako na Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Juma Sweda (mwenye suti ya bluu) wakikagua ofisi mpya ya Uthibiti Ubora wa Shule ya wilaya hiyo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akifurahi kwa kucheza kwaya na baadhi ya viongozi wa wilaya ya Misunhwi mara baada ya kufungua ofisi mpya za Uthibiti Ubora wa Shule ya Wilaya Misungwi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi wilayani Misungwi.
Muonekana wa Ofisi mpya za uthibiti ubora wa shule ya Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi
……………….

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amefungua majengo ya ofisi mpya za Uthibiti Ubora wa Shule za Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi na Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Akizungumza baada ya ufunguzi wa ofisi hizo Waziri Ndalichako amewataka wathibiti Ubora wa Wilaya kufanya kazi kwa bidii na weledi na waone kuwa uwepo wa ofisi hizo uwe chachu ya kuendelea kutoa taarifa za ukaguzi wa shule zenye ubora na kwa wakati. Ndalichako amewataka kuhakikisha kuwa changamoto zinazoainishwa katika kaguzi zao zinafanyiwa kazi ili kuinua ubora wa elimu hususan katika taaluma na sekta ya elimu kwa ujumla katika wilaya hizo.

“Tumieni ofisi hizi kuwa chachu ya kuwawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na kutoa taarifa za changamoto zinazozikabili shule pamoja na sekta nzima ya elimu ili ziweze kufanyiwa kazi kwa haraka,” amesema Profesa Ndalichako.

Prof. Ndalichako amesema serikali itahakikisha changamoto zote zinazowakabili wathibiti ubora wa shule nchini zinafanyiwa kazi kwa dhati ili kuzipunguza ama kuzimaliza kabisa ikiwemo ukosefu wa ofisi na vitendea kazi.

Akizungumzia uboreshaji na ujenzi wa miundombinu ya sekta ya elimu unaoendelea nchini, Profesa Ndalichako amesema suala hilo ni endelevu na litakuwa likifanyiwa kazi muda wote ili kuwezesha utoaji wa elimu bora kwa watoto wa Kitanzania.

Aidha, Waziri Ndalichako amewataka wathibiti ubora wa shule kwa kushirikiana na Maafisa Elimu kufanya tathimini za kina kila mara ili kubaini sababu halisi za mdondoko wa wanafunzi wote wa kike na kiume.

“Tumeona hapa Misungwi takwimu zinaonyesha mdondoko mkubwa zaidi upo kwa upande wa watoto, hivyo fanyeni tathimini ili tujue sababu na kuacha kuegemea upande mmoja wa mtoti wa kike na kwamba sababu ni mimba” amesema Profesa Ndalichako

Mkuu wa wilaya ya Misungwi, Juma Sweda ameishukuru serikali kwa kuhakikisha wathibiti ubora wa shule wanapata ofisi za kisasa na vitendea kazi na kuhaidi kuwa wilaya ya Misungwi itaendelea kusimamia ubora wa elimu na kuongeza ufaulu katika ngazi zote.

“Sisi tutaendelea kusimamia utoaji wa elimu bora kwa watoto wote wa hapa Misungwi pamoja na kupunguza mdondoko wa wanafunzi kwa kuanzisha mpango wa kutoa chakula shuleni” amesitiza Mkuu wa Wilaya.

Naye Mthibiti Mkuu wa Wilaya hiyo, Faustine Sahala ameishukuru serikali kwa kuona changamoto zilizokuwa zikiwakabili za ukosefu ofisi ambapo walipatiwa zaidi ya shilingi milioni 152 kwa ajili ya ujenzi wa ofisi hizo.
  Sahala amesema ujenzi wa ofisi hiyo umekamilika kwa asilimia 100 pamoja na ununuzi wa vitendea kazi ikiwemo mashine ya kurudufu (photocopy), ufungaji mtandao wa internet, uwekaji samani, camera za ulinzi (CCTV) na ujenzi wa vyoo vya nje.

Katika Mpango huu Serikali inajenga ofisi 100 za Wadhibiti Ubora wa shule katika Halmashauri 100 kwa shilingi bilioni 15.2
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com