****************************
Na.Mwandishi Wetu-MAELEZO
11/10/2019
Shirika la Taifa la Hifadhi za Jamii (NSSF) limewataka wateja wake kuwa wazo kwa hisia zao, ili maswali, maoni na hoja zao mbalimbali zijibiwe na Shirika kwa lengo la kuimarisha huduma zitolewazo na Shirika hilo, ambapo ‘Wiki ya Huduma kwa Wateja Duniani’ imekuja na Kauli Mbiu “ Sema na NSSF”, inayowapa nafasi wateja kusema kero zao., Akizungumza Jijini Dar es Salaam, wiki hii, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. William Erio alisema kuwa wanatumia kauli mbiu hiyo ikilenga kuwasikiliza wanachama na wateja wao kubaini hisia na changamoto zao juu ya mafao pamoja na huduma zingine zinazotolewa na NSSF ili kuimarisha huduma zao.
“NSSF tunatoa huduma kwa wateja ndani ya wiki hii ya huduma kwa wateja ulimwenguni kwa hiyo tuko hapa leo kuhakikisha tunatoa huduma iliyobora kwenye siku hii; na siku zijazo kama kawaida yetu, tayari tunamkataba wa huduma kwa wateja ambao tunatakiwa kufuata ili kuendeleza huduma bora kwa watu waweze kufurahia huduma zetu”, Bw.Erio.
Erio alitoa wito kwa wanachama na wateja wote kuwa NSSF iko wazi kupokea maoni, matatizo, malalamiko na mema ambayo wateja na wanachama wanapaswa wanahitaji kufanyiwa ili kuimarisha huduma zao, pia alieleza zoezi la utoaji huduma iliyobora siyo la siku moja bali ni zoezi endelevu.
Kwa upande wake Meneja Huduma kwa Wateja wa NSSF, Bi.Christina Kamuzola, alisema kuwa NSSF iko tayari kila siku kutekeleza kauli mbiu yake ya wiki ya huduma kwa wateja kwani inachochea kuimarisha utoaji huduma kwa wateja wake.
“Wiki hii ambayo ni wiki ya Huduma kwa wateja duniani, tuna kauli mbiu isemayo “Sema na NSSF” ambayo sasa imekuja wakati muafaka na hii italeta utekelezaji wa majukumu ya kuwapatia wananchi, hasa waliowateja wa NSSF huduma zilizoboreshwa kutoka kwenye Shirika hili”, Bi. Christina Kamuzola.
Aliongeza kuwa NSSF inamkataba wa Huduma kwa wateja, ambao unalifanya Shirika kutekeleza majukumu yake ipasvyo kwa wateja, lakini pia wateja wake kujua wajibu wao kwa Shirika hilo la hifadhi za Jamii nchini; ikiwa ni pamoja na upokeaji wa malalamiko kwa wateja na kutatua kero zao.
Naye Mkurugenzi wa Tehama kutoka NSSF, Bw.Robert Mtendamema, alisema kuwa huduma za Shirika hilo zimeboreshwa kwa kuwa mifumu ya kimtandao imeimarishwa na kuhakikisha kila mteja anapata huduma iliyobora zaidi.
“Tumeboresha mifumo yetu ya Tehama ambayo inachangia kwenye ubora wa huduma kwa wateja wetu, kwa sasa hakuna tena mambo ya foleni wakati wa ufuatiliaji wa mafao, kwa sasa watu wanalipwa moja kwa moja kupitia akaunti zao na pia tumejiunga na mfumo wa malipo ya serikali GEPG kwa hiyo hii inaboresha huduma zetu kwa wanachama wetu”, alisema Mtendamema.