METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, January 19, 2019

TADB, NFRA ZAJA KIMKAKATI KATIKA KUIMARISHA MNYORORO WA THAMANI WA MAHINDI

Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Japhet Justine (kushoto) akihimiza jambo kuhusu ushirikiano wa pamoja kati ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula katika kuchagiza mnyororo wa thamani wa mahindi nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Japhet Justine (katikati kushoto) akizungumza na ugeni kutoka NFRA walioongozwa na Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu, Bi Vumilia  Zikankuba  (katikati kulia) kuhusu mkakati wa kuimarisha mnyororo wa thamani wa mahindi nchini.
Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Bi Vumilia  Zikankuba akizungumza wakati wa kikao hicho. 


Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) zimekuja na mkakati kabambe unaolenga kuimarisha mnyororo wa thamani wa mahindi ili kuleta tija na kuwawezesha wakulima wadogo wadogo wa zao hilo hapa nchini kwa kuwapatia soko la uhakika la mazao yao.

Mkakati huo wa pamoja unalenga kupunguza changamoto za ukosefu wa soko la uhakika la zao la mahindi ambazo zimekuwa zikiwakabili wakulima wa zao hilo hapa nchini.

Mkakati huo umewekwa wazi na Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Japhet Justine mara baada ya kikao cha pamoja kilicholenga kujadili namna bora ya kuwanyanyua wakulima wadogo wadogo wa zao la mahindi kupitia ununuzi zao hilo kupitia NFRA.

“Tumekubaliana na NFRA kuja na mpango wa mkakati utakaosaidia kuimarisha mnyororo wa thamani wa mahindi ili kuongeza tija kwenye masoko ili kuwaondolea wakulima wadogo wadogo changamoto za masoko ya mahindi yanayowakabili kwa sasa,” alisema Bw. Justine.

Akizungumzia nafasi ya TADB katika kuchagiza uwekezaji katika mnyororo mzima wa ongezeko la thamani wa zao la mahindi, Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Bibi Vumilia  Zikankuba, amesema utayari wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo katika kusaidia zao la mahindi utasaidia kwa kiwango kikubwa uhakika wa soko na hivyo kuwawezesha wakulima wadogo wadogo wa zao hilo hapa nchini.

“Fursa za mikopo ya TADB inatupa nafasi ya kujipanga kimakakati kwa ajili ya kupata mtaji wa uhakika wa uendeshaji wa shughuli zetu za kununulia mahindi yenye ubora hivyo kuwa na uhakika wa soko kwa mazao ya wakulima,” alisema.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com