METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, May 2, 2024

RAIS SAMIA ATOA BIL 5 KUREJESHA MIUNDOMBINU YA BARABARA NA MADARAJA


Mvua kubwa za El-Nino zilizonyesha zimeleta athari maeneo mbalimbali hapa Nchini ikiwemo katika Mkoa wa Lindi ambapo zimesababisha uharifu mkubwa wa miundombinu ya barabara na madaraja.

Mvua hizo katika baadhi ya maeneo zilikwamisha shughuli za maendeleo ya Wananchi, na hivyo kuifanya Serikali kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kufanya kila linalowezekana kurejesha mawasiliano ya barabara zilizokatika kwa haraka.

Kwa kuliona hilo,  Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa shilingi bilioni 5 ambazo ni fedha za dharura kwajili ya kurejesha  miundombinu ya barabara na madaraja ambayo imeharibika katika Mkoa wa Lindi.

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Lindi Mhandisi Emil Zengo ameyasema hayo tarehe 2 Mei 2024; alipotembelea kukagua hatua za ujenzi zinazoendelea katika daraja la Somanga linalounganisha Mikoa wa Dar es Salaam - Pwani, Lindi, Mtwara na Ruvuma ambalo lilikatika kutokana na mvua za El-Nino na kusababisha magari ya abiria na mizigo kukwama njiani.

"Tunamshukuru sana Waziri wetu wa Ujenzi Mhe Innocent Bashungwa alitupa maelekezo ya kuhakikisha maeneo yote yaliyoathirika na mvua za El-Nino tuhakikishe ndani ya muda mfupi yanapitika nasi kupitia Mtendaji Mkuu wa TANROADS Mhandisi Mohamed Besta tumefanya kazi usiku na mchana kwa sasa miundombinu imerejea" Amesisitiza Mhandisi Zengo

Amewataka Wananchi wanaoishi karibu na barabara kuacha kufanya shughuli za kibinadamu kwenye kingo za barabara pamoja na kutupa taka ngumu katika mitaro kwani kufanya hivyo kunasababisha maji kushindwa kupita pindi mvua zinaponyesha. 

Kwa upande wake Msimamizi Kitengo cha Matengenezo TANROADS Mkoa wa Lindi Mhandisi Robert Mosea  ametaja barabara ambazo zimeathiriwa na mvua hizo na zinaendelea na matengenezo ni Kilwa Masoko – Nangurukuru mpaka Liwale, Barabara ya Liwale – Nachingwea, Nachingwea mpaka Kilimarondo pamoja na Barabara ya Tingi – Kipatimo.

“kwa kuzingatia maelekezo ya viongozi wetu tumeweka kambi maeneo mbalimbali kwa ajili ya kurahisha ukarabati wa barabara hizo na kwa sasa Wakandarasi wapo maeneo yaliyoathirika ili kuimarisha zaidi miundombinu iliyoharibika’' ameeleza.

Naye Msimamizi wa Miradi ya Maendeleo TANROADS Mkoa wa  Lindi Mhandisi Roman Mbukwini  amesema Barabara kuu  ya Lindi – Pwani – Dar- es Salaam imeharibika zaidi maeneo ya Somanga – Mtama na Mbwemkuru ambapo maji yalipita juu na kuharibu kingo za madaraja.

Aidha Mkoa wa Lindi una jumla ya Kilomita 1289.97 ambazo zinafanyiwa matengenezo ya barabara.
Share:

BARABARA ZOTE ZINAZOSIMAMIWA NA TANROADS ZILIZOATHIRIWA NA MVUA ZA EL-NINO ZINAFUNGULIWA KWA WAKATI-WAZIRI BASHUNGWA

RAIS SAMIA ARIDHIA UJENZI WA BARABARA YA KM 41 KUTOKA KIBADA -MWASONGA -KIMBIJI-WAZIRI BASHUNGWA

Serikali inazifungua barabara zote zilizoathiriwa na mvua za El-Nino ambazo zimeendelea kunyesha kwa muda mrefu katika maeneo mbalimbali kote nchini na kuleta uharibifu wa miundombinu ya barabara.


Licha ya uharibifu unaotokea Wizara ya Ujenzi kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kupitia kitengo cha dharura imekuwa ikirudisha mawasiliano kwenye maeneo ambayo mawasiliano yamekatika kutokana na uharibifu.
 

Waziri wa Ujenzi Mhe Innocent Bashungwa ameyasema hayo tarehe 29 Aprili 2024 katika Manispaa ya Kigamboni wakati alipotembelea na kukagua barabara ya Kibada-Mwasonga-Kimbiji akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili Jijini Dar es salaam


Amesema zoezi la kufungua miundombinnu ya barabara limefanikiwa kutokana na serikali ya awamu sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuiwezesha kibajeti TANROADS kupitia kitengo cha dharura ili kurahisisha shughuli za kiuchumi na utoaji wa huduma.


Waziri Bashungwa amewahakikishia wananchi kote nchini kuwa hakuna barabara ambayo mawasiliano yatakatika kutokana na mvua kisha ikaachwa bila ya mawasiliano yake kurudishwa kwa haraka.


Kuhusu ujenzi wa barabara katika wilaya ya Kigamboni Waziri Bashungwa ameeleza kwamba, serikali ya awamu sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeridhia ujenzi wa barabara ya kutoka Kibada kwenda Mwasonga hadi Kimbiji yenye urefu wa kilometa 41.


"Awali ujenzi wa barabara ya Kibada kwenda Mwasonga hadi Kimbiji yenye urefu wa kilomita 41, ilitakiwa iishie hapo, lakini kutokana na maombi yaliyoletwa na mbunge wenu (mbunge wa Kigamboni) serikali imeridhia na hivyo tumeongeza kilometa 10 na kufanya ujenzi wa barabara hiyo itakuwa ni kilometa 51 kumalizia kipande chote kiluchobakia katika barabara hii" Amesisitiza Waziri Bashungwa


Amepongeza hatua za haraka zinazoendelea kuchukuliwa na TANROADS, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es saklaam pamoja na TARURA katika kukabiliana na athari za miundombinu ya barabara na madaraja zilizotokana ana mvua za El-Nino


Kwa upande mwingine, Waziri Bashungwa ameagiza kuundwa kwa timu maalumu na kisha kupelekwa katika eneo la Magogoni lililopo kata ya Tungi wilayani Kigamboni kwa ajili ya kufanya usanifu na kisha kuja na majawabu ya juu ya nini kifanyike ili kutatua changamoto ya maji kuzingira makazi ya wananchi wa eneo hilo.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amesema mkoa huo unahitajika kufumuliwa kwenye mifumo imara na thabiti ya kusafirisha maji ya mvua lengo likiwa ni kuondoa athari zinazotokana na mafuriko ikiwemo wananchi kupoteza maisha.


Mkuu huyo wa Mkoa ameendelea kwa kusema kuwa, watu wengi wamejenga juu ya mifumo hiyo ya kusafirisha maji ya mvua hivyo kama mkoa watafanya usanifu kupata suluhu ya changamoto ya mafuriko.


Akizungumza kwa niaba ya wanachi, mbunge wa jimbo la Kigamboni Dkt. Faustine Ndugulile amesema, kukamilika kwa ujenzi wa barabara ya kutoka Kigamboni kuelekea Mwasonga hadi Kimbiji itakuwa ni faida kubwa kwa wakazi wa Kigamboni kwani inatumiwa na watu wengi na inapita kuelekea kwenye viwanda zaidi ya 10.

Dkt. Ndugulile ameongeza kuwa, barabara hiyo inapitisha magari zaidi ya 1,000 madogo kwa makubwa yenye uzito tofauti hivyo ni barabara muhimu kiuchumi na kwa shughuli za uzalishaji.


Kando na hayo, Ndugulile ametoa ombi kwa mkandarasi anayejenga barabara hiyo pia kujielekeza kwenye ujenzi wa mifereji ya maji kwani imekuwa ni changamoto kubwa katika barabara za Kigamboni.

 
MWISHO
Share:

Monday, April 29, 2024

DKT.GWAJIMA: UKATILI WA KIJINSIA NI CHANZO CHA MIGOGORO KATIKA FAMILIA


Na Saida Issa,Dodoma.

SERIKALI imesema kuwa ukatili dhidi ya Watoto na ukatili wa kijinsia katika familia umechangia kuongezeka kwa migogoro ya kifamilia hususan kati ya wenza au wanandoa jambo lenye athari kubwa katika malezi na ustawi wa watoto wa familia na jamii kwa ujumla. 

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia Wanawake na Makundi Maalum,Dkt.Dorothy Gwajima wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya siku ya kimataifa ya Familia Mei 15 ,2024 katika Mikoa yote ya Tanzania Bara ambapo amesema hiyo ni kwa mujibu wa utafiti wa hali ya Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria nchini ya mwaka 2022. 

Dkt. Gwajima amesema kuwa utafiti huo unaeleza kuwa watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani wengi wamekimbia familia zao kutokana na migogoro ya wenza au wanandoa ambapo Taarifa ya utafiti inaonesha asilimia 27 ya wanawake wa umri wa miaka 15 hadi 49 walifanyiwa vitendo vya ukatili wa kimwili huku asilimia 12 ya wanawake wa umri huo walifanyiwa ukatili wa kingono.

Amesema asilimia 13 ya wanawake waliowahi kuwa na mume au mtu mwenye mahusiano katika kipindi cha miezi 12 kabla ya utafiti huo walifanyiwa vitendo vya ukatili wa kimwili, kingono na kihisia.

Amesema kuwa unyanyasaji wa kimwili, kingono, au kihisia miongoni mwa wanawake walioolewa umepungua kutoka asilimia 50 mwaka 2015/16 hadi asilimia 39 mwaka 2022/23.

Hata hivyo Dkt.Gwajima amesema kuwa Wizara imeendelea kuratibu huduma za usuluhishi wa migogoro ya ndoa na familia kupitia Baraza la Usuluhishi wa Ndoa la Kamishna wa Ustawi wa Jamii lililopo Makao Makuu ya Wizara, Mabaraza ya Kata na Mabaraza ya Jumuiya. 

Amebanisha kuwa,Kwa kipindi cha Julai, 2023 hadi Aprili, 2024 Jumla ya mashauri 14,600 yalishughulikiwa ambapo, yaliyohusu migogoro ya ndoa yalikuwa 5,306 (36%), yaliyohusu migogoro ya kifamilia na matunzo ya Watoto 5,944 (41%), yaliyohusu matunzo ya watoto waliozaliwa nje ya ndoa yalikuwa 3,350 (23%).
Share:

Sunday, April 28, 2024

HATUA ZA DHARURA ZAENDELEA KUCHUKULIWA NA TANROADS MOROGORO KUREJESHA MIUNDOMBINU


Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro imewataka Wananchi wa Mkoa huo kuwa watulivi wakati Serikali ikiendelea kuchukuwa hatua za dharura kurejesha miundombinu ya barabara na madaraja yaliyoharibika katika kipindi hiki cha mvua kubwa .

Akizungumzia athari za mvua hizo tarehe 28 Aprili 2024; Meneja wa TANROADS Mkoa wa Morogoro Mhandisi Alinanuswe L. Kyamba ameeleza kuwa tayari Wakandarasi wapo katika maeneo yote yaliyo athirika na kazi ya urejeshwaji wa miundombinu hiyo inaendelea.

"Mvua hizi sio Ulanga peke yake ni Nchi nzima, lakini kwa Ulanga Mwezi Februari liliondoka daraja katika Kijiji cha Mwaya daraja lile liliondoka kwa sababu ya mafuriko tukapeleka daraja la chuma la dharura, tumejenga daraja kwa wiki mbili kwa sasa hakuna shida  panapitika"

Ameainisha maeneo mengine yaliyo athiriwa na mvua hizo ni pamoja na Malinyi, Mlimba, Masagati na Uchendule ambapo pia ameeleza tuelewe kwamba mvua za mwaka huu zimekuwa kubwa kupita kiasi.

MWISHO
Share:

Saturday, April 27, 2024

SERIKALI YATOA BIL 1.5 UREJESHAJI MIUNDOMBINU YA BARABARA MWANZA








Serikali imetoa shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza urejeshaji wa miundombinu ya barabara zilizoharibika maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza.


Fedha hizo zimetolewa na serikali kwenda Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mwanza ili kuanza haraka kazi ya marekebisho miundombinu ya barabara na madaraja ambayo yameharibika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha


Meneja wa TANROADS Mkoa Wa Mwanza Mhandisi Paschal Ambrose ameyasema hayo wakati alipotembelea na kukagua uharibifu uliotokea kwenye barabara katika Wilaya za Nyamagana  na Misungwi ambapo pia ametumia fursa hiyo kukanusha uvumi ulioenezwa kwamba barabara katika eneo la Ng'ombe Wilayani Misungwi ni mbovu na haipitiki na amewataka wananachi kupuuza uvumi huo.


Amesisitiza kuwa Serikali imetoa fedha za dharura ambapo tayari wakandarasi wapo kazini wakiendelea na kazi.


Amesema miongoni mwa barabara zinazofanyiwa marekebisho ni barabara ya kutoka Mwanza kuelekea Musoma eneo la Nyamhongolo ambapo wanarekebisha mfereji ambao umeharibika kutokana na mvua hizo.


Mhandisi Ambrose amewataka wananchi wanaoishi karibu na barabara kuacha kufanya shughuli za kibinadamu kwenye kingo za barabara pamoja na kutupa taka ngumu katika mitaro hali inayosababisha mitaro kushindwa kupitisha maji pindi mvua zinaponyesha. 


Naye Mkandarasi anayefanya marekebisho katika maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza Mhandisi Stephen Mashauri kutoka  kampuni ya ujenzi ya MUMANGI CONSTRUCTION CO. LTD amewaondoa hofu wananchi wanaotumia barabara hizo kwamba zitarekebishwa kwa wakati ili ziweze kupitika muda wote. 


Aidha amewataka madereva wa vyombo vya moto kufuata alama zote, za barabarani zilizowekwa na TANROADS ili kuepuka ajali, huku akiwatahadharisha Wananchi wanaoiba miundombinu iliyowekwa barabarani na kwamba watakaobainika watachukulia hatua kali za kisheria.


MWISHO

Share:

Friday, April 26, 2024

TANROADS YAENDELEA NA UJENZI WA MIUNDOMBINU YA BARABARA GONGOLAMBOTO JIJINI DAR ES SALAAM

Serikali kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) imehakikisha utekelezaji wa mradi wa mabasi yaendayo haraka; barabara ya Nyerere hadi Gongo la mboto unaendelea huku barabara ya kawaida ikiendelea kupitika hata katika kipindi hiki cha mvua kubwa zinazoendelea kunyesha sehemu mbalimbali Nchini.

Akizungumza wakati alipofanya ziara katika mradi huo Meneja wa miradi ya mabasi yaendayo haraka (BRT-3) iliyopo chini ya Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mhandisi Frank Mbilinyi amesema amefanya ukaguzi wa kawaida kumuimiza mkandarasi kuhakikisha pamoja na athari za mvua lakini barabara inapitika wakati wote.

“Tumeendelea kumuhimiza mkandarasi kuhakikisha maeneo yote yanayotekelezwa mradi wa ujenzi wa barabara ya Nyerere - Gongolamboto yanapitika kiurahisi pamoja na athari za mvua kila baada ya mvua kukatika ahakikishe anaziba mashimo na kusawazisha ili kuwezesha kurejesha mawasiliano ya barabara japo kuna ujenzi unaendelea” Amesisitiza na kuongeza kuwa

“Tunashirikiana vizuri na mkandarasi kuhakikisha anapokea maelekezo pale anapokuwa amerudi nyuma tunakumbusha pamoja mhandisi elekezi ili kuhakikisha kazi inafanyika vyema” 

Aidha amewasa madereva wa magari kuhakikisha wanafuata sheria na taratibu za uendeshaji barabarani ili kuondoa changamoto wakati huu wa mvua kubwa.

MWISHO
Share:

TANROADS YAWEKA KAMBI BARABARA YA MOROGORO- IRINGA KUZIBA MASHIMO MAENEO YALIYOHARIBIWA NA MVUA


Na Aisha Malima-Morogoro

Serikali kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro inaendelea na kazi ya kuziba mashimo na kukarabati barabara kuu ya Morogoro – Iringa ikiwemo katika eneo la Kobogwa lilipo katika hifadhi ya Taifa ya Mikumi ambapo kumetokea shimo kubwa baada ya maji kupita pembezoni mwa Kalvati.

Akizungumza na Kipindi cha TANROADS Mkoa kwa Mkoa leo tarehe 26 Aprili 2024; Meneja wa TANROADS Mkoa wa Morogoro Mhandisi Alinanuswe L. Kyamba amesema kuwa tayari Mkandarasi yupo eneo hilo akiendelea na kazi ambapo mpaka kufika leo usiku kazi hiyo utakuwa imemalizika.

"Mvua zimeendelea kunyesha bila kukatika na jitihada zinaendelea kufanyika kila siku, eneo hili ambalo limeleta taharuki katika barabara hii ya Mikumi. Mashimo yametokea juzi, tukayaziba kidharura lakini unapoziba kidharura mvua zikinyesha tena zinaondoa ule mchanga ambao tumeuweka kwa sababu kipindi hiki cha mvua huwezi kuziba na lami, lami haikubali kipindi cha mvua mpaka jua liwake" Amekaririwa Mhandisi Kyamba na kusisitiza kuwa

“Tunaendelea na kazi ya kuziba mashimo yote kwenye barabara hii kuanzia Msamvu - Mikumi hadi Iringa mpaka tuyamalize kutokana na mvua kubwa kila siku mashimo yanajitokeza juzi hapa kwenye hili Kalvati maji yamepita pembeni yametengeneza shimo kubwa hapa katikati tukaanza kuleta mitambo na nyenzo za kazi, kwa sasa barabara inapitika upande mmoja na upande mwingine kazi inaendelea’’

Kwa upande wake Mhandisi Aloyce Stephen kutoka Kampuni ya Kizawa ya CGI Contractor Ltd inayofanya kazi hiyo amesema kazi imeendelea kufanyika bila kusababisha msongamano wa magari na matarajio ni kwamba magari yaemdelee kuruhusiwa kupita pande zote za barabara bila tatizo lolote.

Amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapa fursa na kuwajali Wakandarasi wazawa ikiwa ni pamoja na kuwapa malipo ya kazi kwa wakati jambo ambalo linawapa nguvu ya kuwa tayari kutekeleza majukumu yao wakati wote hata kwenye kazi za dharura kama hizo.

MWISHO
Share:

Wednesday, April 24, 2024

RAIS SAMIA AIPA TANROADS BIL 66 KUANZA UREJESHAJI MIUNDOMBINU YA BARABARA ILIYOHARIBIKA


Na Mathias Canal

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ametoa Bilioni 66 kwa ajili ya kuanza urejeshaji wa miundombinu ya barabara zilizoharibika nchini.

Fedha hizo tayari zimegawanywa kwa mameneja wa TANROADS mikoa yote iliyoathirika kwa ajili ya kufanya kazi kwa haraka usiku na mchana ili kurekebisha kadhia zilizozikumbumba barabara kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha nchini.
 
Akizungumza jana Jijini Arusha mara baada ya kukagua Barabara ya Afrika Mashariki (Arusha bypass) iliyoharibiwa na mvua hizo, Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mha. Mohamed Besta amesema kuwa kutokana na udharula huo tayari Rais Samia ametoa fedha za matengenezo ya miundiombinu hiyo ambazo zimeshapelekwa katika Mikoa yote Nchini.

Mhandisi Besta amesema kuwa tayari kazi inaendelea katika maeneo yote nchini na fedha hizo zinaratibiwa na vitengo maalumu vya dharula vilivyopo TANROADS pamoja na ofisi za mikoa.

Ameongeza kuwa kutokana na tathimini iliyofanyika mpaka sasa zaidi ya Shilingi Bilioni 250 zinahitajika kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya Barabara kuu za Mikoa yote Nchini ambazo zimeharibika vibaya kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha sehemu mbalimbali nchini.

Amesema kuwa kuna baadhi ya maeneo kama Kanda ya Ziwa na Nyanda za juu kusini mwa Nchi mvua zimeendelea kunyesha tangu mwezi Oktoba mwaka jana, na sasa unaelekea mwezi wa saba na mvua bado zinaendelea kunyesha.

 “Tunamshukuru Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani ametupatia shilingi bilioni 66 ambazo tumezisambaza katika Mikoa yote ambapo mameneja wote wa Mikoa wamepewa kutokana na hali ya dharura ya Mkoa husika’’ ameeleza

Naye Meneja wa TANROADS Mkoa wa Arusha Mhandisi Regnald Massawe amesema Mkoa huo umetengewa kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kazi hizo za dharura na matengenezo ya kurejesha miundombinu hiyo yanaendelea kufanyika kwa kasi.

MWISHO
Share:

Monday, April 1, 2024

BAADA YA UKAGUZI KIDATU, DKT. BITEKO ATUA KITUO CHA KUPOZA UMEME CHA ZUZU DODOMA


Baada ya ukaguzi wa matengenezo ya mitambo ya umeme Kidatu Mkoani Morogoro leo tarehe 1 Aprili, 2024 Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko ametembelea na kukagua Kituo cha kupoza umeme cha Zuzu kilichopo Jijini Dodoma.

Kituo cha kupoza Umeme cha Zuzu kilipata hitilafu kubwa baada ya Gridi ya Taifa kupata hitilafu kwenye mfumo wa kudhibiti kiwango cha maji kwenye mitambo na kusababisha mitambo kujizima kwa ghafla ili kujilinda jambo lililopelekea athari kwenye mfumo mzima wa Gridi ya Taifa na maeneo mbalimbali kukosa huduma ya umeme katika kipindi hiki cha mapumziko ya sikukuu ya Pasaka.

Dkt Biteko amewapongeza wataalamu kwa kazi kubwa ya kuendelea kufanya matengenezo ya haraka katika kituo cha kupoza Umeme cha Zuzu na maeneo yote yaliyokumbwa na kadhia hiyo kote nchini huku akisisitiza wataalamu kuendelea kukamilisha matengenezo kwa haraka ili umeme urejee maeneo yote ya nchi.

MWISHO
Share:

Wednesday, March 6, 2024

KADA WA CCM NEEMA MGHEN ACHANGIA MIFUKO 50 UJENZI WODI YA WAZAZI USHETU

Ushetu, Shinyanga...!

Kada wa Chama Cha Mapinduzi Wilayani Bi Neema Mghen amechangia mifuko 50 ya Saruji yenye thamani ya shilingi milioni 1,150,000/= Kwaajili ya ukamilishaji wa Jengo la wodi ya wazazi katika Zahati ya Sabasabini Halmashauri ya Ushetu.

Akizungumza wakati wa sherehe ya wanawake Duniani ambayo imeadhimishwa katika kijiji cha Sabasabini na jukwaa la Wanawake Halmashauri ya Ushetu huku ikiwa imeambatana na Harambee maalumu kwaajili ya ukamilishaji wa wa wodi hiyo.

Amesema kuwa mkakati huo ni kumuunga mkono Mhe. Rais katika utekelezaji wa miradi ya Maendeleo.

Mgheni amesema, lengo la maadhimisho hayo ni kutoa fursa kwa wanawake na wadau wengine kutafakari changamoto na mafanikio ili kuweka mikakati ya kuwainua wanawake kwa kuwekeza katika miradi mbalimbali ikiwemo Afya Elimu na Miundombinu.

Sambamba na hayo Mgheni amesema ni wajibu wa serikali kupitia Halmashauri kutunga sheria ndogo za kukabiliana na ukatili kwa wanawake na watoto lakini pia kuwaelimisha wanawake juu ya fursa za kiuchumi na wajibu wao.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ushetu Hadija Kabojela amesema, Jukwaa la Wanawake Ushetu kwa kutambua umuhimu wa wodi ya wazazi wameona ni vyema kusherehekea siku ya wanawaje dunia kwa kufanya harambee itakayo saidia upatikanaji wa fedha milioni 50 inayohitajika kukamilisha ujenzi wa wodi hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kata ya Sabasabini Diwani wa viti maalumu Felista Nyerere amesema, wodi hiyo ikikamilika itaondoa usumbufu kwa wanawake ambao wanahangaika sehemu ya kupumzika baada ya kujifungua kwakuwa hakuna sehemu nzuri ya kujifungulia hali inayofanya wakazi wa eneo kwenda umbali mrefu katika kata za Lowa na Bulungwa kutafuta usalama wa mazingira ya kujifungulia.

Harambee hiyo imehudhuliwa na Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Shinyanga Lucy Mayenga aliechangia mifuko 30 ya Saruji, Mbunge wa Ushetu Emmanuel Cherehani ambae amechangia fedha shilingi Milion 1 na Laki tatu, madiwani kupitia baraza lao wamechangia milioni 2 ambapo fedha iliyopatikana kwenye harambee hiyo ni shilingi Milioni 6,482,600 na sarufi mifuko 95 ambapo wodi hiyo itaipewa jina la Neema Mgheni.

MWISHO
Share:

Wednesday, February 21, 2024

UTEKELEZAJI MRADI WA TANZANIA YA KIDIJITALI WAFIKIA 70%-KATIBU MKUU WHMTH, MOHAMMED KHAMIS ABDULLA








Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Bw. Mohammed Khamis Abdulla amesema utekelezaji wa mradi wa Tanzania ya Kidijitali umefikia asilimia 70 na utekelezaji wake ni wa miaka mitano kuanzia 2021 hadi 2026.

Amesema mradi huo una malengo ya kuchochea mabadiliko ya kidijitali nchini, uundwaji wa mfumo wa namba moja ya utambulisho (jamii namba) mbayo itatumika kufanya utambuzi kuanzia mtu anapozaliwa ili kumwezesha mwananchi kupata huduma mbalimbali zikiwepo za afya, elimu, usafiri na nyinginezo pamoja na kuunganishwa katika mifumo ya vitambulisho vya Taifa, vyeti vya kuzaliwa na vinginevyo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari Mjini Zanzibar kuhusu mradi wa Tanzania ya Kidijitali, Bw. Abdulla amesema pamoja na mambo mengine, mradi huo pia utawezesha uundwaji wa mfumo wa kitaifa na uunganishwaji wa mifumo (National Enterprises Service Bus) utakaounganisha mifumo ya serikali na binafsi ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Tunalenga kuendelea kuboresha mfuko wa anwani za makazi na postikodi ili kuwezesha watoa huduma mbalimbali nchini, kuweza kutambua wateja wao kielektroniki na kuondoa adha ya mwananchi ya kwenda kila mara kuomba utambulisho kwenye serikali za mitaa, pia mradi huu utawezesha kupeleka mawasiliano ya mtandao wa simu kwenye maeneo ambayo hayakuwa na mawasiliano ambapo kwa sasa, Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inaendelea na ujenzi wa minara mipya ya simu 438 na upandishaji wa hadhi minara 304” amesema Bw. Abdulla.

Aidha amebainisha kuwa mradi huo utawezesha kuunganisha taasisi za Serikali 891 na mtandao wa mawasiliano ya Serikali (GovNet), ili kufikisha mawasiliano ya kimtandao kwenye ofisi hizo, zinazojumuisha hospitali, vituo vya afya, shule, mahakama, vituo vya polisi, vituo vya halmashauri, na taasisi za serikali.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Bi Khadija Khamis Rajab amesema Zanzaibar itanufaika na mradi huo kupitia marekebisho ya kanuni, sheria na sera ya TEHAMA ili kuendana na mabadiliko yake ambapo kwa sasa kupitia mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) tayari wamepata minara 42 ya mawasiliano.

“Kupitia mradi huu tutaweza kupata minara mingine ya nyongeza katika maeneo ambayo bado hayajaweza kufikiwa vizuri kwa upande wa mawasiliano, na hii tutafanya kutokana na ripoti ambazo tutazipata kupitia kwa wenzetu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), wao watatuambia ni minara mingapi na ni kwenye maeneo gani inahitajika, pia tutaweza kuimarisha minara ya mawasiliano ili iweze kuwa bora zaidi, na maeneo yote yaweze kufikiwa na huduma za mawasiliano mijini na vijijini” amesema Bi. Rajab. 

Amesema pia kutakuwa na mifumo 17 ambayo wataweza kunufaika nayo kupitia mradi huo kupitia vituo 159 ambavyo vitajumuisha shule, vituo vya afya, halmashauri na maeneo mengine ikiwemo taasisi za serikali.

Nae Afisa Mwandamizi wa Maendeleo ya kidijitali kutoka Benki ya Dunia Bw. Paul Seaden amesema lengo la Benki hiyo la kutoa Dola za Kimarekani milioni 150 ni kusaidia kuwezesha mradi huo ambao utaiwezesha Tanzania kuendelea katika mifumo ya mawasiliano ya kidijitali.

Mwisho.
Share:

Monday, February 19, 2024

TUNATEGEMEA MAFANIKIO MAKUBWA REA – BODI MPYA



Na Veronica Simba – REA

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) inayosimamia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imesema inategemea mafanikio makubwa katika kuiwezesha Wakala hiyo kutimiza azma yake ya kuwafikishia wananchi walioko vijijini nishati bora za umeme, mafuta na gesi.

Hayo yamebainishwa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Balozi, Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu baada ya kikao cha kwanza cha Bodi hiyo mpya kilicholenga kutambuana na kupanga majukumu.

“Kikao chetu kimeenda vizuri, tumechagua Kamati na kupangiana majukumu. Tunaamini na tunaahidi kuwa tutatekeleza majukumu yetu sawasawa na Sheria iliyoanzisha Wakala wa Nishati Vijijini inavyoelekeza,” amesema.

Aidha, Balozi Kingu amemshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumteua kuwa Mwenyekiti wa Bodi na amemshukuru Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ndiye Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko kwa kukamilisha mchakato wa uteuzi wa Wajumbe wa Bodi, jambo ambalo limeiwezesha kuwa Bodi kamili.

Akieleza zaidi kuhusu majukumu waliyojipangia, Balozi Kingu amesema mapema Mwezi Machi, Bodi itakutana katika kikao cha dharura kupitia na kujadili masuala mbalimbali ya Wakala ambayo yalikuwa yakisuburi baraka za Bodi ili kuyatolea maamuzi yatakayowezesha utekelezaji wake kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Katibu wa Bodi hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa REA, Mhandisi Hassan Saidy amepongeza Mamlaka za Uteuzi, kuteua watu makini, hodari na wachapakazi ambao amesema ni muhimu kuwa nao katika kuisimamia Wakala hiyo yenye majukumu makubwa yanayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

“REA ina jukumu kubwa ambalo linagusa maisha ya watu lakini pia linahusisha kiasi kikubwa sana cha fedha za Serikali. Kwahiyo, kuwa na Bodi nzuri iliyosheheni watu makini, kwetu sisi ni jambo la faraja,” amefafanua.

Mkurugenzi Mkuu, kwa niaba ya Menejimenti na Wafanyakazi wote wa REA, ametoa ahadi ya ushirikiano kwa Bodi hiyo mpya ili kuhakikisha malengo ya Serikali kupitia majukumu yaliyokasimiwa kwa Wakala yanatekelezwa.

“Tunatamani kuona Watanzania wenzetu wanaoishi vijijini wanapata nishati bora kama ilivyo kwa wenzao wanaoishi mjini,” amesisitiza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Wajumbe wa Bodi wamezishukuru Mamlaka za Uteuzi kwa kuwaamini na kuwapa jukumu hilo kubwa la kuisimamia REA ili kuendelea kuleta matokeo chanya.

Aidha, wamepongeza Bodi zilizotangulia kabla yao, Menejementi pamoja na Wafanyakazi wote kwa kazi nzuri waliyofanya tangu kuanzishwa kwa Wakala na kuahidi kuendeleza yote mazuri yaliyofanyika ili kuongeza tija.

Kikao hicho pia kilishirikisha Menejimenti ya Wakala ambapo Wakuu wa Idara na Vitengo waliwasilisha kwa Bodi taarifa za utekelezaji wa majukumu katika maeneo wanayosimamia kwa lengo la kuijengea Bodi uelewa na ufahamu kuhusu Taasisi hiyo waliyopewa jukumu la kuisimamia.

Januari 26 mwaka huu, Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko aliwateua Florian Otman Haule, Lucas Charles Malunde, Mwantum Issa Sultan, Stephen Menard Mwakifamba, James Issack Mabula, Ahmed Martin Chinemba, Sophia Shaban Mgonja na Balozi Radhiya Naima Msuya kuwa Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini, wakiungana na Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Gideon Kingu aliyeteuliwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Septemba 2023 kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo.

Share:

Serikali, Benki ya Dunia wakutana kujadili mradi wa Tanzania ya Kidijitali

Serikali ya Tanzania na Benki ya Dunia-WB, wanaendelea na majadiliano ya namna ya utekelezaji wa mradi wa Tanzania ya kidijitali, ambapo wataalam kutoka katika Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Zanzibar pamoja na taasisi mbalimbali za Umma, wamekutana mjini Zanzibar kwa ajili ya majadiliano hayo.

Mradi huo unatarajia kutekelezwa kwa gharama ya dola za kimarekani milioni 150 sawa na shilingi Bilioni 348 za kitanzania na unatazamiwa kuboresha na kuimarisha huduma za mawasiliano nchini. 

Ni katika mkutano wa tatu wa kikao cha utekelezaji wa Tanzania ya Kidijitali kwa mwaka wa fedha 2023/2024 ulioanza februari 19 hadi 23 mwaka huu mjini Zanzibar, ambapo pamoja na mambo mengine, mkutano huo utajadili malengo ya kuongeza upatikanaji wa huduma za mtandao wa intaneti zenye gharama nafuu na ubora wa juu kwa serikali, wafanyabiashara na wananchi sambamba na kuboresha uwezo wa serikali wa kutoa huduma za umma kidijitali.

Akizungumza wakati akifungua mkutano huo, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bi. Khadija Khamis Rajab, amesema matarajio ya serikali ni kwamba miradi ya kimkakati katika sekta ya mawasiliano itatekelezwa.

“Tunatarajia mradi huu utaenda kutekeleza mambo makubwa ili tuweze kutekeleza miradi mingine ya kimkakati katika sekta yetu hii ya mawasiliano, tuna maeneo mengi ya msingi ambayo yatakuwa yamegawanywa katika mradi huu wa Tanzania ya kidijitali, na katika maeneo hayo kutakuwa na maeneo makuu matatu ambayo ni pamoja na kupitia na kuhuisha sheria miongozo na taratibu za kisheria za TEHAMA ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia” amesema Ndugu. Rajab.

Meneja wa mradi huo wa Tanzania ya Kidijitali Bw. Bakari Mwamgugu amesema pia kutakuwa na maboresho ya miundombinu ya TEHAMA, ikiwepo kuunganisha taasisi za serikali katika mkongo wa mawasiliano taifa, kuboresha vituo vya kuhifadhia kanzidata, na kupeleka mawasiliano katika maeneo ambayo hakuna mawasiliano ikiwa ni pamoja na kuboresha mawasiliano kutoka 2G kwenda 4G.

“Lengo la tatu ni kuboresha na kutekeleza mifumo mbalimbali itakayosaidia kutoa huduma bora kwa wananchi na kwa wakati, ukiwepo mfumo wa jamii namba, ambao kila mtanzania atatakiwa kuwa na namba moja tu ya kupata huduma” amesema Bw. Bakari.

Mradi huo una malengo ya kuongeza upatikanaji wa huduma za mtandao wa intaneti zenye gharama nafuu na ubora wa juu kwa serikali, wafanyabiashara na wananchi, sambamba na kuboresha uwezo wa serikali wa kutoa huduma za umma kidijitali.

Mradi wa ‘Tanzania ya Kidijitali' unaofadhiliwa na Benki ya Dunia unatekelezwa kwa usimamizi wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Pamoja na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kushirikiana na Taasisi mbalimbali zinazohusika na TEHAMA kwa upande wa Tanzania Bara na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Mwisho.
Share:
Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com