METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, December 2, 2025

BASHUNGWA: NINA MUDA WA ZIADA KUWAHUDUMIA WANANCHI WA KARAGWE.

 

Na Mwandishi Wetu- Karagwe 


‎📌 Baraza la Madiwani kupitia upya tozo kandamizi kwa Wakulima.

‎Mbunge wa Jimbo la Karagwe, Innocent Bashungwa, amewahakikishia wananchi wa Wilaya ya Karagwe kuwa ataendelea kushirikiana kwa ukaribu na Madiwani katika kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo, pamoja na kutatua changamoto na mahitaji ya wananchi ambapo ameeleza kuwa kipindi hiki kinampa nafasi na muda mpana zaidi wa kuwatumikia kwa ufanisi kama mwakilishi wao ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

‎ Ameitoa kauli hiyo leo, tarehe 2 Desemba 2025, katika kikao cha kwanza cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe, kikao kilichohusisha viapo vya madiwani pamoja na uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri.

‎Bashungwa amesema kuwa katika kipindi hiki ameendelea kuboresha Ofisi ya Mbunge ili kuwasogelea na kuwahudumia wananchi kwa ukaribu zaidi ambapo atafungua ofisi mbili ndogo za Mbunge katika maeneo ya Rwambaizi na Nyaishozi, na tayari amenunua magari mawili aina ya “pickup” kwa ajili ya kuimarisha huduma kwa wananchi.

‎“Kipindi hiki ambacho nimepata muda wa ziada, niwahakikishie Wanakaragwe, kazi hii ya Ubunge niliiomba kutoka kwenu, mkaniamini na mnaendelea kuniamini. Nitatumia muda huu, hata kama ni kutembea kwa miguu au kwa njia yoyote ile, kufika kwenye vitongoji na vijiji vyote kuhakikisha tunasimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi,” amesisitiza Bashungwa.

‎Bashungwa amesema watashughulikia kero ya tozo kandamizi zinazowaumiza wakulima wanapopeleka mazao yao kwenye masoko na magulio kwa kushirikiana na Madiwani kuhakikisha zinapitiwa upya na kufanyiwa maboresho, sambamba na kuisimamia Halmashauri kufanya marekebisho ya kanuni ili kuondoa vikwazo vinavyowanyima wananchi tija na ustawi katika shughuli zao.

‎Aidha, Bashungwa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa imani aliyomwonyesha katika kipindi kilichopita kwa kumpatia majukumu mbalimbali ya kuwatumikia Watanzania katika Serikali ya Awamu ya Sita.

‎Pia, amewashukuru wananchi wa Wilaya ya Karagwe kwa kumchagua Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mbunge pamoja na Madiwani wa Chama Cha Mapinduzi katika uchaguzi uliofanyika tarehe 29 Oktoba 2025.

‎Akizungumzia miradi ya maendeleo, Bashungwa amesema ataendelea kushirikiana na Madiwani kusimamia kikamilifu miradi inayoendelea na ile mipya itakayoanza kutekelezwa katika Wilaya ya Karagwe, ikiwemo ujenzi wa Soko la Kisasa Kayanga na ujenzi wa stendi mpya ya Kishao.

‎Katika hatua nyingine, Bashungwa amewapongeza Mwenyekiti mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe, Longino W. Rwenduru (Diwani wa Kata ya Chanika), pamoja na Makamu Mwenyekiti, Adriani R. Kobushoke (Diwani wa Kata ya Rugu), kwa kuchaguliwa kwa asilimia mia moja kuongoza Baraza la Madiwani.






Share:

Saturday, November 29, 2025

MHE. NDEJEMBI AWAHAKIKISHIA WAKAZI WA KIGAMBONI UMEME WA UHAKIKA


 ‎📌Afanya Ziara katika Kituo cha Dege 

‎📌Aelekeza hatua za haraka kuchukuliwa kunusuru hali ya umeme Kigamboni

‎📌Umeme wa Megawati 22 kupatikana kwa hatua za haraka 

‎📌Upanuzi wa Kituo cha Dege wafikia asilimia 60 

‎Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi amefanya ziara ya kikazi ndani ya Mkoa wa kitanesco wa Kigamboni na kuagiza kuchukuliwa hatua za haraka za kuhakikisha hali ya umeme katika Mkoa wa Kigamboni inaboreshwa na kuwapa wakazi wa eneo hilo huduma ya uhakika alipotembelea Kituo cha Kupokea, Kupoza na Kusambaza umeme cha Dege tarehe 29 Novemba, 2025.

‎“Leo tumekuja kuona ni namna gani Shirika letu la TANESCO linaweza kutatua changamoto hii kwa haraka zaidi na wameweka mipango mizuri ya muda mrefu katika kuhakikisha wanawezesha kupatikana kwa umeme wa uhakika kwa kujenga na kukiongezea nguvu Kituo cha Dege kwa kuweka transfoma ya MVA 120”, ameeleza Mhe. Ndejembi. 

‎Ili kukabiliana na changamoto ya huduma ya umeme iliyopo kwa haraka, Shirika limekuja na suluhisho la haraka kwa kujenga laini itakayosafirisha umeme kutoka Kituo cha Mbagala wa Megawati 22 kuja Kigamboni kuongeza upatikanaji wa umeme kwa Wananchi wa Kigamboni.

‎“Kwa hatua za haraka TANESCO wamenihakikishia kwamba kuna laini ya umeme ambayo italeta Megawati 22 kutoka Mbagala kuja Kigamboni ili kuongeza upatikanaji wa umeme kwa wakazi wa Kigamboni”, ameongeza Mhe. Ndejembi.

‎Sambamba na mikakati ya muda mrefu ya kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme TANESCO imechukua hatua za haraka kunusuru kadhia hiyo kwa kuweka transfoma 93 ili kuondoa changamoto ya umeme mdogo pamoja na uzoezi la usimikaji wa transfoma 50 ambazo hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Machi, 2026 zitakuwa zimekamilika na kupunguza athari za kukosa umeme mara kwa mara.

‎“Kwa sasa ili kuondokana na changamoto hii, TANESCO imeanza kuweka transfoma kwa ajili ya kuondokana na hali ya umeme mdogo na pia wanaongeza transfoma zingine 50 kwa ajili ya kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme ambapo hadi kufika mwishoni mwa mwezi Machi,2026 zitakuwa zimekamilika kufungwa”, aliongeza. ‎

‎Naye Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Mhe. Mikaya Dalmia amemshukuru Waziri wa Nishati kwa kufanya ziara yake katika Wilaya hiyo na kuelekeza Shirika kutekeleza kwa haraka juhudi za kuhakikisha upatikanaji wa umeme katika wilaya hiyo na kumuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa TANESCO kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma ya umeme. ‎

‎“Nitoe shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa ziara yenye matokeo chanya katika Wilaya yetu ya Kigamboni. Nikuahidi kuwa nitaendelea kushirikiana kwa karibu na wenzetu wa TANESCO katika kuwahudumia wananchi wa Kigamboni na kuhakikisha wanapata huduma bora ya umeme na pia nawasihi wananchi kuendelea kuwa wavumilivu wakati changamoto hizi zinafanyiwa kazi na Shirika”, alieleza Mhe. Mikaya‎

‎Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi Mtendaji Usambazaji Umeme wa TANESCO Mha. Athanasius Nangali amemhakikishia Waziri wa Nishati kuwa kama Shirika wataendelea kufanyia kazi maelekezo yake na kuwa hatua za kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme ndani ya Mkoa wa Kigamboni zinaanza mara moja ili kuimarisha huduma hiyo. ‎

‎“Kama Shirika tutahakikisha kuwa tunafanyia kazi mara moja maelekezo tuliyopewa leo kwa kufunga transfoma na kuleta Megawati 22 Kigamboni kutoka mikoa ya Jirani ili kuimarisha hali ya umeme ndani ya Kigamboni”, alieleza Mha. Nangali.‎

‎Ziara ya Mhe. Ndejembi imelenga kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme ndani ya Wilaya hiyo ikiwemo upanuzi wa Kituo cha Dege ambacho kukamilika kwake kutaipa Kigamboni umeme wa kutosha kuendesha shughuli za kiuchumi na kijamii.




Share:

Tuesday, August 5, 2025

TPHPA Yadhibiti Kweleakwelea kwa Mafanikio, Yaweka Mkakati wa Kilimo Salama kwa 2030

 





Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imeongeza jitihada katika kudhibiti uvamizi wa visumbufu hatarishi, ikiwemo kweleakwelea, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuboresha kilimo na kutekeleza Agenda 10/30   mpango wa kitaifa unaolenga kuongeza tija na ustawi katika sekta ya kilimo hadi kufikia mwaka 2030.

Kweleakwelea ni ndege vamizi anayeshambulia na kuharibu mazao kama mpunga, alizeti, na nafaka nyingine, hivyo kuhatarisha usalama wa chakula na kupunguza kipato cha wakulima. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, TPHPA kupitia wataalamu wake wa Kanda ya Mashariki imeweka mikakati madhubuti ya ufuatiliaji, tathmini, na udhibiti wa kweleakwelea kabla haijasababisha madhara makubwa mashambani.

Akizungumza katika banda la TPHPA kwenye Maonesho ya Nanenane yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. Julius Nyerere  Morogoro, Dkt. Mahudu Sasamalo, Mkuu wa Kanda ya Mashariki, alieleza kuwa TPHPA imeendelea kudhibiti kwa mafanikio maeneo yaliyoathiriwa, ikiwemo Ifakara, Kilosa, Mvomero, na Bagamoyo, ambapo maelfu ya hekta zimeokolewa na mazao ya wakulima kuendelea kustawi.

“Kupitia juhudi hizi za kisayansi na kijamii, tunalenga kuhakikisha wakulima wa Tanzania wanapata mazingira salama ya kilimo bila kutishiwa na visumbufu vya mimea. Hii ni sehemu ya azma ya Serikali ya kuhakikisha kilimo kinakuwa cha kisasa, chenye tija, na chenye mchango mkubwa katika pato la taifa,” alisema Dkt. Sasamalo.

Katika kuendeleza utekelezaji wa Agenda 10/30, inayolenga kuhakikisha kilimo kinachangia angalau asilimia 10 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2030, TPHPA inaendelea kuwekeza katika teknolojia, elimu kwa wakulima, na udhibiti endelevu wa visumbufu mashambani, ikiwemo matumizi ya mbinu rafiki kwa mazingira.

Wananchi na wadau wa kilimo mkoani Morogoro mnakaribishwa kutembelea banda la TPHPA kwenye Maonesho ya Nanenane ili kujifunza zaidi kuhusu mbinu za kisasa za kulinda afya ya mimea na mchango wa Mamlaka katika kuendeleza kilimo bora na biashara ya mazao nchini.

Share:

Friday, July 18, 2025

TPHPA Yachukua Hatua Kunusuru Ikolojia ya Ziwa Victoria Dhidi ya Gugu Maji

 














Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) kupitia maabara zake za kisasa zilizopo katika Kituo cha Udhibiti wa Visumbufu vya Mimea Kibiolojia, Kibaha, mkoani Pwani, imeanza kuzalisha mdudu rafiki wa mazingira aina ya "mbawa kavu" (Cyrtobagous salviniae) kwa ajili ya kudhibiti gugu maji vamizi  (Salvinia molesta). Gugu hilo limekuwa tatizo kubwa katika Ziwa Victoria na vyanzo vingine vya maji hapa nchini, likisababisha athari kwa usafiri, mazingira, uchumi na maisha ya jamii zinazotegemea ziwa hilo.


Akizungumza wakati wa ukaguzi wa zoezi hilo, tarehe 18 Julai 2025, Mkurugenzu wa  Usalama wa Afya ya Mimea TPHPA, Dkt. Benignus Ngowi, amesema matumizi ya mdudu rafiki huyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa kutumia mbinu za kibaiolojia kudhibiti visumbufu bila kuathiri mazingira. Alibainisha kuwa njia hiyo ni salama, rafiki kwa viumbe hai wengine na inaweza kusaidia kupunguza gharama kubwa zinazotumika katika kudhibiti magugu hayo.


Kwa upande wake, Ndugu Keneth Nyakunga, mtaalamu na afisa mwandamizi wa udhibiti wa visumbufu kwa njia ya kibaiolojia  alisema kuwa mdudu rafiki  huyo “mbawa kavu” (Cyrtobagous salviniae) waliletwa kwa ushirikiano na Serikali ya Uganda, ambako tayari wametumika kwa mafanikio makubwa nchini Uganda katika kudhibiti gugu maji vamizi (Salvinia molesta). Kwa upanda wa Tanzania  kwa sasa wapo katika hatua ya kumchunguza kwa kina tabia zake ikiwa ni pamoja na usalama wake katika mazingira pamoja na ufanisi na baadae kuwazalisha  kwa wingi kabla ya kuanza kuwasambaza katika maeneo yaliyoathirika zaidi na gugu hilo, ili kudhibiti tatizo hilo kwa ufanisi na kwa njia endelevu.

Share:

Thursday, May 29, 2025

Dondoo za Aliyoyasema Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde katika Mkutano na Wahariri wa Vyombo vya Habari, Mei 24, 2025 Jijini Dar es Salaam.

 











Mada: Mafanikio ya Sekta ya Madini katika Kipindi cha Miaka Minne ya Uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan

1. Ongezeko la Bajeti – Bajeti ya Wizara ya Madini imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka. Kutoka shilingi bilioni 89 mwaka wa fedha 2023/2024 hadi shilingi bilioni 231 kwa mwaka 2024/2025. Kwa mwaka ujao wa fedha 2025/2026, tumeidhinishiwa bajeti ya shilingi bilioni 224. Asilimia kubwa ya bajeti hii inaelekezwa kwenye Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kwa ajili ya kufanya tafiti za kina za jiolojia na ujenzi wa maabara ya kisasa ya uchambuzi wa madini katika eneo la Kizota, Dodoma. Lengo ni kuifanya GST kuwa kitovu cha huduma za maabara ya madini kwa Afrika nzima. Pia, maabara nyingine zinajengwa katika mikoa ya Geita na Chunya (Mbeya) ili kuboresha huduma za uchambuzi wa madini nchini.

2. Ongezeko la GDP – Mchango wa Sekta ya Madini katika pato la taifa (GDP) umeongezeka kwa kiwango kikubwa. Sera ya Madini ya mwaka 2009 pamoja na Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo kwa Miaka Mitano unalenga sekta kuchangia angalau asilimia 10 ya GDP ifikapo mwaka 2025. Hadi kufikia Desemba 2024, mwaka mmoja kabla ya muda uliopangwa, sekta ya madini tayari ilikuwa imefikia mchango wa asilimia 10.1, hatua ambayo ni ya kihistoria na ya kujivunia.

3. Mining Vision 2030: Kauli mbiu ya mpango huu ni “Madini ni Maisha na Utajiri.” Mpango huu unalenga kuongeza kiwango cha tafiti za kina za madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030. Sekta ya madini pia inatajwa kuwa kichocheo kikuu cha sekta nyingine kama maji, kilimo, afya, viwanda, ujenzi na uchumi kwa ujumla. Kwa sasa sekta imechangia mzunguko wa fedha wa takribani trilioni 1.7 na mauzo yamefikia asilimia 56.2 ya jumla ya mauzo nje ya nchi.

4. Maduhuli – Katika mwaka wa fedha 2015/2016, sekta ya madini ilikusanya maduhuli ya shilingi bilioni 162. Makusanyo haya yameongezeka kwa kasi hadi kufikia bilioni 678 mwaka 2022/2023, na bilioni 753 mwaka 2023/2024. Kwa mwaka huu wa fedha 2024/2025, tumewekewa lengo la kukusanya shilingi trilioni 1. Hadi kufikia tarehe 24 Mei 2025, tayari tumekusanya shilingi bilioni 930, ikiwa ni mafanikio makubwa huku zikiwa zimebaki siku 37 kabla mwaka wa fedha kumalizika.

5. BOT yaanza ununuzi wa Dhahabu – Kufuatia marekebisho ya Sheria ya Madini mwaka 2024, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imeanza rasmi kununua dhahabu kutoka kwa wazalishaji wa ndani. Sheria sasa inawataka wamiliki wote wa leseni za uchimbaji wa dhahabu kutenga angalau asilimia 20 ya uzalishaji wao kwa ajili ya kuuza BoT. Kuanzia Oktoba 2024 hadi sasa (miezi 8), BoT imenunua tani 3.7 za dhahabu. Kwa hatua hii, Tanzania inajiweka kwenye nafasi nzuri kuwa miongoni mwa nchi zenye akiba kubwa ya dhahabu barani Afrika – mfano, hivisasa Algeria barani Afrika inaongoza kwa kuwa na akiba ya tani 174, na Msumbiji iko nafasi ya 10 kwa tani 3.6.

6. Uwezeshwaji Wachimbaji Wadogo – Wachimbaji wadogo hivi sasa wanachangia asilimia 40 ya mapato yote yatokanayo na sekta ya madini. Serikali imefuta leseni na maombi 2,648 ili kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata maeneo halali ya uchimbaji. Shirika la STAMICO limejipambanua kuwa mlezi wao, ambapo limewanunulia mashine 15 za kuchoronga miamba (drilling rigs). Pia, Serikali imefanya mazungumzo na benki mbalimbali kuwahamasisha kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambapo sasa wanakopesheka. Tumeunda timu ya wataalam sita kutoka sekta binafsi na serikali kwa ajili ya kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu namna bora ya kuwainua wachimbaji wadogo. Kupitia Mfuko wa Dhamana wa Hazina (Credit Guarantee Scheme), wachache wataanza kunufaika na matarajio ni kueneza huduma hiyo kwa wengi zaidi.

7. Viwanda vya kuongeza thamani – Kifungu cha 100 cha Sheria ya Madini kinawataka wawekezaji wanaoomba leseni kuwa na mpango wa kuongeza thamani ya madini. Eneo la Mgodi wa Buzwagi (unaofungwa baada ya kusitisha shughuli za uchimbaji) limegeuzwa kuwa eneo maalum la uwekezaji wa viwanda (Special Economic Zone). Moja ya viwanda vitakavyojengwa ni pamoja na Kiwanda cha Kusafisha Makinikia cha Tembo Nickel Refining Limited, hatua inayolenga kuongeza thamani ya madini ya nickel na ajira nchini.

8. Minada ya Vito – Serikali imerejesha rasmi minada ya ndani ya madini ya vito kwa lengo la kuongeza thamani ya madini haya, hasa Tanzanite ambayo ni adimu duniani. Tumefanya minada Mirerani mwezi Desemba 2024 na Arusha Februari 2025, juhudi hizi pia ni sehemu ya rebranding ya Tanzanite ili kutambulika zaidi kimataifa.

9. Marekebisho ya Sheria – tumefanya marekebisho ya Sheria mwaka 2024, ambapo sasa inabainisha kuwa leseni za uchimbaji mdogo wa madini ni kwa ajili ya Watanzania pekee. Hata hivyo, msaada wa kitaalamu kutoka kwa wageni unaruhusiwa kwa masharti maalum, ikiwemo mkataba rasmi unaopitiwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini ili kuhakikisha Watanzania wananufaika. Pia, Marekebisho haya yamepunguza migogoro mingi kati ya wachimbaji wadogo na wawekezaji.

10. Miradi Mikubwa – Serikali inaendelea kusimamia na kuvutia uwekezaji kwenye migodi mikubwa kama ule wa Nyanzaga uliopo wilayani Sengerema.

11. STAMICO – Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limepiga hatua kubwa kutoka kuingiza mapato ya shilingi bilioni 1 hadi bilioni 84 ndani ya kipindi cha miaka minne. Hivi sasa shirika linajilipa  mishahara lenyewe, linatoa gawio Serikalini na limepanga kuanzisha miradi mikubwa ya kimkakati kuanzia mwaka wa fedha ujao ili taifa linufaike zaidi. Kuna pia mpango wa kuanzisha kampuni tanzu ya miradi.

12. Local Content & CSR – Ajira kwa Watanzania kwenye sekta ya madini zimeongezeka. Kwa sasa ajira za moja kwa moja ni zaidi ya 19,356, ambapo asilimia 97 ya ajira hizo ni kwa Watanzania. Watanzania pia wanashikilia nafasi nyingi za juu kwenye migodi. Aidha, wameanza kutoa huduma muhimu kama vile utengenezaji wa vifaa vya migodini, hatua ambayo inachochea uchumi wa ndani.

13. Madini Mkakati – Serikali iko mbioni kukamilisha mkakati maalum wa namna ya kuyavuna na kuyaendeleza madini mkakati kama vile graphite, nickel, rare earths n.k., kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo.

14. MBT – Mining for a Brighter Tomorrow – Mpango huu unalenga kusaidia makundi ya wanawake na vijana kwa kuwapatia leseni na maeneo ya uchimbaji. Tayari tumeanza Nyamongo, mkoa wa Mara, kwa kugawa zaidi ya leseni 48 kwa wachimbaji zaidi ya 2000, na wadau mbalimbali wameonyesha nia ya kushiriki katika kuwawezesha makundi haya.

15. Vituo vya Ukodishaji Mitambo – Serikali imeanzisha vituo vya ukodishaji wa mitambo ya kisasa kwa bei nafuu ili kuwasaidia wachimbaji wadogo kuchimba kwa tija na kwa ufanisi zaidi.

16. Gold Coins – Serikali ipo kwenye mazungumzo na Benki Kuu ya Tanzania kuhusu kuanzisha sarafu za dhahabu (Gold Coins) kwa ajili ya uwekezaji na akiba ya thamani. Lengo ni kuwawezesha Watanzania kuhifadhi dhahabu benki na kuitumia kwa malipo kama vile mafuta ya petroli na dizeli.

17. Vikao vya majadiliano na wawekezaji – Serikali inaendelea kufanya vikao vya wazi na wawekezaji wa Sekta ya Madini – wa Kati na Wakubwa – ili kusikiliza changamoto zao na kuzitatua kwa wakati, kwa lengo la kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini.

18. Masoko na vituo vya ununuzi – Serikali imeimarisha upatikanaji wa masoko ya uhakika kwa wachimbaji wadogo kupitia vituo vya ununuzi wa madini. Hatua hii inalenga kuwapa wachimbaji bei nzuri, kuwasaidia kupata mapato ya haki na kudhibiti utoroshaji wa madini nje ya mfumo rasmi. Tuna masoko 43 nchi nzima na Vituo vya Ununuzi 109.

19. Mahusiano ya Kimataifa (MoUs) – Wizara ya Madini imesaini mikataba ya ushirikiano na nchi mbalimbali ikiwemo Uingereza (UK), Sweden, Finland na nyingine nyingi kwa ajili ya kukuza ujuzi, teknolojia na kupata mitaji kwa ajili ya maendeleo ya sekta kwa manufaa ya taifa.

Share:

Tuesday, May 20, 2025

DC WILAYA YA ARUSHA AWATAKA WAFANYABIASHARA KUSHIRIKIANA NA TRA KATIKA MASUALA YA KODI.









WAZOHURU ARUSHA:

Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mhe. Joseph Modestus Mkude amewataka wafanyabiashara Wilayani hapo kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania ikiwemo kulipa kodi zao stahiki kwa hiari na kwa wakati.

Mkuu wa Wilaya hiyo ameyasema hayo tarehe 19 Mei, 2025 wakati alipokutana na Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambao wapo mkoani Arusha kwa ajili ya kampeni ya elimu kwa Mlipakodi ya mlango kwa mlango.

Aidha, amesema kuwa kodi mbalimbali zinazolipwa na wananchi wa eneo hilo ndizo zinasaidia katika kuleta maendeleo nchini ikiwemo katika sekta ya elimu, afya na ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchini.

Baadhi ya wafanyabiashara wilayani hapo wameiomba TRA kuendeleza elimu ya kodi ikiwemo kuskiliza kero zao za kikodi na wameahidi kuonesha ushirikiano kwa TRA ili waweze kulipa kodi zao stahiki.

Kampeni ya elimu kwa Mlipakodi ya mlango kwa mlango ni zoezi endelevu linalofanywa na TRA katika mikoa mbalimbali nchini kwa lengo la kuwaelimisha walipakodi kuhusu masuala ya kodi ili waweze kulipa kodi zao kwa hiari kwa ajili ya maendeleo ya nchi ambapo kwa sasa kampeni hiyo inafanyika katika Mikoa ya Arusha, Iringa na Pwani.

Share:

Tuesday, February 18, 2025

REA YAENDELEA KUSAMBAZA MITUNGI YA GESI 16,275 MKOANI SIMIYU







WazoHuru - Simiyu

Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Kenani Kihongosi, leo tarehe 18 Februari, 2025 amezindua rasmi zoezi la usambazaji wa mitungi ya gesi ya kilo 6 katika mkoa wa Simiyu na kutoa wito kwa Wananchi kuchangamkia fursa ya matumizi ya nishati safi kama njia mbadala ya kupunguza uharibifu wa mazingira, uliochangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya kuni na mkaa.

Mhe. Kenani amesema kuwa lengo la Serikali ni kuhamasisha matumizi ya nishati safi ili kulinda afya za Watanzania pamoja na kutunza mazingira ambapo amewahamasisha Wananchi wa mkoa wa Simiyu kununua mitungi hiyo ya gesi pamoja na vifaa vyake; mitungi inayosambazwa na kampuni ya ORYX Gas.

“Utekelezaji wa Mradi huu, unaunga mkono Mpango Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo, lengo ni kuhakikisha kuwa angalau asilimia 80 ya Watanzania, wawe wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.” Amesema Mhe. Kihongosi.

Usambazaji wa mitungi hiyo ya gesi unatekelezwa kwa pamoja kati ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na kampuni ya Oryx Gas Tanzania Limited, ambapo Wananchi wanapata fursa ya kukunua mitungi hiyo gesi ya kilo 6 kwa shilingi (20,000); bei ya ruzuku na kiasi kilichobaki kitalipwa na Serikali kupitia REA.

Naye Mhandisi wa Miradi ya Nishati Safi kutoka REA, Geofrey Gedo amesema Serikali, imedhamiria kuhakikisha Wanachi waliopo katika maeneo ya vijijini na pembezoni mwa miji wanatumia nishati safi ya kupikia.

“Serikali ya Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imetenga fedha, takribani shilingi za Kitanzania milioni 325 kwa ajili ya utekelezaji miradi ya kuhamasisha matumizi ya gesi ya kupikia (LPG) kwa mkoa wa Simiyu.

“Mradi pia, unalenga katika kukuza, kuchochea, kuwezesha na kuboresha upatikanaji wa huduma za nishati safi ya kupikia ili kupunguza ukataji miti,ambapo takribani hekta laki 4 (400,000) hukatwa kila mwaka; wakati asilimia 63.5 ya kaya hutumia kuni kama chanzo kikuu cha nishati na asilimia 26.2 hutumia mkaa.

Mhandisi, Gedo ameongeza kuwa mitungi 16,275 itauzwa kwa bei ya punguzo ya asilimia 50 ambayo ni shilingi 20,000 katika mkoa wa Simiyu na kila wilaya ipata mitungi 3,255.

Wilaya za mkoa Simiyu zitakazonufaika na usambazaji huo ni pamoja na wilaya ya Maswa, Bariadi, Itilima, Meatu na Busega.

Mhandisi, Gedo ameongeza kuwa ili Wananchi wapate mitungi hiyo wanatakiwa kuwa na Kitambulisho cha NIDA pamoja na shilingi (20,000) na watakapofika katika vituo vya kuuzia mitungi hiyo wataulizwa majina yao, jinsia; namba ya nida; mkoa, wilaya, kata, kijiji na kitongoji /mtaa anapoishi.

“Natoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi ili kufanikisha zoezi hili na baada ya kununua mitungi hii; wanunue na kuendelea kutumia nishati ya gesi.

Share:

Saturday, November 30, 2024

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Aahidi Kutatua Changamoto za Tanganyika Farmers Association (TFA) ili Kuongeza Faida kwa Wakulima













Leo, Novemba 30, 2024, Arusha ilikua jiji lenye hafla muhimu kwa wakulima wa Mkoa wa Arusha na maeneo mengine ya Tanzania. Ambapo mkutano mkuu wa wanahisa wa Tanganyika Farmers Association (TFA) ulifanyika katika viwanja vya Shopping Mall, ambapo Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Ndug. Gerald Mweli, alikua mgeni rasmi na alitoa ahadi ya kutatua changamoto zinazokikabili chama hicho, ili kuleta manufaa kwa wakulima.


Katika hotuba yake, Katibu Mkuu Mweli alieleza kuwa serikali inatambua mchango wa TFA katika kuunganisha wakulima na kutoa huduma muhimu kama vile ushauri wa kilimo na pembejeo. ambapo alikiri pia kwamba kuna changamoto ambazo wamezipeleka kwake kama vile riba kubwa kutoka kwa mabenki, ubora pembejeo, na ukosefu wa huduma za ugani. Aliahidi kushirikiana na TFA ili kutatua changamoto hizi na kuhakikisha wakulima wanapata fursa zaidi za kunufaika na huduma za chama hicho.


Mweli alisisitiza kwamba ushirikiano kati ya TFA na serikali ni muhimu ili kuimarisha uzalishaji wa wakulima na kuongeza tija katika kilimo. Aliwapongeza viongozi wa TFA kwa juhudi zao za kuboresha maisha ya wakulima na kuongeza uzalishaji kupitia kilimo cha kisasa.


Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TFA, Ndugu Waziri Barnaba, alisisitiza kuwa chama hicho kitaendelea kutoa huduma bora kwa wanachama wake ili kukuza uchumi wao kupitia kilimo. Mkurugenzi Mtendaji wa TFA, Jastin Shirima, aliongeza kuwa chama hicho kitatumia ushirikiano na serikali kuhakikisha wanachama wanapata mbolea za ruzuku kupitia matawi ya TFA yaliyo kote nchini.


Hii ni ahadi muhimu kwa wakulima wa Tanzania, na inatoa matumaini ya mafanikio zaidi kwa sekta ya kilimo mkutano huo ulihudhuriwa na Wanachama zaidi ya 500 kutoka Maeneo mbalimbali hapa nchini

Share:
Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com