METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, August 22, 2017

Dkt. Mwakyembe: MCL Endeleeni Kusimamia Maadili na Kuhabarisha Jamii

PICHA 1
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akibofya kitufe kuashiria uzinduzi rasmi wa Muonekano Mpya wa Gazeti la Michezo la Mwanaspoti Jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia tukio hilo ni baadhi ya Viongozi waandamizi wa Kampuni ya Uchapishaji Magazeti ya Mwananchi Communications Ltd (MCL).
PICHA 2
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe pamoja na baadhi ya Viongozi waandamizi wa Kampuni ya Uchapishaji Magazeti ya Mwananchi Communications Ltd (MCL) wakishangilia mara baada ya uzinduzi wa Muonekano Mpya wa Gazeti la Michezo la Mwanaspoti Jijini Dar es Salaam.
PICHA 3
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akichomoa gazeti jipya la Michezoa la Mwanaspoti ambalo lina muonekano mpya wa kisasa zaidi mara baada ya kulizindua Jijini Dar es Salaam.
PICHA 5
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Uchapishaji Magazeti ya Mwananchi Communications Ltd (MCL), Bw. Francis Nanai (kulia) wakiwaonyesha Waandishi wa habari muonekano mpya wa gazeti la michezo la Mwanaspoti mara baada ya uzinduzi Jijini Dar es Salaam.

Na Benedict Liwenga-WHUSM.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe ameipongeza Kampuni ya Uchapishaji Magazeti ya Mwananchi Communications Limited (MCL) kwa jitihada kubwa wanazozifanya katika kusimamia maadili kwa kuhabarisha na kuielimisha jamii ya Kitanzania.

Pongezi hizo amezitoa jana wakati wa Uzinduzi wa Muonekano Mpya wa gazeti pendwa la michezo la Mwanaspoti linalochapishwa na Kampuni hiyo.

Dkt. Mwakyembe amesema kuwa, mara kwa mara MCL imekuwa ikiisaidia jamii kwa kujihusisha katika masuala mbalimbali ya kijamii kama vile wakati wa tetemeko la ardhi Mkoani Kagera imeweza kutoa mchango wake mkubwa kwa jamii na daima imekuwa ikilinda maadili na weledi wa kazi ya uandishi kwa wafanyakazi wake jambo ambalo linaonyesha ushirikiano mzuri baina ya Serikali, Kampuni na jamii.

“Mimi nawapongeza na kuwashukuru sana MCL kwakuwa mstari wa mbele katika kulinda maadili katika kazi zenu, endeleeni kulinda maadili kwa kuhabarisha na kuielimisha jamii, sijaona mkivunja maadili ya kazi zenu na hakika mnajijengea sifa nzuri kwa wengine”, alisema Dkt. Mwakyembe.

Aliongeza kuwa, kwa sasa kumeibuka wimbi kubwa la Waandishi wa habari (Makanjanja) ambao hawana vyeti wala weledi wa kufanya kazi ya uandishi wa habari na hao wamekuwa kila wakati wakirusha taarifa zisizo sahihi hususani katika mitandao ya kijamii jambo ambalo Serikali haiwezi kulifumbia macho.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa MCL, Bw. Francis Nanai amesema kwamba lengo la kampuni hiyo kuja na muonekano mpya wa gazeti hilo ni kuwapa ladha mpya wasomaji wake nchini kote, na hiyo ni mara ya sita kwa gazeti hilo kubadilishwa muonekano wake tangu kuanzishwa kwake mwaka 2001.

“Sisi kama wadau wa michezo tumewasikiliza wasomaji wa gazeti letu na tukayafanyia kazi mawazo yao na ndiyo maana tukaamua kuja na muonekano mpya wa gazeti hili ambao uko kimataifa zaidi”, alisema Nanai.

Aliongeza kuwa, gazeti hilo lilianzishwa na waandishi wa tatu mwaka 2001 na lilikuwa likitoa nakala 3,000 kwa siku ambapo kwa sasa kuja kwa muonekano mpya wa gazeti hilo kutaongeza idadi ya wasomaji tofauti ilivyokuwa mwanzo na idadi ya uchapishaji imeongezeka hadi kufikia nakala 60,000 kwa siku.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com