METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, June 21, 2017

UN yasema wanajeshi 600 kutoka Congo Brazaville kuondolewa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati

media
Wanajeshi wa Umoja wa Mataifa wanaolinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati

Umoja wa Mataifa umesema zaidi ya wanajeshi 600 kutoka nchini Congo Brazaville wanaohudumu katika jeshi lake la kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati MINUSCA, watarejeshwa nyumbani.

Katibu Mkuu wa Umoja huo Antonio Guteress anatarajiwa kutangaza hatua hiyo baadaye hivi leo baada ya wanajeshi hao kubainika kuhusika katika visa vya unyanyasaji wa kingono na makosa mengine ya kinidhamu.

Kabla ya hatua hii Kamanda wa MINUSCA Luteni Jenerali Balla Keita alikuwa ameionya serikali ya Brazaville kuwarudisha nyumbani wanajeshi wake la sivyo, umoja wa Mataifa utachukua hatua.

Mwaka uliopita, wanajeshi wengine 120 kutoka Congo Brazaville walirudishwa nyumbani kwa makosa hayo ya unyanyasaji wa kingono hasa kwa watoto.

Congo Brazaville imetuma wanajeshi 629 kusaidiana na wengine katika kulinda amani nchini humo na kituo chao kimekuwa ni Berberati, mji wa tatu kwa ukubwa nchini humo.

Umoja wa Mataifa umetuma kikosi cha wanajeshi 12, 000 kulinda amani nchini humo.
Share:

Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2025 WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com