METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, February 16, 2024

MBUNGE NYONGO AIGEIKUIA SERIKALI KUNUNUA PAMBA SOKO LINAPOPOROMOKA


SERIKALI ipo katika hatua za awali za uanzishwaji wa Mfuko wa Kinga ya bei ya Pamba utakaotumika kumfidia mkulima wakati bei inaposhuka kwa kiasi kitakachokubalika kwa mujibu wa sheria ya kuanzishwa kwake.

Hayo yamesemwa bungeni leo na Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde wakati akijibu swali la Mbunge wa Maswa Mashariki, Stanslaus Nyongo (CCM).

Katika swali lake, Mbunge huyo ametaka kujua ni lini Serikali itaanza kununua Pamba toka kwa wakulima pindi bei ya Pamba inapoporomoka katika soko la Dunia.

Akijibu swali hilo, Silinde amesema biashara ya pamba nchini hufanyika kwa kuzingatia hali halisi ya soko ilivyo.

Amebainisha kuwa Serikali imekuwa na jukumu la kuhakikisha kuwa bei inayotolewa kwa wakulima inaakisi uhalisi wa bei katika soko la dunia kwa wakati huo.

“Kutokana na kutokuwiana kati ya uzalishaji na mahitaji ya pamba duniani, bei ya pamba hupanda na kushuka kulingana na hali ya wakati huo. “

Mathalani, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita bei ya pamba kwa ratili katika soko la dunia mwaka 2020 ilifikia Senti 50 za Dola ya Marekani na mwaka 2021, bei ilipanda hadi kufikia Dola 1.5 kwa ratili.

“Mwaka 2023 hadi mwanzoni mwa 2024 bei ilikuwa wastani wa Senti 84.”amesema Silinde.

“Kwa kutambua athari ya mabadiliko ya bei kwa wakulima wa pamba nchini, Serikali ipo katika hatua za awali za uanzishaji wa Mfuko wa Kinga ya Bei utakaotumika kumfidia mkulima wakati bei inaposhuka kwa kiasi kitakachokubalika kwa mujibu wa Sheria ya kuanzishwa kwake,”amesisitiza.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com