METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, March 4, 2023

OSHA KUONGEZA IDADI YA MAENEO YA KAZI YALIYOSAJILIWA KUTOKA 4,336 HADI 11,956

Na Saida Issa,Dodoma

SERIKALI kupitia Wakala wa Usalama na Afya mahala Pa kazi (OSHA),imesema kutokana na kuimarika kwa shughuli za usimamizi wa usalama na afya mahali pa Kazi, umefanikiwa kuongeza idadi ya maeneo ya kazi yaliyosajiliwa kutoka 4,336 hadi 11,953 ongezeko hilo ni sawa asimilia 276 na  idadi ya kaguzi zilizofanyika zimeongezeka kutoka kaguzi 104,203 hadi kufikia Kaguzi 322,241 sawa na asilimia 132.


Hayo yameelezwa na Mtendaji Mkuu wa OSHA  Khadija Mwenda , wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali na utekelezaji wa majukumu ya Wakala hiyo ,mbele ya waandishi wa habari leo Machi 4,2023,Jijini Dodoma.


"Katika kipindi hiki cha miaka miwili kumekuwa na umarishaji mkubwa sana wa shughuli za usimamizi wa usalama na afya mahali pa Kazi ndio maana usajili wa maeneo ya kazi umeongezeka kwa asilimia 276 ambapo kuna ongezeko kutoka 4,336 hadi 11,953  na hata idadi ya kaguzi tulizoganya nazo zimeongezeka kutoka 104,203 hadi 322,241 sawa na asilimia 132 ni mafanikio makubwa haya,"amesema Mwenda


Bi.Mwenda amesema kumekuwa na ongezeko la asilimia 175 ya Wafanyakazi waliopata mafunzo ya Usalama na afya mahali pa kazi kutoka wafanyakazi 32,670 hadi kufikia Wafanyakazi 43,318. 


"Mafunzo haya yanajumuisha mafunzo ya usimamizi wa masuala ya usalama na afya mahali pa kazi na uundwaji wa kamati za Usalama na Afya (Health and Safety Managemnet System), mafunzo ya kufanya kazi za mazingira ya juu (working at height), mafunzo ya huduma ya kwanza, mafunzo ya usimamizi na udhibiti wa kemikali katika maeneo ya kazi, mafunzo ya usalama na afya katika sekta ya mafuta na gesi na katika sekta ya ujenzi na majenzi, mafunzo ya usalama wa mitambo,"amesema Bi.Mwenda 

 
Aidha, Bi.Mwenda ameongeza kuwa kumekuwa na ongezeko la upimaji afya za wafanyakazi kwa asilimia 320. Upimaji afya kutoka Wafanyakazi 363,820 hadi kufikia Wafanyakazi 1,112,237 waliopimwa katika kipindi hicho cha miaka miwili ,kutotokana na kupunguzwa kwa ada mbalimbali na kuboresha mifumo ya usimamizi ambayo imewezesha maeneo mengi ya kazi kukaguliwa, wafanyakazi wengi kupimwa afya na mafunzo mbalimbali kufanyika, ongezeko hili ni tafsiri kwamba hali ya usalama na afya  katika maeneo ya kazi inazidi kuimarika.


Aidha, katika kusimamia Sheria ya Usalama na Afya kwa lengo la kuzuia ajali, magonjwa na vifo vitokanavyo na kazi, maeneo ya kazi ambayo hayakuzingatia Sheria na Kanuni za Usalama na Afya yalichukuliwa hatua mbali mbali za kisheria zikiwemo kupewa hati ya maboresho (Improvement Notice) ambapo maeneo ya kazi 1,588 yalipewa hati hizo na maeneo ya kazi mengine 105 yalitozwa faini. 


Mtendaji Mkuu huyo  amebainisha kuwa ,miongoni mwa majukumu ya OSHA ni kuchunguza ajali mbali mbali zinazotokea katika sehemu za kazi kwa lengo la kubaini vyanzo vya ajali hizo ili kushauri namna bora ya kuzuia ajali kutokea tena.

"Katika kipindi cha miaka miwili, ajali zilizoripotiwa zilipungua kwa asilia 13.2 kutoka ajali 2,138 kupungua hadi kufika 1,855.  Magonjwa yanayotokana na kazi yalipungua kwa asilimia 22.1 kutoka wagonjwa 140 kufikia wagonjwa 109,"amesema Bi.Mwenda 


Katika hatua nyingine Bi.Mwenda asema kuwa katika kipindi hicho cha miaka miwili ya Utawala wa serikali ya Awamu ya Sita,OSHA wamefanikiwa Kupunguza Urasimu na kuboresha   Mifumo ya TEHEMA,ambapo mifumo ya TEHAMA kama TANEPS, GePG, GAMIS, MUSE, E-office imesimikwa na inatumika na imekuwa ni nyenzo muhimu katika kutoa huduma.


"Kwa kutumia mifumo hiyo imetusaidia kupunguza muda wa kupata Cheti cha Usajili wa sehemu za kazi kutoka siku 14 hadi siku 1 kwa kuwa usajili unafanyika kwa njia ya kielektroniki na ambapo mteja ana uwezo kuprinti cheti chake cha usajili popote alipo (Online registration),Kutoa Leseni ya Kukidhi Matakwa ya Sheria ya Usalama na Afya mahali pa kazi (Compliance License) kutoka siku 28 hadi siku 7 kwa sasa,"amesema Bi.Mwenda 


Dhima kuu ya  Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi(OSHA), ni kuelimisha na Kuhamasisha masuala ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa kuweka mifumo thabiti itakayo zuia ajali, magonjwa na vifo pamoja na uharibifu wa mali ili kupunguza gharama za uendeshaji na kukuza uchumi wa Taifa.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com