METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, December 12, 2020

TBA YAPEWA KONGOLE KUTEKELEZA MIRADI 85

Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga, akifungua mkutano wa kwanza wa mwaka 2020\2021 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) jijini Dodoma.

Baadhi ya uongozi  wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi) na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi Katibu Mkuu wa Sekta ya Ujenzi Arch. Elius Mwakalinga, katika mkutano wao wa kwanza wa mwaka 2020/2021 uliyofanyika jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Arch. Daud Kondoro,  akiteta jambo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga wakati wa mkutano wao wa kwanza wa mwaka 2020/2021 wa baraza hilo, jijini Dodoma.

Imeelezwa kuwa katika kipindi cha miaka mitano Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), umefanikiwa kutekeleza miradi mikubwa ya ujenzi wa Majengo ya Serikali 85 nchi nzima yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 142 ikiwamo miradi ya “Buni – Jenga”.

Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga, ameyasema hayo jjini Dodoma wakati akifungua mkutano wa mwaka wa 2020/2021  wa  Baraza la Wafanyakazi wa wakala huo na kusisitiza kuwa hiyo ni hatua kubwa kitaasisi lakini hatua hiyo haijawaondoa moja kwa moja kwenye changamoto za kuchelewa kwa baadhi ya miradi ya ujenzi.

Mwakalinga ameutaka uongozi wa wakala  kutazama kwa undani hatua gani walizofikia katika utekelezaji wa majukumu yao hususani namna wanavyoweza kushughulikia changamoto  katika kila eneo la kiutendaji.

“Hakikisheni mnajitathimini kwa kina bado kuna changamoto za kuzifanyia kazi na Serikali yenu inawaamini katika utoaji ushauri na usimamizi wa miradi ya ujenzi na usimamizi wa miliki za Serikali”, amesema Katibu Mkuu huyo.

Aidha, ameupongeza Wakala kwa hatua nzuri waliyofikia katika miradi mbalimbali ya ujenzi ikiwamo ujenzi wa nyumba za makazi eneo la Magomeni Kota jijini Dar es Saalam ambapo hapo awali kulikuwa na malalamiko mengi.

Mwakalinga ameitaka TBA kuendelea kujali masuala ya wafanyakazi kutoka sekta binafsi kwa kuzingatia kuajiri watu wengi kwenye miradi ya ujenzi hususani walinzi, babalishe, mamalishe, watalaamu wa ujenzi, mafundi, vibarua na wanafunzi wa taaluma zote kutoka vyuo vikuu ili kuinua kipato cha mtu mmoja mmoja na kupunguza umaskini nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala  huo, Arch. Daud Kondoro, amemueleza Mgeni rasmi kuwa katika mkutano huo wajumbe wa baraza la wafanyakazi watapewa elimu ya “haki za mtumishi mahali pa kazi na wajibu wa mtumishi kwa mwajiri” ili iweze kuwasadia kwenye utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com