METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, May 22, 2020

TUME YA MAENDELEO YA USHIRIKA YAJIPANGA KUSIMAMIA UVUNAJI WA MIWA KUKABILIANA NA UPUNGUFU WA SUKARI NCHINI


      Mrajis wa Vyama vya Ushirika Dkt. Benson Ndiege  akiongea na Viongozi wa Vyama vya Ushirika vya Wakulima wa miwa wa Bonde la Kilombero kuhusu namna bora ya kuongeza uzalishaji sukari kupitia Kiwanda cha Sukari cha Kilombero, kikao kilchofanyika katika ofisi za Kiwanda cha Kilombero hivi karibuni
Viongozi wa Vyama vya Ushirika wa miwa wa Kilombero wakiwa katika kikao na Mrajis wa Vyama vya Ushirika katika ofisi za Kiwanda cha Kilombero
Afisa Ushirika wa wilaya ya Kilombero   Bw. Jackson Mshumba akifafanua  jambo wakati wa kikao na Viongozi wa Vyama vya Ushirika wa miwa Kilombero.

Kuhama vyama vya msingi vya Ushirika mara nyingi ni moja ya changamoto zilizobainika kupunguza ufanisi wa uvunaji wa miwa wenye tija na faida zaidi kwa wakulima wa miwa. Suala hili limekuwa ni changamoto kutokana na mkulima kuishi eneo tofauti na shamba lake, hivyo kuleta ugumu wa uratibu wa rasilimali za uvunaji miwa.

Haya yalibainishwa wakati wa kikao cha majadiliano ya muenendo wa hali ya upungufu wa sukari nchini hivi sasa. Kikao kilichokuwa kati ya Mrajis wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC) Dkt. Benson Ndiege, viongozi wa Vyama vya wakulima wa miwa wa Bonde la Kilombero pamoja na uongozi wa Kiwanda cha Sukari cha Kilombero, mkoani Morogoro hivi karibuni.

Katika kikao hicho Mrajis wa Vyama vya Ushirika Dkt. Benson alipata fursa ya kujadiliana na wakulima hao changamoto mbalimbali zinazowakabili wakulima wa miwa ambazo zinasababisha uzalishaji kuwa mdogo kulinganisha na mahitaji ya soko na kuangalia kwa pamoja namna bora ya kuongeza uzalishaji wa sukari. Moja ya changamoto kubwa zilizojadiliwa ni pamoja na ufinyu wa soko la miwa kulinganisha na uwezo mkubwa wa uzalishaji miwa unaotokana na wakulima kuhamasika na kilimo cha miwa, upatikanaji wa mikopo na hali nzuri ya hewa.

Aidha, Mrajis amewaomba wakulima kuwa wavumilivu wakati Serikali inaendelea na juhudi za kuangalia uwezekano wa kuongeza kiwanda cha uzalishaji sukari, jambo ambalo linaenda kutoa suluhu ya soko kwa kiwango kikubwa kuliko hali ilivyo sasa.

“Nia ya Serikali ni kujitosheleza kwa sukari, naomba Kiwanda muendelee na juhudi za kuongeza uzalishaji wa sukari ili kuongeza kiwango cha upatikanaji wa bidhaa hiyo muhimu katika jamii,” alisema Dkt. Ndiege 

Mrajis aliwaagiza Maafisa Ushirika pamoja na Mrajis Msaidizi wa Mkoa kusimamia taratibu pale mkulima anapohitaji kuhama uanachama kutoka chama kimmoja kwenda kingine ili kuondoa changamoto za uvunaji pamoja na kumbukumbu ya taarifa za mkulima huyo katika vyama. Alishauri ni vizuri mkulima akawa na shamba katika eneo lake la makazi. Vilevile viongozi hao wameshauriwa kufanya kazi kwa uadilifu na kufanya uwekezaji wenye tija kwa wanachama.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mawasiliano Joseph Rugaimukamu amesema Kiwanda hicho mwaka huu kimeanza uzalishaji wiki mbili mapema kuliko tarehe za kawaida za uzalishaji kutokana na hali ya upungufu wa Sukari iliyopo nchini. Akiongeza kuwa kiwanda kimelazimika kufanya hivyo ili kuongeza bidhaa hiyo sokoni pamoja na kuitikia wito wa Serikali wa kusaidia upatikanaji wa sukari kwa wananchi na kwa bei nafuu. Alisema mwaka huu lengo la Kiwanda ni kuzalisha sukari Tani 127,000 akikiri kuwa bado uwezo wa kiwanda ni mdogo kulinganisha na uzalishaji wa miwa hivi sasa ingawa juhudi za makusudi kwa kushirikiana na Serikali zinaendelea katika kuhakikisha kuwa uzalishaji unaongezeka.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com