Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji,
Mhandisi Anthony Sanga (katikati) akielekeza jambo wakati wa ziara ya
kukagua athari ya mvua kwenye miundombinu ya maji Wilayani Handeni.
Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe na kulia ni
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA), Mhandisi Clement
Kivegalo.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji
Vijijini (RUWASA), Mhandisi Clement Kivegalo (wa tatu kutshoto) akieleza
jambo wakati wa ziara ya kukagua athari ya mvua kwenye miundombinu ya
maji Wilayani Handeni. Wa pili kulia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya
Maji, Mhandisi Anthony Sanga.
Athari ya mvua kwenye miundombinu ya maji Wilayani Handeni
******************************
Serikali
imewahakikishia wakazi wa Handeni, Mkoani Tanga uendelevu wa huduma ya
maji licha ya kuharibika kwa miundombinu ya maji kulikosababishwa na
mvua zinazoendelea kunyesha.
Naibu Katibu Mkuu
wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga ametoa kauli hiyo hapo juzi
wilayani hapa wakati wa ziara yake iliyolenga kukagua athari ya mvua
kwenye miundombinu ya maji sambamba na kupata ufumbuzi wa haraka
kufuatia hali ya mvua zilizonyesha kwa takribani wiki mbili mfululizo.
Mara baada ya
kujionea hali halisi, Mhandisi Sanga aliwatoa hofu wananchi wa Handeni
ambapo aliwataka kuwa watulivu na aliahidi kuwa Serikali itahakikisha
huduma ya maji inarejea haraka iwezekanavyo.
“Ninawasihi wananchi kufanya subira na kuwa watulivu na kuzingatia maelekezo ya Serikali,” alisisitiza Naibu Katibu Mkuu Sanga.
Mhandisi Sanga
alibainisha kuwa zoezi la tathmini ya athari ya mvua hizo kwenye
miundombinu ya maji wanaloendelea nalo halitochukua zaidi ya siku tatu
kama ilivyoagizwa na Waziri wa Maji, Profesa Makame Mbarawa.
“Waziri wa Maji
ametuagiza kuharakisha kukamilisha zoezi hili, nasi tutahakikisha
linafanyika kwa kasi ikiwa ni pamoja na kutazama njia mbadala ili
wananchi wapate huduma ya maji kwa haraka,” alisema Mhandisi Sanga.
Aliongeza kuwa
Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli haipo tayari kuona wananchi wake
wanataabika na kwamba hatua madhubuti na za haraka zinachukuliwa ili
kuhakikisha wananchi wanapata maji.
Awali Mkuu wa
Mkoa wa Tanga Martin Shigela akielezea kwa ujumla athari za mvua hizo
kwenye Mkoa wa Tanga, alisema kuwa zimeleta madhara kwenye miundombinu
ya barabara na madaraja na kusababisha huduma ya usafiri katika maeneo
mbalimbali kuathirika.
“Tulichokibaini
katika mvua hizi zilizonyesha ni kuwa zimeharibu mabwawa ya maji na
kusababisha maji yaliyotoka katika mabwawa hayo kuathiri miundondombinu
mbalimbali ikiwemo ya maji na barabara,” alieleza Shigela.
Kwa upande wake
Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe akielezea athari za mvua hizo
alisema ni pamoja na kuharibika kwa mabwawa 11 ya maji yanayotumiwa na
wakazi wa Handeni na maeneo jirani na kati ya hayo yapo mabwawa makubwa
matano ambayo aliyataja kuwa ni Kwenkambara, Mandera, Suwa, Msomera na
Mkomba.
Aidha, Gondwe
alipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe
Magufuli kwa namna inavyotekeleza majukumu yake kwa wakati na kwa hatua
mbalimbali za haraka zinazoendelea kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na
kurejesha mawasiliano ya miundombinu ya barabara na maji iliyoathirika.
Sambamba na hilo,
Gondwe alimpongeza Mhandisi Sanga na timu ya wataalam aliyoambatana
nayo kutoka Wizara ya Maji na taasisi zake kwa kufika Wilayani hapa
mapema ili kufanya tathmini ya uharibifu wa miundombinu ya mabwawa ya
maji ili kupata ufumbuzi.
“Kwa niaba ya
wananchi wa Wilaya ya Handeni tunatoa shukrani nyingi sana kwa
Mheshimiwa Rais kwa kutujali na kuwatuma watendaji wa Serikali kufika
hapa Handeni ili kutatua matatizo yaliyosababishwa na mvua kubwa
zilizonyesha,” alisema Gondwe.
Kwa upande wake
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA), Mhandisi Clement
Kivegalo ambaye ameambatana na Naibu Katibu Mkuu Sanga alisema kuwa
wanaendelea na tathmini ila kwa mabwawa yaliyopasuka wamebaini
yalijengwa chini ya kiwango na pia hayakuwa yakitunzwa inavyostahili na
hivyo kupelekea kuharibika wakati mvua hizo zilizonyesha.
0 comments:
Post a Comment