Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji
Tanzania (TBC), Dkt. Ayoub Rioba akizungumza jambo wakati wa kikao baina
ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison
Mwakyembe (kulia) na wadau wa sekta ya habari wakiwemo watayarishaji wa
vipindi vya televisheni vyenye maudhui ya ndani wakati wa mkutano wake
uliofanyika jana Alhamisi Julai 25, 2019 .
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (mbele) akizungumza na wadau wa sekta
ya habari wakiwemo watayarishaji wa vipindi vya televisheni vyenye
maudhui ya ndani wakati wa mkutano wake uliofanyika jana Alhamisi Julai
25, 2019.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (katikati) akibadilishana mawazo na
Kaimu Mkurugenzi wa Utangazaji wa TCRA, Mhandisi Andrew Kisaka pamoja na
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Patrick Kipangula
wakati wa mkutano baina ya Waziri na Wadau wa sekta ya habari wakiwemo
watayarishaji wa vipindi vya televisheni vyenye maudhui ya ndani
uliofanyika jana Alhamisi Julai 25, 2019.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja
na wadau mbalimbali wa sekta ya habari mara baada ya kumalizika kwa
mkutano wake baina yake na wadau hao uliofanyika jana Alhamisi Julai 25,
2019.
(NA MPIGAPICHA WETU)
……………………….
Na Mwandishi Wetu,MAELEZO
DAR ES SALAAM
WAZIRI wa Habari, Utamadani, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe amewahakikishia wadau wa sekta ya
utangazaji nchini ikiwemo waandaaji na wazalishaji wa vipindi vya
televisheni vya maudhui ya ndani kuwa Serikali itaendelea kushirikiana
nao na kuwajengea mazingira wezeshi ili kuwawezesha kutimiza wajibu wao
wa msingi katika jamii na Watanzania kwa ujumla.
Akizungumza katika kikao maalum baina
yake watayarishaji wa vipindi vya maudhui ya ndani jana Alhamisi (Julai
25, 2019) Jijini Dar es Salaam, Dkt. Mwakyembe amesema malengo ya
Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kuwa tasnia ya habari inapiga
hatua kubwa za maendeleo na kutoa mchango unaostahiki katika maendeleo
ya jamii na Taifa kwa ujumla.
Waziri Mwakyembe alisema Serikali
inatambua wajibu na umuhimu wa tasnia ya habari nchini, na hivyo
imetunga sheria na kanuni mbalimbali zinazoongoza vyombo vya habari
ikiwemo televisheni, ambapo vimewekwa utaratibu wa kurusha na kuandaa
vipindi mbalimbali kupitia miongozo inayotolewa mamlaka husika ikiwemo
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
“Tunatambua kuwa kuna baadhi ya vifungu
vya kisheria vinavyoongoza maudhui ya vituo vya utangazaji vimekuwa
changamoto, kwa kuwa Sheria hizi sio biblia au msahafu takatifu,
tunaweza kuzifanyia marekebisho kila baada ya kipindi cha miaka 3-4 ili
kuona ni namna gani inasaidia sekta ya utangazaji sambamba na kutumia
fursa mbalimbali zinazojitokeza” alisema Waziri Mwakyembe.
Aidha Waziri Mwakyembe alisema Wizara
yake ipo tayari kupokea aina yoyote ya ushauri, mapendekezo na maoni ya
wadau wa wazalishaji na waandaji wa vipindi vya Televisheni hususani
masuala yote ambayo yamekuwa yakiwaletea changamoto katika utekelezaji
wa majukumu yao ya kuhabarisha umma kupitia vipindi mbalimbali ambavyo
vimekuwa daraja la kuwaunganisha Watanzania.
Akifafanua zaidi Dkt. Mwakyembe alisema
Serikali itahakikisha kuwa waandishi wa vyombo vya habari kutoka sekta
ya umma na binafsi ikiwemo waandaaji wa vipindi vya maudhui ya ndani
wanajengewa uwezo ikiwemo kuwapatia mafunzo ya muda mfupi, ya kati na
mrefu, hatua inayolenga kuwaongezea weledi, ujuzi na maarifa na hivyo
kutimiza wajibu wao wa msingi katika jamii.
Dkt. Mwakyembe alisema katika mfumo
uliopo sasa wa kutangaza maudhui ya ndani kumekuwepo na changamoto
mbalimbali katika kanuni, sheria na taratibu ambazo zimekuwa zikileta
malalamiko kutoka kwa wadau, na hivyo Serikali itahakikisha kuwa
vipengele hivyo vinafanyiwa kazi kwa kuwa Serikali na vyombo vya habari
vyote kwa pamoja vimekusudia kujenga msingi imara wa ushirikiano baina
yao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Matukio wa
Shirika la Utangazaji Nchini (TBC) Martha Swai amesema TBC imekuwa
mstari wa pembe katika kutangaza vipindi vyake vya Televisheni katika
maudhuo ya ndani, ambapo asilimia 82 vimegusa masuala ya elimu, biashara
na kuburudisha, na asilimia 18 ikijikita katika masuala ya muziki.
Anaongeza kuwa Shirika hilo limekuwa
likiatangaza matangazo yake ya Televisheni katika chaneli kubwa tatu
ambazo ni TBC 1, TBC 2 na Tanzania Safari ambazo zote kwa pamoja
vimekuwa na mchango mkubwa katika kutangaza habari na matukio ya vipindi
mbalimbali vyenye kuakisi maudhui ya ndani.
Naye Meneja Vipindi wa Kampuni ya Tumaini
Media, Paul Mabuga amesema kwa sasa kumekuwepo na changamoto kubwa ya
ukosefu wa matangazo ya biashara katika vituo vya Televisheni kwani
wafanyabiashara wengi wamekuwa wakitumia zaidi mitandao ya kijamii ili
kuweza kufikisha ujumbe wananchi kwa njia ya kisasa na haraka zaidi.
0 comments:
Post a Comment