METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, March 17, 2019

Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini yapongeza mradi wa umeme wa Makambako-Songea


Baadhi ya mitambo ya umeme katika kituo cha kupoza umeme cha Makambako mkoani Njombe ambacho kimejengwa kupitia mradi wa umeme wa Makambako- Songea.


 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa pili kushoto) akiongoza Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kutembelea kituo cha kupoza umeme cha Makambako mkoani Njombe. Wa Pili kulia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mariamu Ditopile Mzuzuri na Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakati walipotembelea kituo cha kupoza umeme cha Makambako mkoani Njombe. Wa Pili kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mariamu Ditopile Mzuzuri.
Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga (aliyenyoosha mkono) akitoa maelezo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu kituo cha kupoza umeme cha Songea ambacho kimejengwa kupitia mradi wa umeme wa Makambako-Songea. Wa Pili kulia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mariamu Ditopile Mzuzuri
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, chini ya Mwenyekiti, Mariamu Ditopile Mzuzuri, imeipongeza Serikali kwa kutekeleza mradi wa umeme wa Makambako- Songea (kV 220) ambao umewezesha Mikoa ya Ruvuma na Njombe kupata umeme wa uhakika kutoka Gridi ya Taifa.
Kamati hiyo, imetoa pongezi hizo wilayani Songea, Mkoa wa Ruvuma, baada  ya kukagua utekelezaji wa mradi huo ambao umehusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kV 220 kutoka Makambako hadi Songea, ujenzi wa Vituo vya kupoza umeme vya Makambako, Madaba na Songea na usambazaji umeme katika Vijiji 122.
Kabla ya  kukagua kituo cha kupoza umeme cha Songea, Kamati hiyo ilikagua vituo vya Makambako na Madaba pamoja na njia ya usafirishaji umeme kutoka Makambako hadi Songea ambapo watendaji mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), walihudhuria.
Pamoja na pongezi hizo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, aliiagiza Wizara pamoja TANESCO kuhakikisha kuwa, wanapeleka umeme katika Vijiji vyote vilivyopangwa kupelekewa umeme kupitia mradi huo na kutoruka kijiji chochote ambacho kimepitiwa na mradi.
Aidha, aliiagiza Wizara ya Nishati na TANESCO kuhakikisha kuwa, inahamasiha wananchi kutumia umeme huo kwa matumizi mbalimbali ikiwemo ya viwandani kwani mikoa hiyo sasa ina umeme wa kutosha na wa uhakika na Serikali inahitaji wateja wengi zaidi ili kuongeza mapato.
Awali, katika kituo kupoza umeme cha Makambako, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani aliieleza Kamati hiyo kuwa, mradi huo umekamilika mwaka 2018 na kazi inayoendelea sasa ni usambazaji wa umeme katika Vijiji vya awali 122 ambapo Vijiji 105 tayari vimeshaunganishwa na nishati hiyo.
Dkt. Kalemani aliongeza kuwa, mradi huo umetekelezwa  na Serikali ya Tanzania kupitia TANESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida) ambapo jumla ya gharama za mradi ni shilingi bilioni 216 na jumla ya wateja wa awali 22,000 watafaidika na mradi huo.
Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, alisema kuwa, miundombinu hiyo ya usafirishaji umeme (kV 220) imejengwa kwa umbali wa kilomita 250 na jumla ya nguzo (Tower erection) 711 zimesimikwa.
Aliongeza kuwa, kufika kwa umeme wa Gridi katika mikoa hiyo, kumefanya wananchi wahamasike kutumia umeme huo na kutoa mfano kuwa, awali matumizi ya  umeme kwa Mkoa wa Ruvuma yalikuwa ni takriban megawati 9 lakini sasa yameongezeka na kufikia megawati 11 huku kazi ya kuwasambazia umeme wananchi ikiendelea.
Share:

Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2025 WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com