METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, August 11, 2021

MRADI WA UPIMAJI IKUNGI WAMKUNA NAIBU WAZIRI MABULA

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akingalia namna upimaji ardhi unavyofanyika kwa kutumia teknolojia ya kisasa katika kijiji cha Mnang’ana katika wilaya ya Ikungi mkoani Singida alipokwenda kukagua mradi wa upimaji ardhi unaotekelezwa kwa pamoja na UNWOMEN, UNFPA na Halmashauri ya Ikungi kwa ufadhili wa KOICA Agosti 11, 2021.

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akizungumza na baadhi ya wakazi wa kijiji cha Mnang’ana wilayani Ikungi mkoani Singida alipokwenda kukagua mradi wa upimaji unaotekelezwa kwa pamoja na UNWOMEN, UNFPA na halmashauri ya Ikungi kwa ufadhili wa KOICA Agosti 11, 2021.

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akingalia sehemu unapoanzia upimaji ardhi katika kijiji cha Mnang’ana wilayani Ikungi mkoani Singida alipokwenda kukagua mradi wa upimaji ardhi unaotekelezwa kwa pamoja na UNWOMEN, UNFPA na Halmashauri ya Ikungi kwa ufadhili wa KOICA Agosti 11, 2021.

Na Munir Shemweta, SINGIDA 

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ameridhishwa na kupongeza mradi wa upimaji mipaka ya vijiji na makazi katika wilaya ya Ikungi mkoani Singida unatekelezwa kwa pamoja na mashirika ya UNWOMEN, UNFPA na halmashauri ya Ikungi kwa ufadhili wa KOICA.

Mradi huo utakaowawezesha wananchi wa Ikungi kupata hatimiliki za Kimila utakamilika katika vipindi vya miaka 3 kuanzia 2020 hadi  2023 na kugharimu dola milioni 4.9 na kuwafikia  moja kwa moja wanawake na wasichana 2,350.

Akizungumza wakati wa kutembelea na kukagua mradi huo katika kijiji cha Mnag’ana Agosti 11, 2021 Dkt Mabula alisema, mradi huo una faida kubwa kwa wananchi wa ikungi kwa kuwa mbali na faida nyingine utawasaidia wananchi wanaopimiwa kujua mipaka ya maeneo na kuepuka migogoro ya ardhi.

‘’Faida ya kupimiwa ni  usalama wa miliki na uhakika wa kutambua maeneo na kuondokana na migogoro, pia kutumia ardhi yako kwa kushughuli za maendeleo kwa hiyo sasa serikali imefanya hivyo mara nyingi imekuwa ikiishia mijini na kusahau wale wa vijijini wenye maeneo makubwa  na sasa imeona itupie jicho maeneo ya vijijini kama ikungi.

Aidha, Dkt Mabula alisema kupitia mradi huo wa UNWOMEN mbali na kunufaisha vijana kupitia fedha wanazopata katika ushiriki wa zoezi lakini pia unatoa fursa ya ujuzi kwa vijana kwa kupeleka katika maeneo mengine kile kilichofanyika kjijiji cha Mang’ana halmashauri ya Ikungi.

‘’Mradi huu unatumia teknolojia na taarifa zote zinaingia kwenye mfumo hivyo hakuna mtu mwingine anaweza kuingizwa katika kiwanja kimoja hivyo takwimu ni faida ya mradi huo’ alisema Dkt Mabula.

Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Singida Shamim Hozza aliuelezea mradi huo wa upimaji kama mradi wezeshi wenye lengo la kuwafanya wananchi maeneo yanayofanyiwa upimaji kushiriki katika zoezi hilo.

“Mradi huu wa upimaji hapa Ikungi pamoja na kuwawezesha wananchi wanaopimiwa maeneo yao kuwa na hati za kimila lakini una pia lengo la kuwafanya wananchi kushiriki katika zoezi zima la upimaji na kupatiwa hati za kimila” alisema Shamim.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Ikungi Ambrose Ngonyani aliuelezea mradi huo kuwa, mbali na zoezi la upimaji mashamba na makazi kwa wananchi wa Ikungo pia unaboresha mazingira ya ofisi.

‘Mradi huu wa UNWOMEN unatumia teknoljia mpya na unafikia watu wengi zaidi na kwa hati za kimila Ikungi inakuwa halmashauri ya kwanza kujaribu mfumo huo’’. Alisema Ngonyani

Naye mkazi wa Ikungi Salum Abrahman ameshukuru uanzishwaji wa mradi huo katika kijiji cha Mang’ana  kwa kueleza kuwa umewapatia fedha sambamba na kuondoa migogorpo ya ardhi.

‘’Mradi huu mbali na kutupatia fedha kutokana na kushiriki katika zoezi lakini utasaidia sana migogoro ya ardhi ambayo inasumbua sana maana hata ushahidi unaotolewa kwenye mabaraza ya ardhi hauko sawa  kwa kuwa haina uthibitisho wa kutosha’’ alisema Abdulrahman.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com