METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, December 3, 2018

“TIMU YA UHAKIKI WA WAKULIMA WA KOROSHO YAONGEZEKA, BIL 35 ZIMESHALIPWA” MHE HASUNGA

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa CBT Mkoani Mtwara kutoa ufafanuzi juu hali ya ununuzi wa korosho Tarehe 3 Disemba 2018. (Picha Na Mathias Canal-Wizara ya Kilimo)

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Mtwara

Timu ya wataalamu wa Uhakiki wa wakulima wa Korosho imeongezeka katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma kutoka 11 mpaka kufikia timu 20 ili kuongeza uharaka wa uhakiki kwa ajili ya malipo ya wakulima.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga ameyasema hayo tarehe 3 Disemba 2018 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa CBT Mkoani Mtwara kutoa ufafanuzi juu hali ya ununuzi wa korosho.

Katika mkutano huo pia Waziri Hasunga amesema kuwa timu ya wataalamu tayari imewasili mkoani Pwani kwa ajili ya kuanza uhakiki wa wakulima wa korosho kuanzia leo tarehe 3 Disemba 2018 ambapo mkoa wa Pwani utakuwa mkoa wanne kuhakikiwa ukiungana na mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.

Alisema kuwa hadi kufikia tarehe 1 Disemba 2018 jumla ya vyama vya ushirika 212 vilikwisha hakikiwa kati ya vyama 504 vilivyopo katika mikoa hiyo mitatu ya kusini.
Aidha, Vyama 157 vimekwishalipwa fedha zao kati ya vyama 617 vinavyojihusisha na korosho nchini.

Mhe Hasunga alisema kuwa tayari Bilioni 35,540,709,854 zimekwishalipwa kwa wakulima wa korosho ambapo kilo 10,769,912 za korosho zimekwishalipiwa.

Mhe Hasunga ameviambia vyombo vya habari kuwa idadi ya wakulima ambao wameshalipwa mpaka tarehe mosi Disemba ni wakulima 34,938

Amefafanua zaidi kwa kusema kuwa katika mkoa wa Lindi tayari Bilioni 12.7 zimelipwa ilihali katika Mkoa wa Ruvuma ni Bilioni 4.9 na Mkoa wa Mtwara ni Bilioni 17.9

MWISHO
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com