METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, October 26, 2018

WAZIRI LUKUVI ASULUHISHA MGOGORO WA ARDHI BAINA YA WATAWA NA WANANCHI WA KIJIJI CHA MLONGONI SIHA



Na Munir Shemweta, WANMM Kilimanjaro
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amesuluhisha mgogoro uliodumu zaidi ya miaka thelathini ambao ulileta uhasama na chuki baina ya Shirika la Watawa  wa Kikatoliki na wananchi wa kijiji cha Mlongoni katika Wilaya ya Siha mkoa wa Kilimanjaro kuhusiana na shamba la Kirari.
Katika shamba hilo wananchi wa kijiji cha Mlongoni wanaishi katika eneo lenye ukubwa wa ekari 347 na Watawa kubakia na ekari 1063 ambapo kwa mara ya kwanza Hati ya shamba hilo ilitolewa tarehe 26 Oktoba, 1950 kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kilimo.
Lukuvi alifikia suluhu na pande hizo mbili baada ya kukutana na Watawa wa Katoliki na baadaye viongozi wa kijiji cha Mlongoni kwa lengo la kutafuta suluhu baada ya Mahakama ya Rufaa Tanzania kuwapatia ushindi Watawa na hivyo kulazimu wananchi wa kijiji hicho wanaofikia 3,700 kutakiwa kuondoka katika shamba la Kirari.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi aliamua kuenda eneo hilo la kijiji cha Mlongoni jana wakati akiwa katika ziara yake ya kutembelea wilaya za Hai, Moshi na Same mkoa wa Kilimanjaro kwa ajili ya kushughulikia migogoro ya ardhi katika wilaya hizo.
Katika kikao chake na Watawa wa Katoliki, Lukuvi aliwaeleza kuwa Shirika lao ni wamiliki halali wa shamba hilo kama ilivyoamuliwa na Mahakama ya Rufaa na Serikali haiwezi kupingana na maamuzi ya Mahakama na kusisitiza anachotaka yeye ni kuangalia namna bora ya kutekeleza hukumu ya Mahakama.
Aliwaeleza Watawa kuwa, pamoja na wao kupatiwa ushindi katika kesi hiyo kuna haja ya wao  kuangalia namna bora ya utekelezaji wa hukumu hiyo bila kuathiri wananchi wanaoishi eneo hilo ambao wengi wameishi kwa muda mrefu wengine wakiwa wameuziwa maeneo bila ya kufahamu.
“Ninyi ni wamiliki halali wa eneo hilo kama ilivyoamuliwa na Mahakama ya Rufaa lakini ili kuweza kufanya kazi kwa amani kwenyea eneo hilo ni lazima kutafuta namna bora ya kutekeleza uamuzi wa mahakama, ni lazima kuwe na win win situation” alisema Lukuvi
Haikuwa kazi rahisi kuweza kuwashawishi Watawa kukubaliana na ombi la Lukuvi lakini baada ya kutumia takriban saa mbili kuwaelewesha namna alivyoweza kushughulika na migogoro ya aina hiyo zaidi ya 120 katika maeneo tofauti ya nchi, Watawa walikubali kumuachia kushughulikia utekelezaji bora wa hukumu ya mahakama .
Uamuzi huo wa Watawa ulimfanya Lukuvi kuenda eneo la tukio wilayani Siha na kukutana na uongozi wa kijiji cha Mlongoni na baadaye wananchi wote wa kijiji hicho.
Katika mazungumzo yake na wananchi wa kijiji hicho, Lukuvi aliwaeleza kuwa kufuatia hukumu ya Mahakama ya Rufaa, wananchi hao hawana haki ya kuwepo eneo hilo na Serikali haiwezi kuingilia uamuzi huo na katika kutekeleza maamuzi ya Mahakama wananchi wanatakiwa kuondoka kwenye shamba hilo ikiwemo kuvunjiwa nyumba zao.
Hata hivyo, Lukuvi aliwaeleza wananchi hao kuwa, Serikali ya awamu ya tano ni Serikali inayowajali wanyonge hivyo haitakuwa busara kuwaondoa wananchi wanaokadiriwa kufikia 3,700 hasa ikizingatiwa baadhi yao walijenga nyumba kwa kuweka fedha kidogo kidogo.
Katika kutekeleza namna bora ya hukumu ya Mahakama, Lukuvi aliwaeleza wana kijiji kuwa ili suala hilo liishe kwa usalama na amani ni vyema wakakubaliana na utaratibu utakaopangwa na Serikali na hatua ya kwanza ni kufanya tathmini katika eneo hilo kwa lengo la kujua idadi halisi ya wakazi pamoja na mali zao ili kuepuka wajanja wachache wanaoweza kujipenyeza kwa nia ya kujinufaisha na kumuagiza Mkuu wa Wilaya ya Siha na timu yake kuanza kazi hiyo mara moja.
Aidha, katika kushughulikia suala hilo Lukuvi alisitisha uendelezaji wowote katika eneo hilo hadi hapo utaratibu mzuri utakapofanywa na kufafanua kuwa uendelezaji wowote utakaofanyika unaweza kuleta athari kwa wana kijiji ambao kwa sasa hawana haki na eneo hilo.
Mwenyekiti wa kijiji cha Mlongoni Manase Herman alimshukuru Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa jitihada zake za kutafuta suluhu katika mgogoro huo uliodumu kwa zaidi ya miaka thelathini na kubainisha kuwa wao kama viongozi wa kijiji cha Mlangoni wanakubaliana na utaratibu utakaotumiwa na Lukuvi katika kutafuta suluhu ya jambo hilo huku mwananchi mwingine John Ngwandi akitaka serikali kuangalia namna ya kuwasaidia hasa ikizingatiwa kizazi cha awali kilishatoweka na wengi waliobaki ni wa kuanzia miaka ya sitini.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com