Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela Tuzo ya Udhamini Mkuu wa maonyesho ya Viwanda mkoani Pwani. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ametoa rai kwa Watanzania kupenda vya kwao kwa kujenga Utamaduni wa kutumia bidhaa zinazozalishwa nyumbani.
Makamu wa Rais ameyasema hayo leo wakati wa Hafla ya Ufunguzi wa Wiki ya Viwanda mkoani Pwani.
“Natoa wito kwa jamiikujenga utamaduni wa kutumia bidhaa zilizozalishwa kwenye viwanda vyetu ndani ili viweze kuendelea kwa kuwa tusipofanya hivyo viwanda vinavyojengwa havitaedelea na nchi yetu kubaki masikini pamoja na wananchi wake” alisema Makamu wa Rais.
Makamu wa Rais ambaye amekuwa kwenye ziara ya kukagua na kuhamasisha shughuli za kimaendeleo mkoani Pwani amefahamishwa kuwa mkoa huo una viwanda takribani 429 vikiwemo vikubwa vya kati na vidogo.
Kauli Mbiu ya Maonyesho hayo ni “Viwanda Vyetu, Uchumi wetu Pwani Tumeweza Tunatekeleza na Tunakuza Uchumi wa Viwanda”.
Makamu wa Rais alitoa pongezi kwa mkoa kubuni onyesho hilo na kulitaka liwe endelevu na pia alipongeza Wizara ya Nishati, Dawasa pamoja na Shirika la Reli kwa kuwa na mkakati maalum wa kuwafikishia huduma hizo wenye viwanda.
Makamu wa Rais pia aliwapa angalizo wazalishaji wa bidhaa zinazofanana kutochafuana kibiashara badala yake waache bidhaa zao zishindane zenyewe sokoni.
Aidha, Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amempongeza Makamu wa Rais kwa kufanya ziara ya siku sita mkoani humo na kuwafungulia maonyesho ya Viwanda na kuahidi mkoa wake utaendelea kuwa pokea wawekezaji wa viwanda na kuhakikisha wanafanikisha taratibu zao kwa haraka zaidi.
Hitimisho ; Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano amemaliza ziara yake ya kukagua na kuhamasisha shughuli za maendeleo mkoani Pwani na kuwataka viongozi hao kufanya kazi kwa kushirikiana na kuelewana katika kuleta ufanisi kwenye kazi.
0 comments:
Post a Comment