METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, February 22, 2018

DKT MABULA ASHANGAZWA NA UTATA WA UMILIKI WA HATI ZA ARDHI




Na Mwandishi Maalum- Mara

Naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi mhe. Angelina Mabula ameshangazwa na uwepo wa majalada ya ardhi katika halmashauri za Butiama na Musoma ambayo wamiliki wake hawafahamiki na majalada hayo kujulikana kama ‘’ndugu mhusika’’.

Akiwa katika ziara yake ya siku tatu ya kushughulikia migogoro ya ardhi pamoja na kukagua mfumo wa ulipaji kodi ya ardhi mkoani Mara mhe. Mabula alisema  majalada hayo yamekuwa na matatizo ya viwango vya kulipa kodi kwa kuwa yanaonekana kuwa deni huku mmiliki akitaka kumilikishwa upya kwa gharama ndogo.

Kufuatia mkanganyiko huo, naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi  aliyakabidhi majalada yenye utata kwa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) kwa uchunguzi zaidi ili kubaini kama suala hilo limefanyika kimakosa ama ni kwa makusudi.

‘’Mtu anamilikishwa leo kwa pesa ndogo sana halafu za huko nyuma zinapotea hapa kuna mchezo unafanyika kupunguza mapato ya serikali’’ alisema Mabula.

Aidha, naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi ametaka majalada ya ardhi kuingizwa katika mfumo kwa kila robo ya mwaka ili iwe rahisi kufuatilia waliolipa kodi ya ardhi na wale wasiolipa.

Kwa mujibu wa Mabula tatizo baadhi ya watumishi hawana nia thabiti ya kutumia mfumo wa kukusanya maduhuli ya serikali ndiyo maana utekelezaji wa maagizo yanayotolewa unashindwa kufanikiwa.

Awali mkuu wa wilaya ya Musoma Dk. Vicent Anney Naano alimueleza naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi kuwa wilaya yake ina changamoto kubwa ya watumishi wa ardhi, ukosefu wa ramani za vijiji, kutoendelezwa kwa baadhi ya viwanja na wananchi wengi  kutokuwa na fedha kwa ajili ya kupimiwa maeneo yao.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi
22 Februari, 2018
Share:

Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2025 WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com