METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, November 1, 2016

Serikali kukipandisha kituo cha afya cha Laela kuwa hospitali ya Wilaya

jafo
Naibu waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mhe. Suleimani Jafo akijibu swali la Mbunge wa Kwela Mhe. Ignas Malocha (hayupo pichani) aliyehitaji kujua ni lini kituo hicho cha afya kitapewa hadhi ya kuwa Hospitali ya Wilaya,

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kukarabati kituo cha afya cha Laela kilichopo mkoani Rukwa ili kikidhi vigezo vya kuwa Hospitali ya Wilaya ikiwa ni moja ya jitihada za kupunguza adha ya wananchi kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya zilipo.

Hayo yamesemwa jana mjini Dodoma na Naibu waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mhe. Suleimani Jafo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kwela Mhe. Ignas Malocha aliyehitaji kujua ni lini kituo hicho cha afya kitapewa hadhi ya kuwa Hospitali ya Wilaya.

Mhe. Jafo amesema kuwa ni uamuzi wa muda mrefu wa Serikali kuiweka Hospitali hiyo kuwa ya Wilaya na ndiyo sababu ya kufanya jitihada za kukiongezea uwezo kituo hicho kwa kujenga wodi nyingi pamoja na kutoa kibali cha kuajiri watumishi wapya kwani kwa sasa kituo hicho kina upungufu wa watumishi .

Amefafanua kuwa hadi sasa kuna baadhi ya majengo ambayo tayari yameshakamilika ambayo ni jengo la upasuaji wa dharura, wodi ya wagonjwa waliofanyiwa upasuaji pamoja na wodi ya mama wajawazito.

“Kwa sasa kituo cha afya cha Laela hakina miundombinu inayokidhi sifa za kuwa Hospitali ya Wilaya ila kutokana na kupanuka kwa Mji huo na kuongezeka kwa watu wanaohitaji huduma katika kituo hicho tumeamua kukiboresha ili kifikie hadhi ya kuwa Hospitali ya Wilaya”, amesema Jafo.
Ameongeza kuwa kwa sasa huduma za rufaa kwa wagonjwa wanaohudumiwa katika kituo hicho zinatolewa kupitia magari ya kawaida ya Halmashauri kutokana na ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa lakini Wizara ina matarajio ya kutenga fedha ya kununulia gari hilo katika Bajeti ya mwaka 2017/2018.

Aidha, Mhe. Jafo amethibitisha kuwa kituo hicho kimetengewa jumla ya shilingi 9,358,100 katika Bajeti ya fedha ya mwaka huu ambayo itagharamia kununua dawa na vifaa tiba vitakavyorahisisha upatikanaji wa matibabu kwa wananchi wa eneo hilo.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt Hamisi Kigwangalla amesema kuwa Wizara hiyo inaendelea kuipitia mikataba ya makampuni binafsi ili kuangalia namna ya kushirikiana nao katika kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba katika Hospitali na vituo vya afya nchini.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com