Waziri wa Fedha na Mipango,Dk. Mwigulu Nchemba, akiwa amebeba kikapu chenye fedha wakati alipokuwa akiongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa shule mbili za sekondari zitakazomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kati katika changizo lililofanyika Kanisa la Emmauel Msalaba Mrefu Mjini Singida leo Juni 4, 2023. Wa pili kushoto ni Katibu Mkuu wa Kanisa hilo, Robert Kitundu.
Na Dotto Mwaibale,
Singida
WAZIRI wa Fedha na Mipango,Dk,Mwigulu Nchemba, ameongoza
harambee ya kuchangia ujenzi wa shule mbili za sekondari zitakazomilikiwa na
Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kati ambapo jumla
ya Sh. 443,063,800 zilipatikana na lengo lilikuwa ni kukusanya Sh.Milioni 500.
Katika fedha hizo zilizopatikana, taslimu zilikuwa ni Sh. 400,103,
800 na ahadi ikiwa ni Sh. 42,960,000. Dk.Mwigulu wakati wa harambee hiyo aliambatana
na Mbunge wa Singida Mjini, Mussa Sima,Mbunge wa Singida Mashariki, Miraji
Mtaturu,Mbunge wa Makete, Festo Sanga, Mbunge wa Handeni Mjini, Reuben Kwagilwa na Mbunge wa Nsimbo, Anna Lupembe na viongozi mbalimbali wa kanisa hilo
akiwamo Baba Askofu Dk.Alex Malasusa na Katibu Mkuu wa kanisa hilo, Robert Kitundu.
Akizungumza katika harambee hiyo iliyofanyika Kanisa la KKKT Usharika wa Emmanuel
Msalaba Mrefu Mjini Singida, Dk.Nchemba ambaye pia ni Mbunge wa Iramba
Magharibi alisema Serikali inatambua mchango mkubwa unaofanywa na taasisi za
dini hasa katika eneo la sekta ya elimu na afya kwani shule nyingi kongwe hapa
nchini zilikuwa zimeanzishwa na taasisi hizo likiwamo kanisa la KKKT.
“Kanisa la KKKT hapa nchini ni taasisi iliyochangia sana
katika maendeleo ya Mtanzania na lipo katika historia ya nchi yetu na haitafutika
kwani ukiondoa hizi shule za sekondari zilizopewa jina katika kila kata kabla
ya hapo shule zote zilizokuwa zikitumika kwa kiwango kikubwa zilikuwa ni za
kanisa,” alisema Dk. Mwigulu.
Dk.Mwigulu alisema hata katika sekta ya afya hospitali nyingi
zilizokuwa zikitoa huduma zilikuwa ni za kanisa na kwamba lengo la harambee
hiyo lipo kwenye malengo yaleyale ya kuhudumia jamii.
Aidha, Mwigulu alisema moja ya muundo ambao anapenda
kuhusisitiza katika utekelezaji wa shughuli za miradi ya maendeleo baina ya
Serikali na sekta binafsi ni ile iliyofanywa na kanisa na kuwa viongozi wengi bila
ya kujali dini zao wamepitia kwenye mikono ya kanisa na kusoma katika shule za taasisi
hiyo.
Askofu wa kanisa hilo Dayosisi ya Kati, Dk.Syprian Hilinti
akizungumza kwenye harambee hiyo alisema Halmashauri Kuu ya kanisa hilo imeweka
mpango mkakati wa miaka mitano ya kujenga shule mbili za Sekondari Kiomboi na
Kititimo kuanzia mwaka 2022/ 2027 kama mradi wa kitega uchumi cha kanisa.
“Miradi hii hailengi kuuwa historia za Missioni au biblia
Kiomboi balikupanua kuendana na hali halisi
na mahitaji ya wakati bila kuacha au kupoteza kusudi la injili bali
kulitoa kwa ubora wa kukidhi changamoto za sasa.
Alisema kuwa hawawezi kuendesha gari la kisasa kwa kutumia
gia za mwaka 1926 na kuwa halmashauri hiyo imeweka mipango ya muda mrefu
kujenga kitega uchumi maeneo ya nyuma ya ofisi Kuu ya Dayosisi hiyo mara baada
ya kumaliza mpango wa ujenzi wa shule.
Aliongeza kuwa sambamba na mpango huo Dayosisi imeweka sera
ya kuendelea kuimarisha ukarabati, maongozi, usimamizi na utendaji kwenye
vituo, miradi na taasisi zake zilizopo tayari.
Alisema katika awamu ya kwanza zilikuwa zikihitajika
Sh.Milioni 500 na ndio lengo la kufanya harambee hiyo.
Katika hatua nyingine Dk. Hilinti alimuomba Dk.Mwigulu
kuwasilisha ombi la kanisa hilo kwa Rais Samia Suluhu Hassan la kutaka
warejeshewe Shule ya Sekondari ya Luluma iliyopo wilayani Iramba Kiomboi.
Askofu wa kanisa hilo Dayosisi ya Kati, Dk.Syprian Hilinti, akiendesha harambee hiyo.
0 comments:
Post a Comment