METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, July 29, 2022

WAKUFUNZI WA MAKARANI WA SENSA NA WASIMAMIZI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUTANGULIZA UZALENDO

Mwenyekiti wa Kamati ya Sensa Wilaya ya Kongwa, Mhe. Mkuu wa Wilaya Remidius Mwema




Na Maganga Gwensaga  Kongwa, Dodoma

Mwenyekiti  wa kamati ya sensa wilaya ya kongwa Mkoani Dodoma  ambaye pia ni Mkuu  wa wilaya hiyo Mhe. Remidius Mwema, amewataka wakufunzi wa sensa wilayani  humo kufahamu kwamba serikali  imewaamini kusimamia zoezi kubwa lililo mbele  la kuwafundisha makarani, wasimamizi wa maudhui na wasimamizi wa  Tehama  akiwataka kufanya kazi wakitaguliza uzalendo mbele.

Mhe. Mwema amesema hayo Julai 28, 2022 wakati akizungumza na timu ya wakufunzi  hao  zikiwa ni siku chache kabla ya kuanza kwa mafunzo kwa makarani, wasimamizi wa maudhui na wasimamizi wa  Tehama  yanayotarajia kuanza tarehe 31 Julai mpaka tarehe 19 Agosti mafunzo yatakayoendeshwa na wakufunzi hao.

Muamini kwamba mmeaminiwa na wilaya ya kongwa tunajivunia uwepo wenu tukiamini kwamba zoezi litaenda vizuri, tunaamini mtaenda kuwa mstari wa mbele na mkumbuke yale yote mliyojifunza  na yatakuwa na tija endapo tu mtayafanyia kazi.” Alisema Mhe. Mwema

Amewataka wakufunzi hao kutambua kwamba wamebeba dhamana kubwa ya nchi  na kwamba tukio hili ni zoezi la kitaifa  kila mmoja ana wajibu wa kulinda na kuhakikisha kwamba jambo hili analikamilisha kikamilifu.

Tuna matarajio makubwa kwenu na tusingependa litokee doa lolote na Kwa kuwa mnaenda kuwafundisha wengine hakikisheni mnazingatia msingi ya ualimu muende kusimamia miongozo nasi kama kamati ya  wilaya tutashirikiana bega kwa bega  kuhakikisha tunafanikisha zoezi hili.” Aliongeza Mhe. Mwema

Kwa upande wao wakufunzi hao wamesema wamejiandaa na kujipanga vizuri na wako tayari kuanza kazi na wamemhakikishia Mwenyekiti kwamba kwa mafunzo waliyoyapata na mbinu walizopewa  na walimu wao kila kitu kitaenda sawa.

Mafunzo kwa makarani wa sensa, wasimamizi wa maudhui na wasimamizi wa Tehama wapatao 205,000 yatafanyika katika ngazi ya Wilaya kuanzia tarehe 31 Julai hadi tarehe 18 Agosti.

Aidha washiriki wengine wa mafunzo katika ngazi za Wilaya ambao watashiriki katika siku mbili za Mwanzo, yaani tarehe 31 Julai, 2022 na tarehe 1 Agosti, 2022 ni watendaji wa kata wote nchini kwa Tanzania Bara  na Masheha wote wa Tanzania Zanzibar.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com