METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, November 20, 2021

WILAYA YA NYAMAGANA YAZINDUA TAMASHA LA MAWASILIANO, UTALII, UTAMADUNI PAMOJA NA MAONYESHO YA BIASHARA


Kuelekea miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika na 59 ya Jamhuri, Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza imezindua tamasha la mawasiliano, utalii, utamaduni pamoja na maonyesho ya biashara litakalovikutanisha vikundi mbalimbali vya Sanaa, utamaduni , ngoma asilia na vikundi vya wafanyabiashara .

Akizungmza na waandishi wa habari Novemba 19, 2021 Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mhe, Amina Makilagi alisema anawashukuru sana waandaaji wa maonyesho ya tamasha hilo kuichagua Nyamagana kuwa sehemu ya maonyesho hayo.   

“ Maonyesho haya ya kibiashara, utalii na  mawasiliano katika nchi yetu, tunataka kwenda kuonyesha jamii namna tulivyopiga hatua katika Nyanja mbalimbali kama unavyojua  Jiji la Mwanza ndo kitovu cha kila kitu na tunatengeneza uchumi wa buluu kupitia uvuvi.” Alisema Mhe, Makilagi

Alisema Mwanza ni kiungo kikubwa cha mawasiliano kwa Mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani hivyo kupitia maonyesho hayo ni fursa kubwa na kipekee kwa Mkoa wa Mwanza kuyatumia na kujiletea maendeleo kwani kutokea Mwanza unaweza kupeleka bidhaa zako Kenya, Uganda na hata Burundi.

“ Mwanza ni kitovu cha mawasiliano, Mwanza ni lango la kuingia na kuunganisha mikoa ya Kanda ya Kanda ya ziwa na kitovu cha biashara katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa maonyesho yamekuja hapa tunaenda kuitangazia jamii kwamba wapi tulipotoka katika kupigania uhuru .” Aliongeza  Mhe, Makilagi

Aidha kupitia maonyesho hayo kutakuwa na banda maalumu ambalo litakuwa likionyesha na kuelezea harakati zilizokuwa zikifanywa na hayati Baba wa Taifa katika kupigania uhuru ili Watanzania waweze kujifunza. 

Naye Mratibu wa Tamasha hilo Buche Buche Enos amesema Lengo la Tamasha hilo kuhamasisha utalii Mkoani Mwanza nani  fursa ya pekee kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo ili jamii ivitambue na kuanza kuvitembelea kwa lengo la kujifunza masuala mbalimbali yahusuyo utalii.

Alisema katika tamasha hilo la siku 10 ambalo limeanza tarehe 19 - 29 Novemba litapambwa na michezo na mashindano mbalimbali yakiwemo mashindano ya mitumbwi yakihusisha mitumbwi 15 ya wanawake itakayobeba wanawake 3 na  mitumbwi 25 ya wanaume itakayobeba wanaume 3 kila mmoja kufikisha idadi ya wanaume 75 .

Kwa upande wake Afisa utamaduni Mkoa wa Mwanza Bi Agnes Majinge alisema ndani ya siku 10 hizo watakusanya wajasiliamali, wafanyabiashara lakini pia watahamasisha utalii wa kitamaduni kwa vile Mwanza kuna vivutio vingi vya utalii.

“Jiji la Mwanza lina fursa nyingi za kibiashara, tutakuwa na mashindano ya ndoma, kwaya, kazi za mikono mfano usukaji wa mikeka lakini pia tutakuwa na taasisi mbalimbali za kibiashara na watoa huduma kama ngoma nk.” Alisema Bi Agnes

Alisema katika maonyesho yanayoendelea katika uwanja wa Malamala uliopo Igoma wameandaa maeneo kulingamna na aina ya bidhaa mfano kuna maeneo ya wafanyabiashara wa kazi za utamaduni, kazi za mikono, kuchora, kuchonga,  biashara ndogondogo na wajasiliamali.

Akizungmzia mashindano ya Mitumbwi Bi Majinge alisema zawadi mbalimbali zitatolewa kwa washindi kuanzia mashindano ya ngoma za asili , mitumbwi, kwaya na muziki wa kizazi kipya.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com