METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, November 20, 2021

TWCC YAVUNA WANACHAMA WAPYA 70 WILAYANI MISUNGWI


Mkuu wa wilaya ya Misungwi Veronica Kessy, akiangalia baadhi ya bidhaa za wanawake


Mwenyekiti wa TWCC Mkoani Mwanza Fausta Ntara

Bakari Ally Songwe Meneja wa SIDO Mkoani Mwanza

Viongozi wa TWCC, wanawake wajasiliamali wakiwa  katika picha ya pamoja na Mgeni Rasmi Bi Veronica Kessy.

Chama cha wafanyabiashara wanawake Mkoa wa Mwanza(TWCC) kimeendelea kupanua wigo wake kwa Kufungua matawi mkoani humo na kuvuna wananchama 70 wilayani Misungwi.

Katika hafla ya uzinduzi wa tawi hilo iliyofanyika wilayani Misungwi Mkoani Mwanza, Mkuu wa wilaya ya Misungwi Veronica Kessy, aliwataka wanawake Wilayani humo kuitumia TWCC kukamilisha ndoto zao za kibiashara.

“ Natambua Misungwi wako wanawake wengi sana wanaojishughulisha na biasahara kubwa, za kati na ndogo lakini pia kuna wajasiliamali wadogo wadogo hivyo uwepo wa TWCC utawasaidia sana kuleta mabadiliko katika biashara zenu.” Alisema Bi Kessy

Aidha aliwashauri wanawake wafanyabiashara wilayani humo kujiunga na TWCC kwani kwa muda mrefu wamekuwa wakitoa fursa za mafunzo kwa wanawake wafanyabiashara lakini pia kupitia maonyesho mbalimbali wamekuwa wakiwakutanisha wanawake na kujifunza kutoka kwa wanawake wenzao.

“ TWCC wamekuwa na mtandao mkubwa na taasisi nyingine ambazo zinajihusisha moja kwa moja na wafanyabiashara mfano taasisi za kifedha , SIDO na taasisi zingine ambazo zinatoa elimu kwa wafanyabiashara namna ya kuboresha na kukuza biashara zao.” Aliongeza Bi Kessy

Katika Risala yao waliomba Mkuu huyo awe mlezi wao jambo ambalo alilikubali na kuahidi kuwapa ushirikiano katika kila jambo linalohusu wanawake Wilayani humo.

Akizungumza na wazo huru Blog Mwenyekiti wa TWCC Mkoani Mwanza Bi Fausta Ntara alisema lengo la kufungua tawi hilo wilayani humo, ni kuhakikisha fursa mbalimbali za wanawake zinawafikia hata ambao wapo vijijini.

Alisema mara nyingi fursa uwa zinafikia maeneo ya Mijini tu hivyo baada ya kutambua kwamba hata maeneo ya nje ya Miji kuna wajasiliamali wakaona waanze kupeleka huduma na huko, Tawi la Misungwi likiwa ni tawi lao la pili kufunguliwa katika Mkoa wa Mwanza.

“TWCC ni kampuni ya wanawake wote na makampuni mengi yanapokuja hufikia mjini na TWCC ni ya wanawake wote wajasiliamali na wafanyabiashara sasa tukaona ni vyema tupeleke huduma hii kwa wanawake waliopo nje ya Mji.” Alisema Bi Fausta

“ Wajasiliamali wengi wapo nje ya Mji waliopo mjini ni wachache sana na wapo kwa sababu wengi wapo kwasababu waume wao wapo Mjini na wengine ni waajiliwa lakini wengi wapo huku nje ya Mji.” Aliongeza Bi Fausta

Akizungumzia fursa mbalimbali zinazopatikana TWCC alisema ni mafunzo wanayoyatoa kupitia taasisi wanazoshirikiana nazo, lakini pia huwakutanisha wanawake wafanyabiashara kupitia maonyesho mbalimbali wanayoandaa hivyo wanawake hujifunza kutoka kwa wanawake wenzao.

Kabla ya uzinduzi huo wanawake hao walipewa elimu na mafunzo kutoka taasisi mbalimbali za kifedha na taasisi za kimafunzo ya kibiashara ambazo zilihalikwa kutoa mada katika hafla hiyo

Bakari Ally Songwe Meneja wa SIDO Mkoani Mwanza aliyekuwa mmoja wa wawezeshaji katika hafla hiyo alisema ni miaka kadhaa sasa SIDO imekuwa ikitoa elimu na fursa kwa wafanyabiashara na wajasiliamali.

Alisema SIDO ina jukumu la kusimamia na kuendeleza biashara na viwanda vidogo na inafanya kazi kubwa nne moja ikiwemo utoaji wa mafunzo mfano ujasiliamali, mafunzo ya hati miliki, utengenezaji wa mashine mbalimbali na utoaji wa mikopo kwa wafanyabiashara pamoja kuhakikisha bidhaa za wafanyabiashara zinafika sokoni.

Mmoja wa wajasiliamali waliofika katika hafla hiyo Bi Fortunata Nkwande mkazi wa Misungwi kata ya Ukiriguru mtengezenaji wa sabuni, batiki, karanga za mayai na unga wa lishe ameupongeza sana uoingozi wa TWCC kufungua tawi wilayani humo akiamini wataleta tija kubwa sana wilayani humo.

“ Niwapongeze sana TWCC kutuona wanawake wa Misungwi na tulikuwa tunapitwa sana na fursa mfano tuna changamoto  kuhusu barcode, vifungashio naamini kupitia viongozi wetu tutapata elimu na mafunzo ya namna bora za kufungasha na hivyo kuongeza tija kwenye biashara zetu.” Alisema Bi Fortunata

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com