METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, December 19, 2020

RC KUNENGE APIGA MARUFUKU UTARATIBU WA MADALALI KUPEWA VIZIMBA KWENYE MASOKO, ASEMA MADALALI HAO NI CHANZO CHA KUPANDA KWA BEI YA KODI YA PANGO NA KUUMIZA WAFANYABIASHARA

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Aboubakar Kunenge amepiga marufuku tabia ya baadhi ya masoko kupangisha vizimba kwa madalali Kisha madalali hao kuwapangishia wananchi kwa Bei ya juu Jambo linalowaumiza wafanyabiashara wakati lengo la Serikali kujenga masoko hayo ilikuwa ni kuwasaidia wafanyabiashara na sio kuwakandamiza.

RC Kunenge ametoa onyo hilo wakati wa ziara Jijini humo ambapo pia amewaelekeza Wakurugenzi wa Manispaa zote za jiji hilo kukaa pamoja na kufanya mapitio ya Bei elekezi za kupanga kwenye masoko ili kusiwe na kupishana kwa gharama za Bei ya upangaji.

Aidha RC Kunenge amesema masoko yanayojengwa yakikamilika na wafanyabiashara wakapangiwa sehemu za kuuza Bidhaa zao ni marufuku kwa mfanyabiashara kufanya Biashara nje ya masoko au sehemu zisizo rasmi.

Akiwa kwenye Mradi wa Soko la Tandale amemtaka mkandarasi kukamilisha Mradi ifikapo mwezi wa nne mwakani Kutokana na umuhimu mkubwa wa Soko hilo huku akimtaka Mkandarasi wa kampuni ya MECCO inayojenga soko la Kibada kwa gharama za shilingi bilioni 6.6 nae kuhakikisha anakamilisha kabla ya mwezi wa tano mwakani ili wananchi waweze kunufaika na Manispaa ipate Mapato.

Hata hivyo RC Kunenge ametembelea Mradi wa Ujenzi wa Barabara tano zenye urefu wa Km 10.5 za Muungano chini ya DMDP RC ambapo amekasirishwa na kusuasua kwa ukamilishaji wa Mradi huo huku wahusika wakitoa kisingizio Cha Corona na Mvua na kumuelekeza mkandarasi kutoka Kampuni ya CRJE kufanya kazi usiku na Mchana na kukabidhi Mradi mwishoni mwa mwezi January pasipo kisingizio chochote.

RC Kunenge pia ametembelea Barabara ya Mikadi Beach - Sheraton yenye urefu wa Mita 800 inayotekelezwa na mkandarasi kutoka Osaka Ltd na ujenzi wa Daraja la Malimbika linalounganisha Kata ya Somangila na Kisarawe 11 chini ya mkandarasi wa kampuni ya Lumo Cons Ltd amapo amewataka wakandarasi hao kukamilisha miradi kwa wakati.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com