METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, October 26, 2020

WAZEE ILEMELA: OKTOBA 28 TUNA JAMBO LETU

Wazee wa wilaya ya Ilemela wamesema kuwa Siku ya Jumatano ya Oktoba 28, 2020 watakuwa na Jambo lao la kuhakikisha wanafanya maamuzi sahihi kwa kuwapigia Kura nyingi za NDIO wagombea  wa nafasi ya Uraisi, Ubunge na Udiwani kutoka Chama Cha Mapinduzi Kama shukran kwa Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Mhe Dkt John Magufuli kwa namna walivyotatua kero na changamoto za muda mrefu zilizokuwa zikiwakabili katika kipindi kilichopita.

Akizungumza kwa niaba ya wazee hao, Mwenyekiti mstaafu wa CCM wilaya ya Ilemela Selemani Kamesa katika kikao kilichowakutanisha wazee wa kutoka kata zote 19 za manispaa ya Ilemela kilichofanyika katika ukumbi wa Monarchy akasema kuwa wazee wa Ilemela wanashabaha moja tu ya kuhakikisha wanachagua wagombea kutoka CCM kwa kuwa ndio watu sahihi wenye uwezo wa kusimamia maslahi yao pamoja na kumpa tano ya kongole Rais Mhe Dkt John Magufuli na Mbunge wa Jimbo la Ilemela Dkt Angeline Mabula kwa jitihada zao shirikishi zilizosaidia kutatua kero za upatikanaji wa huduma bure za uhakika za afya kwa wazee sanjari na uwepo wa mpango wa bima ya gharama nafuu 

'.. Wazee wa Ilemela tunajambo letu tarehe 28 Oktoba, Tukampigie Kura Rais wa CCM, Mbunge wa CCM na Diwani wa CCM kwani bila hawa haya mambo mazuri tunayoyazungumza hapa tusingeyapata ..' Alisema

Akimkaribisha Mgombea wa nafasi ya Ubunge Jimbo la Ilemela kupitia CCM, Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wilaya ya Ilemela Ndugu Mohamed Yusuph mbali kueleza namna Serikali ilivyochukua jitihada mbalimbali zenye lengo la kulinda maslahi ya wazee akaongeza kuwa kwa kipindi Cha miaka mitano ya uongozi wa awamu ya tano matukio ya mauaji ya wazee na vikongwe yamepungua kwa kiasi kikubwa hivyo wana kila sababu kuhakikisha wanaunga mkono Serikali ya Mhe Dkt John Magufuli kwani ndio Serikali pekee yenye kuweka Kinga kwa Wazee

Nae Mzee Jonas Nyango kutoka kata ya Bugogwa akapongeza uboreshaji wa huduma za wazee huku akitolea mfano wa namna yeye alivyosaidiwa kupata huduma nzuri ya kiafya bila gharama katika Kituo Cha Afya Karume Cha wilaya ya Ilemela

Akihitimisha Mgombea wa nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Ilemela kupitia CCM Mhe Dkt Angeline Mabula akawahakikishia ushirikiano wazee hao huku akiwashukuru kwa mchango wao katika kuhakikisha Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wazee ikiwa ni pamoja na kuendelea na mradi wa mpango wa kunusuru kaya masikini TASAF kwa awamu ya tatu na kubeba Ilani yenye kumaliza kiu na matamanio ya wazee kwa kuweka kipengele Cha makundi maalum ndani yake chenye lengo la kutetea maslahi ya wazee hao.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com