METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, October 18, 2020

WANANCHI WA KIGAMBONI KUPATA UMEME WA UHAKIKA

Waziri wa Nishati,Dkt Medard Kalemani(mwenye miwani),Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi. Innocent Luoga, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania(Tanesco) Dkt Tito Mwinuka pamoja na wataalamu mbalimbali, wakikagua maeneo mbalimbali ya  ujenzi  wa  mradi wa kituo cha kupooza Umeme kilichopo Dege, Wilaya ya Kigamboni, jijini Dar es Salaamu.Oktoba 17,2020.

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani amesema kuanzia tarehe 1 Desemba mwaka huu, wananchi wanaoishi katika wilaya ya kigamboni wataanza kupata umeme wa uhakika kwakuwa ujenzi wa kituo cha kupooza umeme kilichopo dege kinatarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.

Ameyasema hayo, Oktoba 17,2020 wakati akizungumza na waandishi wa Habari, mara baada ya kumaliza kukagua kituo cha kuupoza umeme kilichopo Dege, wilaya ya Kigamboni,Jijini Dar es Saalam.

Amesema, lengo la kutembelea kituo hicho mara kwa mara ni kwasababu ya kuweka mkazo na msukumo ili kituo hicho kikamilike kwa haraka na wananchi wa kigamboni waanze kupata umeme wa uhakika katika maeneo yao.

Ameeleza kuwa, kwasasa wananchi wa kigamboni wapatao zaidi ya 48,000 wanaotumia umeme wanategemea umeme kutoka Ilala na Kurasini, na Serikali imeamua kujenga  kituo hicho ili kuhakikisha kuwa wananchi wa kigamboni nao wanapata umeme wa uhakika na wakujitosheleza.

“Nitoe taarifa kwa wananchi wa kigamboni kwamba hali ya ujenzi wa kituo hiki inaendelea vizuri na ujenzi wake umefikia asiliamia 81 hadi sasa na nimeridhishwa na utaalamu unaofanyika hapa na hatua iliyofikiwa”alisema Dkt Kalemani.

Aidha, amesema kuwa mkandarasi wa mradi huo atakamilisha kazi zake zote ndani ya mwezi mmoja uliobaki baadala ya miezi miwili aliyokuwa amejipangia mkandarasi huyo, kwakuwa kazi zilizobaki ni zile ndogo ndogo ambazo mkandarasi huyo anaweza kuzikamilisha ndani ya mwezi mmoja.

Amefafanua kuwa, kituo hicho ujenzi wake utakapokamilika kitazalisha  megawati 48 ambazo ni mpya na zikijumlishwa na megawati 12 za hapo awali jumla zitakuwa megawati 60 ambapo mahitaji ya wananchi wa kigamboni kwasasa ni megawati 18 na kueleza kuwa  kutakuwa na ziada ya takribani megawati 42 katika wilaya hiyo.

Dkt.Kalemani amesema, mradi huo utakapokamilia pia utawanufaisha wananchi wa Ilala na Kurasini kwakuwa wanatakuwa na umeme wa kutosha kwasababau hawatagawana tena umeme na  wananchi wa Kigamboni.

Pia, amesema Serikali imejenga vituo vingi vya kupooza umeme kwa nchi nzima, ambapo takribani vituo vikubwa 134 vimejengwa nchi nzima, na vituo 7 vidogo, na kwa maana hiyo    jumla ya vituo 141 vimejengwa katika nchi nzima.

Vilevile, amewatoa wasiwasi wananchi wote wa kigamboni ambao  mpaka sasa hawajapata umeme kuwa watapelekewa huduma hiyo na tayari wakandarasi wameshapatikana kwaajili ya kazi hiyo.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi huo Mhandisi Neema Mushi amesema kazi zinaendelea vizuri katika ujenzi wa  kituo hicho na wakandarasi wote wapo katika eneo la  mradi huo unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.

Pia, ameeleza kuwa vifaa vyote vinavyohitajika katika mradi huo vipo tayari kwenye eneo hilo, na waatalamu wengi wanaojenga katika ujenzi huo ni waatalamu wa kutoka katika Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO).

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com