METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, May 7, 2020

DKT MABULA: SHUKRANI AZANIA BENKI KWA KUUNGA MKONO SHUGHULI ZA MAENDELEO

Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula ameishukuru benki ya Azania kwa kumuunga mkono katika ujenzi wa nyumba vya madarasa kwa kutoa mifuko 100 ya saruji kati ya mifuko 500 iliyoahidiwa na benki hiyo.


Akizungumza kwa niaba ya Mbunge huyo, Katibu wa ofisi ya mbunge wa Jimbo la Ilemela Bwana Kazungu Idebe amesema kuwa jimbo la Ilemela lina upungufu wa nyumba vya madarasa baada ya ongezeko la wanafunzi kutokana na sera ya Serikali ya Rais Mhe Dkt John Magufuli ya elimu bure, Hivyo msaada huo wa saruji uliotolewa na benki ya Azania utaenda kupunguza changamoto hiyo katika utoaji wa elimu ndani ya jimbo hilo

'.. Nachukua fursa hii kuishukuru benki ya Azania kwa msaada huu ambao kwetu sisi ni mkubwa sana utaenda kutatua kero ya upungufu wa vyumba vya madarasa kwa watoto wetu ..' Alisema

Katibu huyo pia akawataka wadau wengine kuunga mkono juhudi za mbunge wa jimbo la Ilemela na Serikali katika kuboresha sekta ya elimu ili kuwa na kizazi bora kilicho elimika.

Aidha meneja wa benki ya Azania tawi la mwaloni Bwana Sasa Milingwa akasema kuwa mchango walioutoa umetokana na ombi lililowasilishwa na Mbunge wa Ilemela Dkt Angeline Mabula kwa benki hiyo na menejimenti yake kuridhia kumchangia mifuko 500, Awamu ya kwanza wakiwasilisha mifuko 100 na baadae kumalizia iliyobaki ili kuunga mkono juhudi za utekelezaji wa miradi ya maendeleo unaofanywa na Serikali kwa ushirikiano na viongozi wake.

Wakati Katibu tawala wa wilaya ya Ilemela Mhe Said Kitinga akaipongeza benki hiyo kwa kuunga mkono Serikali pamoja na kuwakumbusha wananchi kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Covid-19 unaosumbua dunia kwa sasa, Huku mkurugenzi wa wilaya ya Ilemela John Wanga akimpongeza Mbunge Dkt Mabula kwa juhudi zake za kutafuta wadau wanaounga mkono utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo ndani ya manispaa yake sanjari na kuahidi  kusimamia saruji hiyo na kuhakikisha inatumika katika malengo yaliyokusudiwa.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com