METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, March 18, 2020

MAJALIWA, SERIKALI IMEFUNGA VYUO VYA KATI, VIKUU KUJIKINGA NA CORONA


Waziri Mkuu amesema kwa sasa wanafunzi wengi wa vyuo wamefunga, hivyo amewataka wasirudi vyuoni hadi watakapotaarifiwa na walioko vyuoni wametakiwa warejee majumbani kwao ili kuondoa msongamano kwenye maeneo hayo.

“Vyuo vya ualimu wanafunzi wake walitakiwa kufanya mitihani mwezi Mei, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia atafanya taratibu za kurekebisha  ratiba ya mitihani kulingana na matokeo ya hali ya maambukizi.”

Waziri Mkuu amewasisitiza wananchi waendelee na shughuli zao kwa umakini na wasiwe na taharuki kwani Serikali inaendelea kulifanyia tathmini suala hilo na kwamba itakuwa inatoa taarifa kadiri inavyohitajika.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema huduma katika  maduka, masoko na za usafiri ziendelee kutolewa kama kawaida ila kwa umakini mkubwa na kwenye vyombo vya usafiri wa umma wahusika wahakikishe hawajazi sana abiria.

Jana, Machi 17, 20202 Serikali ilitanga kuzifunga shule zote za awali, msingi na sekondari  kwa muda wa siku 30 na kwamba wanafuzi wa kidato cha sita waliopaswa kuanza mitihani Mei 4, 2020 nao watapaswa kusibiri Wizara ifanye utaratibu mwingine kulingana na matokeo ya hali ya maambukizi.

Waziri Mkuu alisema mikusanyiko yote mikubwa ya ndani na nje isiyo ya lazima imesitishwa kuanzia sasa ikiwemo shughuli za michezo, matamasha ya muziki, mikutano mbalimbali ikiwemo ya shughuli za kisiasa, mahafali na shughuli nyingine za kijamii. 

Alizitaka wizara na taasisi zizitishe semina, warsha, makongamano na mikutano yote hapa nchini ambayo inahusisha washiriki toka nchi zenye maambukizi makubwa. “Watanzania wenye safari zisizo za lazima kwenye nchi zenye maambukizi makubwa, wanashauriwa wasitishe safari hizo,” alisisitiza.

Akielezea hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali ili kudhibiti ugonjwa huo, Waziri Mkuu alisema: “Serikali imesitisha michezo yote inayokusanya makundi ya watu ikiwemo Ligi Kuu ya Tanzania Bara (VPL), Ligi Daraja la Kwanza (FDL), Ligi Daraja la Pili (SDL) na aina nyngine. Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo iziandikie taasisi zake.”

Pia aliwataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wahakikishe maeneo yote yaliyobainishwa na kutengwa (vituo vya huduma na ufuatiliaji) kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa endapo watajitokeza katika maeneo yao yanakuwa na mahitaji yote muhimu na yanahudumiwa ipasavyo.

Alisema Watanzania hawana budi kuzingatia ushauri unaotolewa na Serikali na kupuuza taarifa za uzushi zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii. “Watanzania tuache mzaha wa kutumia mitandao ya kijamii kufanya upotoshaji wa tahadhari katika jambo hili,” alionya.

Kuhusu viongozi wa dini, Waziri Mkuu aliwaomba waendelee kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha waumini wao wote kuzingatia tahadhari za ugonjwa huu. Pia amevitaka vyombo vyote vya habari vishirikiane na Serikali katika utoaji wa elimu kwa umma kuhusu kujikinga na Corona bila kufanya upotoshaji wala kuipa jamii hofu.

Aliwataka wananchi watoe taarifa kuhusu uwepo wa mgonjwa au kupata ufafanuzi kuhusu ugonjwa huu kupitia namba za bure za 0800110124, 0800110125 na 0800110037.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com