METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, November 19, 2019

MBINU ZA WIZARA YA MAJI ZIMEKUJA NA UTATUZI WA HUDUMA YA MAJI MIJI MIKUU YA MIKOA


Na Ismail Ngayonga,MAELEZO
DAR ES SALAAM
Maji ni hitaji muhimu sana katika ukuaji wa uchumi  na hii inatokana na ukweli kuwa maendeleo ya kiuchumi ya nchi yoyote duniani  yawe ya viwanda, kilimo na kadhalika yanategemea maji.

Aidha Maji ni hitaji muhimu sana katika uhai wa mwanadamu na viumbe wengine na ndio maana maji hayana  mbadala na pia bila maji hakuna uhai na hivyo serikali inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maji ili kuimarisha uendeshaji na utoaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Huduma za maji mijini hutolewa kupitia Mamlaka za Maji na Usafi wa Mazingira kwenye Miji Mikuu ya Mikoa 23 pamoja na Dar es Salaam; Miji Mikuu ya Wilaya 99, Miji Midogo 14; na miradi 8 ya maji ya Kitaifa ili kufikia malengo yaliyopo ya kuboresha huduma hiyo katika Miji Mikuu ya Mikoa kutoka asilimia 86 hadi kufikia asilimia 95 mwaka 2020


Taarifa ya Serikali kupitia Wizara ya Maji inaonesha kuwa mwaka 2016, Uzalishaji wa majisafi maeneo ya mijini umeongezeka kutoka lita milioni 385 kwa siku mwezi Aprili 2015 hadi kufikia lita milioni 470 kwa siku mwezi Machi, 2016 sambamba na ongezeko la idadi ya wateja waliounganishiwa huduma ya maji kuongezeka kutoka kutoka 362,953 mwezi Aprili, 2015, hadi wateja 405,095 mwezi Machi, 2016 ambapo wateja 392,942 sawa na asilimia 97 wamefungiwa dira za maji.


Aidha makusanyo ya maduhuli kwa mwezi yatokanayo na yatokanayo na mauzo ya maji yameongezeka kutoka Tsh. Bilioni 7.28 mwezi Aprili, 2015 hadi kufikia Tsh. Bilioni 8.50 mwezi Machi 2016 sawa na ongezeko la asilimia 17.


Katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza katika sekta ya maji nchini, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais Dkt. John Magufuli, imeendelea kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Miji Mikuu ya Mikoa ili kufikia asilimia 95; na Miji Mikuu ya Wilaya, Miji Midogo na Miradi ya Kitaifa kufikia asilimia 90 ifikapo mwaka 2020.


Akiwasilisha Hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2019/2020, Waziri wa Maji, Prof. Makame Mbarawa anasema katika mwaka 2018/2019, Serikali imeendelea kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji mijini kwa kujenga, kukarabati na kupanua miundombinu ya majisafi na majitaka pamoja na kuzijengea uwezo Mamlaka za Maji Mijini.


Akbainisha baadhi ya Miradi inayotekelezwa na Serikali katika Miji Mikuu ya Mikoa, Waziri Mbarawa anasema katika Manispaa ya Kigoma Serikali kwa kushirikiana na  na Serikali ya Ujerumani na Umoja wa Ulaya inatekeleza mradi wa usambazaji wa huduma ya majisafi na usafi wa mazingira kwa gharama ya Euro milioni 16.32, ambapo hata hivyo mwaka 2018 Serikali imesitisha mkataba na mkandarasi wa mradi huo kutokana na uwezo mdogo wa mkandarasi.


‘’Hadi kuvunjwa kwa mkataba, utekelezaji wa mradi ulikuwa umefikia asilimia 87 na mradi ulikuwa umeanza kutoa huduma ya maji kwa wananchi, kutokana na hali hiyo, Wizara imechukua jitihada za kuhakikisha huduma iliyokuwa ikitolewa kwa wakazi wa Mji wa Kigoma inarejeshwa kwa kuajiri mkandarasi wa kuweka mitambo ya muda ya kusukuma maji’’ anasema Waziri Mbarawa.


Kuhusu Jiji la Arusha,, Waziri Mbarawa anasema Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) inatekeleza mradi wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji majisafi na uboreshaji wa huduma ya uondoaji wa majitaka katika Jiji la Arusha kwa gharama ya Dola za Marekani Milioni 233.9.


Anaongeza kuwa Kazi zinazotekelezwa ni pamoja na uchimbaji wa visima virefu 56, ujenzi wa matanki 10; ujenzi wa mtambo wa kutibu na kusafisha maji, upanuzi na ukarabati wa mtandao wa mabomba ya majisafi, upanuzi na ukarabati wa mtandao wa majitaka, ujenzi wa mabwawa mapya 18 ya majitaka, ujenzi wa ofisi ya Mamlaka; ununuzi wa vitendea kazi na kutoa mafunzo mbalimbali kwa watumishi.


Akifafanua zaidi Waziri Mbarawa anasema hadi mwezi Aprili 2019, utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 30 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2020, ambapo kukamilika kwa mradi huo kutaongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 40 kwa siku za sasa hadi kufikia lita milioni 200 kwa siku na muda wa upatikanaji wa huduma ya majisafi utaongezeka kutoka wastani wa saa 12 za sasa kwa siku hadi saa 24.


Waziri Mbarawa anasema katika Manispaa ya Lindi, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani na Umoja wa Ulaya inatekeleza mradi wa majisafi na usafi wa mazingira katika Manispaa ya Lindi unaogharimu Euro milioni 11.7 ambao ulitarajiwa kukamilika mwaka 2017 lakini haukukamilika kutokana na uwezo mdogo wa kiutendaji wa mkandarasi.


Anasema kuwa Serikali ilichukua hatua ya kuvunja Mkataba na Mkandarasi huyo mwezi Oktoba 2018 ambapo utekelezaji wa mradi ulikuwa umefikia asilimia 92.3 na unatoa huduma ya maji kwa wakazi wapatao 81,343 wa Mji wa Lindi, ambapo kazi zilizobaki ni kufunga mfumo angalizi wa uzalishaji maji, ununuzi wa gari la uondoaji majitaka na kurekebisha maeneo yenye mapungufu katika mradi huo.


Aidha Waziri Mbarawa anasema katika mpango wa muda mfupi wa kuboresha huduma ya maji katika Mji wa Njombe, Serikali imekamilisha ujenzi wa mradi wa maji wa chemchemi ya Kibena uliogharimu Tsh. bilioni 1.1, ukihusisha  ujenzi wa kidakio cha maji, ulazaji wa bomba kuu lenye urefu wa kilomita 2.2 na ufungaji wa pampu mbili za kusukuma maji zenye uwezo wa kuzalisha lita 72,000 kwa saa.


Kukamilika kwa mradi huo kumeongeza uzalishaji wa maji kutoka lita 480,000 hadi lita 864,000 kwa siku na kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji katika Hospitali ya Kibena, Chuo cha Uuguzi, na Ofisi za Makao Makuu ya Mkoa na hivyo kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji katika Mji wa Njombe kutoka asilimia 69 mwaka 2016 hadi asilimia 87 za sasa.


Ili kufanikisha malengo yaliyopo, ni wajibu wa Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira katika miji mikuu ya Mikoa kuimarisha hali ya Uzalishaji wa majisafi pamoja na kupunguza kiwango cha upotevu wa maji pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma iliyo bora na endelevu kwa wananchi.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com