METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, November 25, 2019

KAMPENI YA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA

 

***********************************

Tanzania inaungana na ulimwengu mzima kuadhimisha Kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia nchini. Chimbuko la maadhimisho haya limetokana na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Awamu ya 7, Mhe. Koffi Annan alipotoa Tamko mwaka 2006, la kutaka Dunia itambue kuwa lipo tatizo kubwa la ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto wa kike, hivyo ikapendekezwa kuna haja ya kuwa na kipindi maalum cha Kampeni ya kupinga ukatili wa kijinsia, na kukubaliwa iwe inafanyika kuanzia tarehe 25 Novemba hadi tarehe 10 Desemba kila mwaka.

Kwa mwaka huu maadhimisho ya Kampeni hii yatafanyika kitaifa Jijini Dodoma katika Uwanja wa Jamhuri kuanzia tarehe 25 Novemba, 2019 na kilele chake kuwa tarehe 10 Disemba, 2019 na yatazinduliwa tarehe 26 Novemba, 2019 na Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Mb). Maadhimisho haya  yamelenga kuongeza ushawishi, kubadilishana taarifa na uzoefu, kujenga uwezo wa pamoja, matumizi mazuri ya rasilimali zinazopatikana na kuunganisha nguvu za pamoja katika kuhamasisha, kuelimisha, kukemea na kuchukua hatua kwa pamoja ili kupinga ukatili wa kijinsia katika jamii, kwa kuzingatia mazingira na matukio yanayoenda sambamba na kauli mbiu husika.
Kauli Mbiu ya Maadhimisho ya mwaka huu ni “Kizazi Chenye Usawa: Simama Dhidi ya Ubakaji”. Kauli mbiu hii inatupa jukumu sisi sote kutafakari wajibu wetu kama kizazi kinachoamini na kuthamini usawa wa kijinsia. Kauli mbiu hii inatupa msukumo wa kuhakikisha kuwa kila mtu katika nafasi yake anapaza sauti na kuchukua hatua ya kuzuia na kutokomeza vitendo vya ukatli wa kingono hasa ubakaji na matendo yote ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika nyumba tunazoishi, mahali pa kazi, shuleni na mahali pengine katika jamii zetu. 





Katika kupambana na tatizo la ukatili wa  kijinsia,Wizara inawaomba watanzania na wadau kuunganisha nguvu na kubuni mikakati  ya kijamii ambayo italeta suluhisho la kudumu. Katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu matokeo mazuri yameanza kupatikana kwa kuwashirikisha wananchi wenyewe  na hasa kuwahusisha viongozi wa kijamii kama vile viongozi wa dini, viongozi wa kimila, wazee maarufu na watu wengine ambao wana sauti katika jamii husika.  

Tunatoa wito kwa wadau wote  na wanachi kushiriki na kutumia kampeni hii  kupata elimu na uelewa kuhusu namna ya kuzuia na kutokomeza ukatili wa kijinsia na kuwa na sauti ya pamoja katika kukabiliana na vitendo hivyo.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com