kulia ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akiwa Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Atashasta Nditiye
kulia ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo katikati ni Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Atashasta Nditiye na kulia ni Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Wizara ya Madini Issa Nchasi wakijadiri jambo
Jengo la kituo cha umahiri lililopo Mkoani Simiyu.
*************************
Na Tito Mselem, Simiyu
Naibu Waziri wa Wadini Stanslaus Nyongo akiwa ameambatana na Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Atashasta Nditiye amekabidhiwa jengo la kituo cha umahiri Mkoani Simiyu.
Mpaka sasa majengo matatu ya Wizara ya Madini yamekabidhiwa baada ya kukamilika kwa asilimia 100 ambayo yamegharimu zaidi ya shilingi bilioni 4.4 ambapo Wizara kupitia mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) ilitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vitua vya umahiri saba nchi nzima kikiwemo kituo cha Simiyu kilicho gharimu shilingi Bilioni 1.308.
Imeelezwa kuwa kampuni ya SUMA JKT iliingia mkataba na Wizara ya Madini ili kukamilisha Ujenzi wa Vituo vyote saba nchi nzima ambapo Kituo cha Simiyu Ujenzi wake ulianza tarehe 5 septemba, 2018 na kukamilika Septemba, 2019.
Akizungumza kwenye makabidhiano hayo Naibu Waziri wa Madini Nyongo alisema Lengo la vituo hivi pamoja na mambo mengine ni kutoa mafunzo ya kitaalam yahusuyo Madini, mafunzo haya yatahusu Utafiti wa Madini, ikiwa ni pamoja na kuonesha mikanda ya Madini ilipo na muelekeo wake, Uchimbaji wa Madini wenye tija na salama, Uchenjuaji wenye kuleta uvunaji mkubwa wa madini na hivyo kuwapatia faida kubwa wachimbaji, pia katika majengo haya kutakuwa na mafunzo ya kuomba leseni kwa njia ya mtandao na kutakuwa na usagaji wa mawe na kupima sampuli za madini mbalimbali.
“Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) ulifanya utafiti wa kijiolojia na kubaini maeneo saba muhimu ambayo vituo vya umahiri vitajengwa pakiwemo Simiyu,” Nyongo alisema.
Baada ya Naibu Waziri kukabidhiwa jengo hilo nae alilikabidhi kwa Tume ya Madini na kuwataka Ofisi ya Madini Simiyu kulitumia vizuri jengo hilo ili lilete manufaa yaliyokusudiwa ikiwa ni pamoja na kuwapatia wachimbaji wadogo mafunzo ya namna bora ya kuendesha shughuli zao ili wafanye shughuli zao kwa ufanisi na hatimae kuongeza makusanyo ya Serikali.
Wakati huo huo, Naibu Waziri ametoa wito kwa wachimbaji wa madini na wananchi kwa ujumla wakitumie kituo hicho cha Simiyu ili kujifunza na kupata taarifa kuhusiana na shughuli za utafiti na uchimbaji madini kwa kuwa kituo hiki kimejengwa kwa ajili ya wananchi na kwa kodi za wananchi.
Kwa upande upande wake mkuu wa Mkoa wa Simiyu Antony Mtaka aliipongeza Wizara ya Madini kwa ujenzi wa kituo hicho muhimu kitakacho wasaidia wachimbaji wengi wa madini katika Mkoa wa Simiyu.
Aidha wake kaimu meneja wa mradi wa usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) Veronica Francis alisema kuwa mradi huo umegawanywa katika sehemu kuu tatu ambazo ni kuongeza unufaikaji kutokana na sekta ya Madini kwa Nchi, kukuza uwazi na uwajibikaji katika Sekta ya Madini na Mafunzo na Usimamizi wa Mradi.
“Mradi ulijikita katika kutekeleza kazi mbalimbali zikiwemo ujenzi wa vituo saba vya umahiri, ujenzi wa vituo vya mfano, ukarabati wa ofisi za madini, ununuzi wa vifaa vya ofisi za madini, ununuzi wa samani za ofisi, utafiti wa kijiolojia katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uchimbaji mdogo, na kuongeza ushirikiano na serikali za mitaa zinazofanya shuguli za madini,” Veronica alisema.
“Tumeamua kujenga kituo cha umahiri Simiyu kwa kuwa utafiti wa kijiolojia umebaini kuwepo na mashapo ya kutosha katika maeneo ya Nyaranja Meatu na kuwepo na madini ujenzi, pia Mkoa kuna taarifa za awali za kijiolojia zikionesha utafiti mkubwa wa Madini ya Nickel kule Dutwa na Ngasamo,” Veronica aliongeza.
Vilevile, Wizara kupitia Mradi imejenga jengo la taaluma katika Chuo cha Madini (MRI) kwa ajili ya matumizi ya ofisi, madarasa, kumbi za mikutano na ofisi za ushirika wa wachimbaji madini wanawake Tanzania kwa ajili ya kuendeshea shuguli zao.
Kazi za ujenzi kwa baadhi ya majengo zimekamilika na mengine yapo katika hatua za ukamilishaji na Mkandarasi anatarajia kukabidhi Majengo hayo hivi karibuni kwa jumla ya gharama ya Sh.7.897 kwa majengo yote saba.