METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, June 19, 2019

Jafo Aonya Halmashauri Ambazo Hazijashiriki Mafunzo ya Kuandaa Maandiko ya Miradi ya Kimkakati

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo akifungua semina ya kuandaa maandiko ya miradi ya kimkakati
Washiriki  wakimskiliza Waziri Jafo wakati wa ufunguzi semina ya kuandaa maandiko ya miradi ya kimkakati
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Serikali za Mitaa Angelista Kihaga atoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa semina ya kuandaa maandiko ya miradi ya kimakati
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa semina hiyo.

…………………

Nteghenjwa Hosseah,OR-TAMISEMI

WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), Selemani Jafo ameionya mikoa ya Dodoma,Lindi na Njombe iliyoshindwa kupeleka watendaji wake kuhuduhuria semina ya kuandika miradi ya kimkakati.

Onyo hilo juzi jijini hapa wakati akifungua semina ya siku mbili iliyoshirikisha mamlaka za serikali za mitaa zilizopo Tanzania Bara na sekretarieti za mikoa semina iliyofanyika katika Chuo cha serikali za mitaa Hombolo.

Jafo alisema semina hiyo ni muhimu sana kwao kwa ajili ya kuwajengea uwezo utakaowawezesha kuibua miradi mbalimbali lakini ameshangaa mikoa hiyo kutopeleka watendaji wake.

“Hapa hatuna wawakilishi wa mkoa wa Dodoma,Njombe na Lindi wakati Dodoma mradi mkakati walioupata ni Kondoa peke yake,hakuna Bahi,Chamwino wala Jiji,Njombe nao hakuna mradi mkakati walioupata cha kushangaza kwenye semina hii hawapo,”alisema.

Alieleza Lindi wana mradi mkakati katika halmashauri ya Liwale na Ruangwa lakini bado hawajahudhuria semina hiyo na Mtwara halmashauri wana mradi katika halmashauri moja lakini Nanyumbu,Masasi,Newala,Tandahimba na Nanyamba hakuna mradi wowote walioupata lakini pia hawajahudhuria.

“Hii Nanyamba ni halmashauri ya mwisho katika ukusanyaji wa mapato nawaagiza  wahakikishe awamu ya pili ya semina hiyo wanakuwepo,”alisema.

Jafo alisema mpaka sasa kiasi cha Sh.Bilioni 268.37 zimeshatolewa na serikali kwa ajili ya kugharamia miradi 38 na hapo kuna halmashauri hazijaguswa na miradi hiyo kutokana na maandiko yao kutokuwa na sifa za kuweza kupata fedha na hali yao ya uchumi bado ipo mbaya sana.

“Leo hii unapoona halmashauri zimepewa nafasi hiyo lakini still zimelala kuanzia wilayani hadi mkoani hapo kuna matatizo,”alisema Waziri Jafo.

Alibainisha kuwa ni lazima kubadili mbinu za ukusanyaji wa mapato kwa kuwa serikali lengo lake kubwa ni kuhakikisha inaondoa mzigo kwa watu wanyonge na ili hizo kodi na tozo zenye kero ziweze kuondoka ni lazima halmashauri iweze kupata mapato kwa njia nyingine mbadala.

“Jiji la Dodoma hawapo hapa,sijui kiburi cha  kukusanya mapato mengi ndio maana hawataki kuja hapa na fedha hizo ujue ni fedha za kwetu tumeandikia miradi sisi ya TSP  wala hawajaandika ya kwao,nilitamani waje hapa wajifunze, leo hii Dodoma mpaka mwezi huu wameshakusanya Sh.Bilioni 60 wangekuja hapa wangepata maarifa mengine zaidi,”alisema.

Alizitaka halmashauri kutekeleza miradi inayopelekwa kwao bila ya kusua sua kwa kuingiza maslahi yao hasa katika ajenda ya manunuzi ambapo kila mtu anaenda na makaratasi yake ikiwa na mkadarasi wake hali inayofanya miradi hiyo kutoendelea mbele .

Awali, Mkurugenzi Msaidizi Idara za Serikali za Mitaa, Angelista Kihaga alisema miradi ya kimkakati ni utaratibu mpya wa serikali wa kutoa fedha za maendeleo kwa mamlaka za serikali za mitaa.

Naye, Kaimu Mkuu wa Chuo cha Hombolo Dk. Michael Msendekwa alisema mafunzo hayo yametokana na tafiti zilizofanywa na chuo hicho kuonyesha kuna changamoto katika maandishi ya miradi katika mamlaka za serikali za mitaa.

Alisema mafunzo hayo yanatolewa kwa ushirikiano baina ya TAMISEMI na Wizara ya Fedha lengo likiwa ni kuelekezana na kusaidiana kutatua changamoto hiyo.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com