Mhandisi Burton Komba
kutoka Wakala wa Barabara akitoa maelezo ya Ujenzi wa Jengo la III la abiria
kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Miundombinu walipofanya ziara katika Jengo hilo mapema leo.
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege
Tanzania (TAA), imebainisha kwamba itakua tayari kwa ajili ya utoaji wa huduma
za uendeshaji katika Jengo la tatu la abiria pale mradi wa Ujenzi utakapokuwa
umekamilika.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es
Salaam na Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere
(JNIA), Bw. Paul Rwegasha alipokua akitoa taarifa fupi ya TAA kwa Kamati ya
Bunge ya kudumu ya Miundombinu ilipofanya ziara katika eneo la Ujenzi huo.
Bw. Rwegasha amesema hatua
mbalimbali za Maandalizi tayari zimeshachukuliwa kwa kushirikiana na wadau wa huduma
hizo, ikiwa ni pamoja na utoaji wa mafunzo yanayohitajika kwa watendaji wa
ngazi mbalimbali.
“Mamlaka inaendelea kufanya taratibu za maandalizi ya
utoaji huduma za uendeshaji katika Jengo la tatu la abiria, katika mpango huo
tayari mafunzo kwa watendaji mbalimbali yameanza na hivi sasa watendaji 40 wapo
Korea ya kusini katika mafunzo” amesema Bw. Rwegasha.
Aidha Bw. Rwegasha amebainisha
kwamba katika utekelezaji mpango wa uhamishaji shughuli, Mamlaka imejipanga
kuhakikisha hakuna madhara yeyote ya kiuendeshaji yanajitokeza.
“Mamlaka itahakikisha kwamba inazuia
athari zote zinazoweza kutokana na zoezi la uhamishaji wa shughuli za
uendeshaji ikiwa ni pamoja na kuchelewa kwa Ndege na abiria, uharibifu wa
mitambo,madhara ya kiusalama na kadhalika.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi
wa Idara ya Viwanja vya Ndege katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
Mhandisi Emmanuel Raphael amebainisha kwamba
hadi kufika mwezi February 2019 utekelezaji wa kazi zote ulifikia asilimia 95.
“Ujenzi wa kazi zote za Ujenzi
umefikia 95%, ambapo mchanganuo unaonesha kwamba ujenzi wa jengo umefikia 96%,
maegesho ya magari 92%, maegesho ya ndege 98% na kwa ujumla kazi zinaenda
vizuri na zinatarajiwa kukamilika Mei 31, 2019”, alisema Mhandisi Raphael.
Naye, Naibu Waziri Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amebainisha kwamba mpaka
sasa Wananchi wa Kipawa waliopisha upanuzi wa Kiwanja wameshalipwa fidia na
kwamba mpaka sasa hamna mgogoro wa fidia.
Akitoa majumuisho baada ya ziara
ya kamati katika eneo la ujenzi, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Bunge, Mhe.
Seleman Kakoso amesema kwa ujumla Kamati imeridhishwa na hatua ya ujenzi
iliyofikiwa na kwamba wameridhishwa na namna pesa ya serikali ilivyotumika.
“Kwa ujumla Kamati imeridhishwa
na hatua ya Ujenzi iliyofikiwa, matumizi ya pesa ya Serikali yanaonekana ni
mazuri, lakini natoa wito kwa TAA kuongeza kasi ya maandalizi ili kwenda sawa
na kasi ya ujezi huu, lakini pia mjipange kuongeza wafanyakazi ili kuhakikisha
kwamba watendaji wa huduma za uendeshaji wanajitosheleza”, amesema Mhe. Kakoso.
0 comments:
Post a Comment