METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, January 14, 2019

Nkasi waitikia wito wa serikali katika kukikuza kilimo cha kahawa Mkoani wa Rukwa


Wakulima katika halmashauri ya wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa wameitikia wito wa kuunga mkono juhudi za serikali katika kukuza zao la kahawa mkoani Rukwa na kuhakikisha wanalima zao hilo kwa wingi ili kubadili kipato chao na hatimae kushawishi wawekezaji wa kuchakata zao hilo kuwekeza Mkoani humo ili kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Zao la kahawa ni miongozi mwa mazao matano ya kimkakati yanayohimizwa na serikali ya awamu ya tano katika kuinua kipato cha wananchi pamoja na pato la nchi kwa ujumla.
Wakulima hao wakiongozwa na mkulima mzoefu wa zao hilo Elias Mwazembe alisema kuwa zao la kahawa linastawi katika mkoa mzima wa Rukwa hivyo aliushukuru uongozi wa Wilaya pamoja na Mkoa kwa kuendelea kuwasaidia pale wanapokwama mbali na changamoto aliyoipata mara ya kwanza alipolima katika hifadhi yam situ wa mfili na kuondolewa na serikali.
“Nilipoona kwenye Mkoa inakubali na kwenye wilaya ikabidi nije huku (Kijiji cha) Kalundi nikaanzisha kulima mwezi wa tatu nikaona ile kahawa inastawi vizuri kwahiyo nikaona hapa sio pa kuachilia niendelee na zao la kilimo lakini sikutulia niliendeleza hamasa kwa watu wengine kuwaambia kuwa zao la kahawa mkoani Kwetu linakubali ingawa changamoto ikawa mtu alikuwa anahitaji avune kwa mwaka huo huo nikasema mbegu iliyopo ni miaka miwili unaweza kuvuna kahawa na kwa umri nilionao nitavuna mpaka vitukuu,” alisema.
Nae Afisa kilimo wa Kijiji cha Kalundi Jiasi Muyunga alikiri kuwa kitendo cha mkulima huyo Elias Mwazembe kufika katika Kijiji hicho kumepelekea wakulima wengi kutaka kujihusisha na kilimo hicho cha kahawa baada ya kuona kuwa kinastawi vizuri katika Kijiji hicho na hivyo kutoka wito kwa maafisa ugani wenzie juu ya kuwasaidia wakulima na kuwakikishia kuwa zao hilo ndilo litakalokuwa mkombozi.
Kwa upande wake Afisa kilimo wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi alisema kuwa baada ya kubaini kwamba kata 18 zilizopo ufipa ya juu zenye eneo la hekta 48,000 kuwa zinafaa kulima zao hilo hal,mashauri ilianisha maeneo ya kuanza nayo huku wakishirikiana na kituo cha utafiti cha Tacri kilichopo Mbimba Wilaya ya Mbozi, ili kujua mbegu inayofaa katika maeneo hayo na hatimae kuwapeleka wataalamu na wakulima kwenda kujifunza.
“Mkulima ambaye tumemtembelea leo ndugu Mwazembe ni mmoja wa wakulima hao ambao nae alikwenda kujifunza Mbimba na baada ya kutoka huko aliendeleza juhudi za kufanya kilimo hiki cha kahawa na tunae mkulima mwingine yupo Kijiji cha Kakoma kata ya Namanyere nae pia mepanda kahawa karibu miche 500 na kitaluni ana miche karibu 12,000 na kuna taasisi zaidi ya sita ambazo tumepa miche iliyotokana na kilo 100 za mbegu ambapo kila kilo moja inatoa miche 4000, hivyo tunaamini baada ya miaka mitatu halmashauri itaanza kuona faida yake,” Alisisitiza.
Aidha Afisa kilimo wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa Ocran Chengula aliwashauri wakulima wote wanaotarajia kuanza kilimo hicho cha kahawa kuhakikisha kuwa wanaandaa mashimo mapema na kuweka mbolea ili iweze kuchangayikana na udongo
“Tunatakiwa kuandaa mashimo mapema, kama unategemea kupanda mwaka huu maana yake unaze kuandaa mashimo mwezi wa nane ama wa tisa kwa kuchimba mashimo na kuweka mbolea ili mbolea iweze kuchanganyikana na udongo ikishaanza mvua mwezi wa kumi na moja ile miche inatakiwa ihamishwe kwenye mashamba ili mvua itakavyonyesha iweze kushika na kuwa na nguvu zaidi ya kuweza kukua,” Alifafanua.
Mkoa wa Rukwa unategemea kuwa na miche 1,040,000 ifikapo mwakani inayotokana na kilo 260 za mbegu za kahawa inayopandwa kwenye vitalu mwaka huu ili kuweza kuisambaza kwa wakulima na taasisi mbalimbali ikiwa ni kuhamasisha kilimo cha zao hilo pamoja na kuinua kipato cha wananchi, mkoa na taifa kwa ujumla.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com