METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, January 5, 2019

Matinga: Utafiti kuongeza tija na uzalishaji wa madini kwa wachimbaji wadogo




Na Priscus Benard – Mpanda Katavi

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Katavi ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Lilian Matinga amewataka wachimbaji wadogo kuachana na  kutafuta na kuchimba madini kimazoea badala yake  wafuate njia ya kisayansi katika kutafuta, kuchimba na kuchenjua madini katika maeneo yao ili kuongeza tija, pato lao na Taifa kwa ujumla.  

Aliyasema hayo Disemba 4  wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wachimbaji wadogo eneo la D reef na Kapanda Mkaoni Katavi,  na kuongeza kuwa, masuala ya madini ni ya kisayansi na hivyo  kuwataka wachimbaji wadogo kuondoa dhana mbaya iliyojengeka kwa baadhi yao kuwa ukitaka kufanikiwa katika kuchimba madini unatakiwa uende kwa waganga wa jadi.

Mafunzo hayo kwa wachimbaji wadogo, yanafuatia utafiti wa kina wa jiosayansi uliofanywa na wataalam kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST)  kwa kushirikiana na wataalam kutoka Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

Aliongeza kuwa, utafiti huo umefanyika kufuatia nia na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano  inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli katika kuhakikisha kuwa wachimbaji wadogo wanaondokana na uchimbaji usio na tija na kwenda kwenye uchimbaji utakaoongeza kiwango cha uzalishaji na hivyo kuongeza kipato kwa wachimbaji na kuboresha maisha yao na jamii kwa ujumla.

“Baada ya kutumia taarifa za utafiti huu ni matumaini yangu kuwa kipato chenu na mapato yatokanayo na uchimbaji mdogo wa madini kwa ujumla yataongezeka,” alisema  Matinga.

Pia, Matinga aliwataka wachimbaji wadogo kuwa wazalendo katika kulipa kodi ili kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Magufuli katika kuliletea taifa maendeleo makubwa zaidi.

“Miradi ya maendeleo inahohitaji fedha ni mingi ukianzia elimu bure, mradi wa reli ya kisasa, bwawa la kuzalisha umeme na mengine mengi,” alisisitiza Matinga.

Awali, akitoa taarifa ya mazfunzo hayo, Kaimu Mtendaji Mkuu wa GST, Yokbeth Myumbilwa alisema utafiti wa kina ulifanyika kwa lengo la  kubaini uwepo na kiasi cha madini, mwelekeo wa miamba, ubora na tabia za mbale katika maeneo ya D-reef, Kapanda na Ibindi Mkoani Katavi.

Myumbilwa alibainisha kuwa matokeo ya utafiti huo yanaonesha uwepo wa mbale za dhahabu kiasi cha tani 4,394,162 zenye wakia 45,773.40 (kilo 1,423.71) za dhahabu katika eneo la D-reef na tani 452,215 zenye wakia 1,831.92 (kilo 56.98) za dhahabu katika eneo la Kapanda.

“Matokeo haya ni kwa maeneo ya D-reef na Kapanda yenye ukubwa wa jumla ya kilomita za mraba 0.06 yaliyofanyiwa uchorongaji,” alisema Myumbilwa.

Pia, alieleza kuwa, wataalamu wa GST wapo Mpanda kwa ajili ya kutoa mafunzo (mrejesho) juu ya matokeo ya utafiti huo. “Kuna watu walifikiri hatutarudi tena lakini niwahakikishie Serikali ya awamu ya tano ipo pamoja nanyi ndiyo maana tumerudi hapa kuwapa mafunzo baada ya kukamilika utafiti uliofanyika tokea 2016,” alisema Myumbilwa.

Vilevile, alisema kuwa, kupitia mafunzo hayo yatatoa msukumo katika kuboresha utafutaji, uchenjuaji na uchimbaji salama na hatimaye kuongeza tija na kipato cha wachimbaji wadogo.

“Wachimbaji wadogo wanapoteza fedha zao na muda mwingi kwa sababu nyingi ikiwa ni pamoja na kuchimba kwa kubahatisha na kutokujua njia bora za unjenjuaji madini na hivyo kupelekea madini yao mengi kupotea kupitia mabaki,” alisisitiza.

Mnamo Mwaka 2016 Serikali ilitenga kiasi cha dola za kimarekani 3,703,630 kwa ajili ya utafiti wa kina wa jiosayansi chini ya mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) ili kuboresha maisha ya mchimbaji mdogo na kutatua changamoto zinazomkabili ikiwa ni pamoja na uzalishaji mdogo na uchimbaji usiozingatia usalama na afya kwa mchimbaji.
Xxxxxxx xxxxxxx
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com