METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, January 24, 2019

HALMASHAURI YA CHEMBA YAAGIZWA KUPITIA UPYA UAMUZI WA KUCHUKUA ASILIMIA SITINI


Naibu waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk Angeline Mabula akisalimiana na viongozi wa wilaya ya Chemba mkoani Dodoma alipowasili kwa ajili ya  kuhamasisha ukusanyaji maduhuli ya serikali kupitia kodi ya ardhi. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Chemba Simon Odunga.
Naibu waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk Angeline Mabula akizungumza na wajumbe wa kamati ya Ulinzi na Usalama pamoja na watendaji wa sekta ya ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoa wa Dodoma alipofanya ziara ya  kuhamasisha ukusanyaji maduhuli ya serikali kupitia kodi ya ardhi.
Na Munir Shemweta, CHEMBA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angelina Mabula ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kupitia upya uamuzi wake wa kuchukua asilimia sitini wakati wa kutwaa maeneo ya wamiliki  wa Ardhi katika  halmashauri hiyo.
Dkt Mabula alitoa kauli hiyo jana akiwa katika mfululizo wa ziara zake za kuhamasisha ukusanyaji maduhuli ya Serikali kupitia kodi ya Ardhi katika halamashauri za mkoa wa Dodoma.
Alisema uamuzi uliofanywa na halmashauri ya Chemba kuchukua asilimia sitini ya eneo na kumuachia mmiliki asilimia arobaini siyo cha kiungwana na ni cha kinyonyaji ambacho kwa kiasi kikubwa kinamdhulumu mwenye eneo.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi alitoa kauli hiyo baada ya kuelezwa kuwa katika halamashauri hiyo kuna sintofahamu kufuatia halmashauri kuamua kupima viwanja kwenye eneo la Mapango Mji wa Chemba ambapo wananchi wasiokuwa na uwezo wa kupima viwanja halmashauri inawapimia kwa kuchukua asilimia sitini na kuwaachia arobaini.
Alisema, uamuzi wa kuchukua asilimia sitini ya eneo unaofanywa na halmashauri ya Chemba ni tofauti kabisa na inavyofanyika katika halmashauri nyingine ambazo zimekuwa zikiwaachia wamiliki asilimia sitini mpaka sabini.
Dkt. Mabula ameitaka halmashauri ya Wilaya ya Chemba kupitia upya uamuzi wake huo ili kuondoa mgongano baina yake na wananchi ambapo alibainisha kuwa katika zoezi hilo wamiliki wanaweza pia kuuza maeneo kwa watu wengine lengo likiwa kupata fedha ya kumilikishwa maeneo yao.
Alisema, pamoja na kuigiza halmashauri hiyo kupitia upya uamuzi wake lakini pia watendaji wa sekta ya ardhi wanapaswa kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na zoezi hilo ili kurahisisha upimaji kwa lengo la kuwa na mji uliopangika.
Mkuu wa Idara ya Ardhi katika Halamashauri ya Wilaya ya Chemba Enock Mligo alisema halmashauri hiyo kwa sasa inasimamia ukuaji wa Mji wa Chemba na kupima maeneo kwa ajili ya matumizi mbalimbali.
Alisema eneo la Mpango Mji wa Chemba linaundwa na vijiji sita ambapo shughuli mbalimbali za upangaji wa mji zinatekelezwa kwa mujibu wa sheria ya Mipango miji na kubainisha kuwa mchakato wa kuvifuta rasmi vijiji hivyo sita umeshaanza na kuwasilisha maombi Ofisi ya Rais TAMISEMI ili kuanzisha Mamlaka ya Mji mdogo wa Chemba.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com