METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, November 25, 2018

MHE HASUNGA ATANGAZA KIAMA KWA WASAMBAZAJI WA MBEGU FEKI

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga akikagua Maabara ya Kutazama kiwango cha Uotaji wa Mbegu wakati wa ziara yake ya kikazi Mkoani Morogoro alipotembelea Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), tarehe 24 Novemba 2018. (Picha Zote Na Mathias Canal-Wizara ya Kilimo)
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga akikagua shamba la mahindi wakati wa ziara yake ya kikazi Mkoani Morogoro alipotembelea Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), tarehe 24 Novemba 2018.
Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) Ndg Patrick Ngwediagi akitoa taarifa ya Taasisi hiyo mbele ya Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga tarehe 24 Novemba 2018.
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga akikagua bustani ya nyanya wakati wa ziara yake ya kikazi Mkoani Morogoro alipotembelea Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), tarehe 24 Novemba 2018.

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Morogoro

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga, 24 Novemba 2018 ametangaza kiama kwa wafanyabiashara wa mbegu nchini wanaouza Mbegu feki zilizopigwa marufuku na serikali.

Amewataka wafanyabiashara wote wa mbegu ambao wamekuwa wakifanya biashara hiyo kwa kuwauzia wakulima mbegu feki zilizopigwa marufuku na serikali kuacha haraka iwezekanavyo kwani serikali itawachukulia hatua za kisheria wale wote watakaobainika kukiuka maagizo ya serikali.

Ametoa agizo hilo akiwa ziarani Mkoani Morogoro ambapo pamoja na mambo mengine alitembelea Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), Taasisi iliyopewa jukumu na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania la usajili wa wafanyabiashara wa mbegu (Seed Dealers).

"Serikali imepokea malalamiko mengi kwa wananchi kuhusu Ubovu wa mbegu jambo ambalo limepelekea kwa kiasi kikubwa kuwa na mavuno kidogo pasina kukidhi matakwa ya wakulima wetu nchini" Alikaririwa Mhe Hasunga

Waziri huyo pia ameiagiza Taasisi ya udhibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) kutimiza majukumu yao kwa kuwabaini wafanyabiashara wanaokiuka maagizo ya serikali pamoja na taratibu na sheria za nchi.

“Kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu mbegu feki jambo hili serikali haiwezi kukubaliana nalo hivyo TOSCI wanapaswa kusimamia kwa weledi ukaguzi na usajili wa Mbegu bora, pia ni lazima kuwabaini wasambazaji feki wa mbegu ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao” Alisisitiza Mhe Hasunga

Alisema Wizara ya Kilimo imepewa jukumu mahususi la kuhakikisha sekta ya kilimo inaimarika kwa usimamizi madhubuti wa sera, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali hivyo kunapokuwa na kelele za wananchi kuhusu mbegu feki ni dhahiri kuwa Taasisi zenye jukumu hilo hazitekelezi kazi yake kwa weledi.

Mhe Hasunga alieleza kuwa serikali imejipanga kuhakikisha kuwa inaongeza thamani ya mazao yote yanayozalishwa nchini, sambamba na kutafuta masoko mazuri.

Vilevile, ameitaja Wizara ya Kilimo kuwa ina wataalamu wengi hivyo unaandaliwa mfumo mzuri wa kuwaunganisha watalaamu hao ili kujadili kwa pamoja namna ambavyo kilimo kinaweza kubadilika kutoka kilimo cha kujikimu na kuwa kilimo cha kibiashara ili kutoa malighafi za kutosha zitakazohuisha serikali ya viwanda.

MWISHO.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com