METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, July 19, 2018

Naibu Waziri Doto Biteko aahidi neema kwa wachimbaji wadogo nchini


Na George Binagi-GB Pazzo, BMG

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko amewaagiza Maafisa Madini nchini kuhakikisha wanatenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo, badala ya kutoa kipaumbele kwa wachimbaji wakubwa pekee.

Biteko amesema serikali itaendelea kuwatufia leseni ya uchimbaji watu wote waliohodhi maeneo makubwa yenye madini bila kuyaendeleza ili wachimbaji wadogo wapatiwe maeneo hayo.

Naibu Waziri huyo aliyasema hayo Julai 17, 2018 wakati akizungumza na wachimbaji wadogo katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Masugulu.

“Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ukurasa wa 35 tamko namba 25 imetuelekeza tukawatengee maeneo ya kuchimba wachimbaji wadogo, Na mimi nimekuja kuwapa taarifa kwamba mtu yeyote kwenye Wizara ya Madini asiyefuata utaratibu huo hataki kazi yake”. Alikaririwa na kuongeza;

“Ninachukua nafasi hii kuwaagiza Maafisa Madini wote nchini wakiwemo wa Songea, wasikilizeni wachimbaji wadogo, marufuku kumuona tajiri wa maana kuliko masikini. Hawa tukiwasimamia vizuri, matajiri watatoka humu humu”. Alisisitiza Biteko.

Awali Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji na Wafanyabiashara wa Madini mkoani Ruvuma (RUVREMA), Ndg Isack Ngerangera alimpongeza Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli kwa kuchukua hatua stahiki ili kulinda rasilimali madini nchini ikiwemo kufanya marekebisho ya sheria ya madini.

Ngerangera alisema wachimbaji wadogo mkoani Ruvuma wanaamini baadhi ya changamoto zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa maeneo ya uchimbaji zitatatuliwa ambapo aliomba wapewe baadhi ya maeneo ambayo yamekaliwa na watu wenye leseni ambazo hawazifanyii kazi na hivyo kuikosesha serikali mapato.

Naye Mkuu wa Mkoa Ruvuma Mhe Christina Mndeme alisema serikali itaendelea kupima maeneo kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo uchimbaji madini, ufugaji pamoja na kilimo na hivyo kuwataka wananchi kuheshimu maeneo hayo kwa kufanya shughuli zao bila kuingiliana ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima.
Naibu Waziri wa Madini Mhe.Dotto Biteko akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini katika Kijiji cha Masugulu wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma
Wachimbaji wadogo wilayani Mbinga wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa Ruvuma Mhe Christina Mndeme baada ya Naibu Waziri wa Madini Mhe.Doto Biteko kukutana na wachimbaji hao akiwa ziarani mkoani humo
Mmoja wa wananchi akinasa ujio wa Naibu Waziri wa Madini katika Kijiji cha Masugulu wilayani Mbinga
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com