METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, February 9, 2018

MBUNGE WA ILEMELA AKABIDHI MASHINE ZA KUFYATULIA TOFALI KWA UVCCM

Mbunge wa Jimbo la Ilemela na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe Dkt Angeline Mabula  amekabidhi mashine mbili za kufyatulia tofali kwa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi kata ya Kayenze  na Kikundi cha Wasaka Tonge kuhakikisha anawasaidia vijana wa jimbo lake katika kupambana na changamoto ya upatikanaji wa ajira

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Katibu wa ofisi ya mbunge ndugu Michael Goyele   aliyemwakilisha mbunge Dkt Angeline Mabula katika kukabidhi mashine hizo amewaasa vijana hao kuzitunza mashine hizo na kuzitumia kwa lengo lililokusudiwa huku akiwahakikishia kuwa mbunge wao ataendelea kushirikiana nao katika kupunguza tatizo la ajira kwa kuchukua jitihada mbalimbali kwa ushirikiano wa taasisi za umma na binafsi za ndani na nje ya jimbo lake

;… Mbunge wenu amenituma nije kuwakabidhi mashine hizi, Ila anachoomba ni kuhakikisha mnazitunza na kuzitumia kwa malengo yaliyokusudiwa ili vijana wote waweze kunufaika na kupunguza tatizo la ajira linalowakabili kwa kuweza kujiajiri …’ Alisema

Aidha mbunge huyo ameendelea kuziomba taasisi mbalimbali kuja kuwekeza katika jimbo lake lenye fursa nyingi za kiuchumi na kijamii ili kutoa nafasi za ajira kwa vijana wake na kuomba viongozi wengine kuunga mkono jitihada za kuwakwamua vijana na wajasiriamali wadogo waweze kujikomboa kiuchumi

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Kayenze Mhe  aliyeshuhudia makabidhiano hayo  mbali na kushukuru kwa mashine hizo kwa niaba ya vijana wa kata yake, Amempongeza Mbunge Dkt Angeline Mabula huku akisisitiza kuendelea kuunga mkono jitihada zote zinazofanywa na mbunge huyo katika kumaliza kero na adha zinazowakabili wananchi wake

Wakihitimisha Vijana wa Kikundi cha Wasaka Tonge wamemshukuru mbunge wao kwa kuliona  tatizo hilo kubwa la muda mrefu la ukosefu wa ajira na kuamua kulitafutia ufumbuzi sanjari na kumuhakikishia kuwa watazitunza mashine hizo na kuzitumia kwa lengo la kunufaisha wanakikundi wote  waweze kujiletea maendeleo binafsi na jamii kiujumla huku wakiomba Umma kuunga mkono  mradi wao unaotarajiwa kuanza muda si mrefu wa kufyatua tofali ili kurahisisha upatikanaji wa soko la kudumu na la uhakika

Makabidhiano hayo ya mashine za kufyatulia tofali kwa vijana wa kata ya Kayenze pia yalishuhudiwa na mwenyekiti wa umoja wa vijana wa wilaya ya Ilemela, viongozi wa chama cha mapinduzi  wa kata ya Kayenze na wazee maarufu wa eneo hilo

‘ Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga’

Imetolewa na
Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Ilemela
09.02.2018

Share:

Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2025 WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com