METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, August 29, 2017

Soko la ajira linahitaji ujuzi binafsi zaidi ya vyeti

Na Abdallah Ng’anzi 

Kuna nyakati unatafakari namna  mambo yanavyokwenda hasa katika zama za hizi za kidigitali, moja ya jambo kuu linaloumiza vichwa vya wahitimu wengi  ni ukosefu wa ajira. 

Ajira imekuwa changamoto si kwa Tanzania pekee bali kilio cha ukosefu wa ajira kinasikika kila kona ya dunia. 

Kwa mujibu wa ripoti ya shirika la kazi duniani (ILO) mwaka 2017 idadi ya watu wasio na ajira itaongezeka kwa asilimia 5.8 (awali ilikuwa asilimia 5.7) na kufanya jumla ya watu wasio na ajira kufikia milioni 500.8 duniani.

Hili si jambo zuri kulisikia likitamkwa kwani ndoto za wasomi wengi ni kujiajiri au kuajiriwa na kufaidi kile ambacho wamekitafuta kwa zaidi ya miaka 18 wakiwa darasani. 

Zipo sababu zinawakosesha ajira vijana wengi, miongoni mwa sababu hizo ni ujuzi binafsi wa mtu ukiachana na vyeti alivyo navyo. Kwa mfano mhitimu akiulizwa mbali na elimu aliyonayo ni kipi cha ziada alichonacho.

Katika dunia ya sasa elimu siyo stashahada, shahada au zaidi. Elimu ni namna unavyoweza kukabiliana na mazingira magumu ya ushindani. Kwa sasa kama Taifa tumeanza soko la pamoja la Afrika Mashariki, lakini tukiwa kama Taifa tunachanganyika na watu wa mataifa mengine.

Kuna fursa nyingi tu zinazoweza kubadilisha maisha yetu zaidi ya kutegemea ajira rasmi.

Mathalani, mara nyingi watu wanauliza kozi gani inalipa. Ukweli wa mambo ni kuwa kila kilichopo duniani ukiweza kukitumia vizuri na kwa maarifa kinalipa. Lakini pia lazima uelewe kuwa milango haipo wazi kana kwamba utaweza kupata kila kitu kama unavyotarajia, inahitaji uvumilivu na kuvuja jasho.

Mambo yamebadilika, kuna wasomi wengi wenye sifa wanazurura, vijana wanapaswa kutambua kuwa soko la ajira la sasa haliangalii shahada wala stashahada, linaangalia wewe kama mwajiriwa utaleta mabadiliko gani chanya katika kuliletea maendeleo. 

Waajiri wanaangalia una kitu gani kinachokutofautisha na washindani wengine, nafasi moja ya kazi inaweza kuombwa na watu 300, lazima uoneshe sifa zitakazowashawishi kwanini wewe uajiriwe na si mwingine ambaye licha ya ukubwa wa shahada yake lakini pia ana uzoefu kukuzidi.

Pili unawezaje kujiuza kwa sababu nyote mliopeleka wasifu mna bidhaa ile ile, sasa kwanini wakuajiri wewe, je bidhaa zako ni bora zaidi ya zile 299 zilizojitangaza kuwania nafasi hiyo? 

Ninachotaka kusema hapa ni kwamba, kuwa na shahada ya uzamili au udaktari bado hakujakuhakikishia nafasi katika ushindani wa dunia ya leo. Ni jinsi gani unajiuza na unaweza kuuza hizo degree zako.

Tena teknolojia imesonga mbele , barua zinachaguliwa kwa kompyuta, suala la kuajiriwa kwa kujuana linaanza kutoweka kwa waajiri kuhitaji ueledi zaidi na sifa za ziada. 

Ni vema vijana wakafahamu kuwa si lazima kufanya kazi waliosomea tu bali wanaweza kutumia elimu hiyo kama njia ya kufungua fursa mpya na kuziendeleza kwani kuwa na elimu katika taaluma fulani hakumuzuii mtu kufanya kazi nyingine.

Katika dunia ya leo kinachoweza kupunguza janga la ukosefu wa ajira kwa vijana wengi ni kuona fursa na kuzitumia ili kujitengenezea kipato nje ya ajira zao badala ya kutegemea elimu zao tu.

Ni kweli vijana hususani hapa nchini hawajaona fursa hata katika sekta ya kilimo ambayo hutegemewa kwa kiasi kikubwa katika maisha ya kila siku ya mwanadamu kwa kutoa hitaji kuu na la lazima linalowezesha kuishi (chakula).

Naamini eneo hili kama vijana wangeamua kujiajiari hapa na kuwekeza nguvu na fikira zao basi kusingelikuwa na kundi kubwa la watu wanaolia kwa kukosa ajira maana wangejiajiri wao na kuwaajiri wengine wengi.

Hebu fikiria wakati huu ambao Kenya inakabiliwa na tishio la ukame unaosababisha wananchi kukosa uhakika wa chakula na kuilazimu serikali nchini humo kuweka utaratibu wa kila familia kununua mfuko mmoja tu wa unga wa mahindi kwa siku ili kuwezesha walau kila familia kupata mkate wa kila siku, ingeweza kuwa fursa kwa vijana kuongeza utajiri na kukuza soko kwa kuomba vibali vya kuuza nafaka nchini humo.

Naamini kuwa ajira zinaweza kupatikana, vijana na jamii kwa ujumla waachane na dhana ya kutaka kuajiriwa kwa kwenye sekta rasmi tu bali wafikirie kuhusu kujiajiri na zaidi.

Mwisho.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com