MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM, Sophia Simba na wanachama wengine wamefukuzwa uanachama huku wengine wakipewa onyo kali.
Usaliti ndilo kosa lililowagharimu wanasiasa hawa akiwamo Simba
ambaye ni mkongwe ndani ya chama hicho tawala. Siku chache kabla ya
uamuzi huo kufanywa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Simba ambaye
alikuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT), alitangaza kuwa
hatagombea tena wadhifa huo.
Maswali yanayokuja ni je, alijua kinachokuja mbele yake kuwa ni
kufukuzwa chama? Je, ataendelea na siasa kupitia vyama vingine?
Alichokizungumza siku chache kabla ya kufukuzwa, kinaweza kutoa majibu
ya maswali haya.
Mkutano wake na wana UWT, wilaya wa Temeke, mkoani Dar es Salaam
uliojielekeza kwenye kuzungumza Siku ya Wanawake Duniani iliyoadhimishwa
Machi 8, ilikuwa ni miongoni mwa majukwaa ambayo mwanasiasa huyu
alipata fursa ya kuwaaga wanachama.
Simba ambaye ifikapo Julai 27 mwaka huu, atatimiza umri wa miaka 67,
aliwaeleza kuwa anaona vipindi viwili alivyotumika katika umoja huo
vinatosha na kwamba sasa anawaachia wengine. “Namshukuru Mwenyezi Mungu
kwa nafasi alizonijaalia kwani nimekuwa mbunge kwa miaka 22 sasa na
katika miaka hiyo nilibahatika kuteuliwa na kuwa waziri kwa kipindi cha
miaka 10,” alikaririwa Simba.
Tamko la kutangaza kutogombea tena uenyekiti wa UWT lilikuwa
linazingatia kwamba, mwaka huu utafanyika uchaguzi ndani ya CCM pamoja
na jumuiya zake zote. Aliwahamasisha wanawake wote wanaojitambua kuwa
wanaweza uongozi, hususan wana UWT wa kutoka kona zote za nchini,
kujitokeza kuchukua fomu na kugombea nafasi mbalimbali.
“Naomba tusiogopane, nafasi zi wazi na hakuna nafasi ya mtu.
Kumbukeni ule usemi wetu ‘Wanawake Jeshi Kubwa – Ushindi ni Lazima’.
Sisi wanawake tupo wengi tupigiane kura tutashinda. Wanawake wa CCM
tunaweza na chama chetu kinatambua hivyo,” anasema.
Waziri huyo wa zamani aliweka wazi alianzia katika nafasi ya ukatibu
wa tawi la kazini NDC, kisha akawa mwenyekiti wa UWT wa kata ya Upanga
Magharibi, Ilala kabla ya kupata udiwani. Wakati huo huo alishinda
nafasi ya kuwa mbunge wa viti maalumu mwaka 1995.
Akaeleza anavyojivunia kuwa mwanachama mwaminifu wa CCM katika maisha
yake yote. “Mimi nimekulia na kulelewa na wazazi wangu na viongozi
wangu wana TANU na CCM katika maisha yangu yote,” alisema.
Alikiri kuwa uchaguzi ndani ya CCM mwaka huu, utazingatia azma ya
mikakati madhubuti iliyokwishatangazwa na viongozi wa juu wa chama,
hususani mwenyekiti Rais John Magufuli. Alikiri pia kuwa azma iliyopo,
ni kukijenga chama upya na hatimaye Tanzania mpya.
Huku pengine akiwa hajui ambacho kingelimkumba, mwanasiasa huyu
alimuomba Mungu amjaze hekima aendelee kuwa mwana CCM mwaminifu katika
maisha yake yote yaliyobaki. “Hiki ndicho chama ninachokijua na mimi ni
mwana CCM wa asili nisiyeyumba na namuomba Mwenyezi Mungu anijaze hekima
ya kuendelea kuwa mwanaCCM mwaminifu katika maisha yangu yote
yaliyobaki,” alisema.
Katika kauli zake kwenye mkutano huo, inaonesha Simba alikuwa na
imani kuwa ataachia wadhifa huo baadaye mwaka huu baada ya kuitumikia
jumuiya hiyo kwa mapenzi, utii, uaminifu na uadilifu mkubwa kwa kipindi
cha kutosha. Kauli hii inadhihirisha hakujua kama Machi 11, 2017
ingekuwa ndiyo mwisho wa kushikilia wadhifa huo.
Akaeleza kuwa hana shaka iwapo wanawake wengine wenye uwezo wa
kuendeleza harakati za kuwaunganisha wanawake na kuhakikisha chama
kinaendelea kushika dola. “Likiwemo jukumu kubwa la kisiasa na la
kipaumbele ndani ya jumuiya ya UWT. Ambalo ni kuhakikisha kuwa Chama
chetu cha Mapinduzi kinaendelea kushika dola,” alisema mwenyekiti huyo.
Alisisitiza kuwa kwa hiari yake ameamua kutogombea nafasi hiyo ya
uenyekiti wa UWT katika uchaguzi ujao kwa kuwa azma yake tangu
aliposhika wadhifa, ilikuwa ni kutumikia vipindi viwili.
“Nitakabidhi kijiti hiki kwa uongozi utakaochaguliwa kama ilivyo mila
na desturi za chama chetu. Sina shaka kabisa wapo wanawake wengine
wenye uwezo wa kuendeleza harakati za kuwaunganisha wanawake katika
kupigania maslahi na haki zao za msingi, haki na ustawi wa watoto na
masuala ya jamii kwa ujumla.
Simba akawaeleza wana UWT Temeke kuwa ameamua kutangaza mapema azma
ya kutogombea ili kuwaweka huru na kuwapa muda wa kujipanga vizuri wale
wote wanaokusudia kugombea nafasi hiyo kubwa ndani ya jumuiya yao. Pia
akasema ameamua kutangaza mapema ikiwa ni njia mojawapo ya kutoa majibu
kwa wale walioku wa wakimuuliza na kumhamasisha aendelee kugombea.
Iwe, ama alijua au hakujua kama ungefanyika uamuzi mgumu ndani ya
chama juu yake, kinachobaki ni kwamba, Sophia Simba si mwana CCM tena.
Azma ya kujenga chama upya imemkumba na yeye. NEC imekomesha ndoto zake
za kuendelea kuwa mwanaCCM mwaminifu katika maisha yake yote yaliyobaki
kama alivyosema.
Sasa hatasubiri tena baadaye kuachia wadhifa huu wa UWT na kushiriki
uchaguzi, bali anaachia mara moja kwa kuwa siyo mwanachama tena na ndoto
za kuona CCM kinaendelea kushika dola kama ambavyo alikaririwa akisema
hatasaidia kuzikamilisha.
Ni dhahiri Simba aliutumia mkutano huo wa Temeke kuwaaga wana UWT na
chama kwa ujumla, ama kwa kufahamu au kwa kutofahamu. Katibu wa UWT
wilaya ya Temeke, Zahra Mohamed alisema amelelewa naye (Simba). Akasema
‘kung’atuka’ kwake (sasa kufukuzwa kwake ndani ya chama) kunampa
masikitiko.
“Lakini hakuna jinsi, huo ndio utaratibu wa chama kuongoza miaka 10,”
alisema. Akaendelea kumwelezea: “Suala la vikoba, mikopo ya benki na
miradi mbalimbali mwenyekiti wetu ndiye aliyekuwa anatuhimiza. Kulikuwa
na jengo letu lile la Zain huyu mama alilirudisha kwani lilikuwa
linapotea na hivi sasa pesa inaingia.
Vile vile mwenyekiti wetu huyo amekuwa akijitoa sana kwa akina mama
kwa misaada mbalimbali,” anamwelezea Simba. Kwa mujibu wa wasifu kutoka
katika tovuti ya Bunge, Simba ana Shahada ya Uzamivu ya Sayansi ya
Uchumi na Maendeleo ya Jamii aliyoipata mwaka 2007 katika Chuo Kikuu cha
New Hempshire.
Aidha, mwaka 1997 alipata Stashahada ya Uzamili ya Sheria za wanawake
kutoka Chuo Kikuu cha Zimbabwe. Mwaka 1992 alitunukiwa Shahada ya
Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Baada ya kutumika katika taasisi mbalimbali ikiwamo MEIDA
(1979-1995), Tantrust Group of Companies (1977-1978) na pia Shirika la
Maendeleo – NDC (1971-1977), mwaka 1995 aliingia bungeni kwa mara ya
kwanza na hadi anafukuzwa uanachama, alikuwa Mbunge wa Viti Maalumu.
Tuesday, March 14, 2017
KARIBU TUME YA MAENDELEO YA USHIRIKA
KARIBU TUME YA MAENDELEO YA USHIRIKA
Popular Posts
-
Kiongozi wa chama cha upinzani cha Forum for Democratic Change (FDC) nchini Uganda Kizza Besigye amekamatwa tena na maafisa wa polisi. ...
-
Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda akizungumza na watumishi wa Mkoa wa Rukwa (hawapo pichani) Wakuu wa taasisi mba...
-
Na Dotto Mwaibale KUNDI la uhalifu la watoto wenye umri kuanzia miaka 18 hadi 25 maarufu kama panya road linatishia usalama wa ...
-
Mkuu wa Wilaya ya Songwe Samuel Jeremia Opulukwa akinawa mikono kabla ya kuingia katika Zahanati ya Saza itakayotumika kutibu endapo ata...
-
MKURUGENZI wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Tanzania (DCI), Robert Boaz Mikomangwa amesema Jeshi la Polisi nchini Tanzania na vyombo vingi...
Powered by Blogger.
0 comments:
Post a Comment