METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, October 22, 2016

Serikali yaagiza usawa huduma kwa wananchi

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki amewataka watumishi wa umma na sekta binafsi kuwahudumia wananchi kwa usawa na kutumia utawala wa sheria.

Aidha, ameitaka Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kutekeleza majukumu yake ya kulinda na kutetea misingi ya utawala bora na kulinda haki za binadamu kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi.

Kairuki aliyasema hayo Dar es Salaam katika maadhimisho ya Miaka 50 ya Tume ya Kudumu ya Uchunguzi na kueleza kuwa utawala wa sheria unamtaka mtu binafsi, taasisi za umma, taasisi za kitaifa na sekta binafsi kuheshimu misingi yote ya utawala bora.

Alisema umuhimu wa tume hiyo ni kuangalia haki katika utendaji wa serikali, vyombo vya serikali na huduma, ndiyo maana Mwalimu Julius Nyerere aliamua kuanzisha tume hiyo.

‘’Tume hii ilikuwa ni taswira ya utawala bora, kufanya maadili, haki za binadamu masuala ya rushwa. Kupitia tume hii tumepata vyombo vitatu ambayo ni Tume ya Haki za Binadamu, Sekretarieti ya Maadili na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU),’’ alisema Kairuki.

Aliongeza kuwa, vyombo hivyo ni muhimu katika masuala ya uwajibikaji, uadilifu na kusimamia masuala ya sheria na utawala bora.

Aidha, alisema serikali inaendelea kushirikiana nao kuhakikisha wanawajengea uwezo kifedha, miundombinu na kiufanisi ili kufanya kazi nzuri zaidi.

Naye Mwenyekiti wa Tume hiyo, Bahame Nyanduga alisema katika maadhimisho hayo vitu vikubwa wanavyovikumbuka ni kuanzishwa kwa tume hiyo na kumuenzi Mwalimu Nyerere ambaye alikuwa muumini wa haki za binadamu na utawala bora.

Alisema tume hiyo imetetea misingi iliyoanzishwa na Nyerere na wahusika wakuu wanaochunguzwa ni watendaji wa taasisi za umma.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inasimamia hayo ili kuhakikisha kuwa nchi inakuwa na maendeleo licha ya kwamba wapo watu wanaokiuka haki za binadamu.

Naye, Jaji mstaafu na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Tanzania (NEC), Damian Lubuva alisema Mwalimu Nyerere alianzisha tume hiyo ili kujenga Taifa lenye uhuru, umoja na kuheshimiana, lakini pia kusimamia watendaji wenye hulka tofauti na kusimamia tabia za wanaoendesha mamlaka kuu ikiwemo Serikali, Bunge na Mahakama.

Maadhimisho hayo yaliwakutanisha viongozi mbalimbali wa serikali akiwemo Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, mawaziri wakuu wastaafu, Jaji Joseph Warioba na Frederick Sumaye na viongozi wengine wastaafu wa tume hiyo na serikali.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com