METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, October 16, 2016

Marekani na Urusi zashindwa kukubaliana kuhusu Syria

Schweiz Lausanne - Schweiz Sergej Lawrow und John Kerry beraten in Lausanne รผber den Syrien-Krieg (picture-alliance/abaca/A. Gumus)
Mkutano kati ya Marekani, Urusi na nchi nyingine saba za kikanda, umeshindwa kufikia makubaliano kuhusu mzozo wa Syria. Huku mapigano yakiendelea ndani ya Syria kwenyewe, wajumbe wamekubaliana kufanya mazungumzo zaidi.

Mazungumzo hayo ya kimataifa yaliyozijumuisha Marekani, Urusi pamoja na mataifa mengine saba ya kikanda yamemalizika jana Jumamosi, baada ya wajumbe kujadiliana kwa zaidi ya saa nne, huku yakionyesha ishara kuwa yamepiga hatua kidogo sana katika kutafuta suluhisho la kisiasa la vita vya Syria vilivyodumu kwa miaka sita sasa.

Baada ya miezi kadhaa ya mazungumzo, pamekuwa na matarajio kidogo ya kupatikana kwa ufumbuzi wa haraka wakati ambapo Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry na mwenzake wa Urusi, Sergei Lavrov walipokutana na wanadiplomasia waandamizi kutoka Saudi Arabia, Iran, Iraq, Uturuki, Qatar, Misri na Jordan kwenye mji wa Uswisi, Lausanne, mkutano wa kwanza kufanyika tangu kuvunjika kwa makubaliano ya kusitisha mapigano mwezi uliopita. Mataifa yenye nguvu ya Ulaya hayakuhudhuria mkutano huo, lakini yatakutana katika mkutano mwingine tofauti na Marekani, mjini London, Uingereza leo Jumapili.

Wakati mapigano yaliyosababisha mauaji ya watu 400,000 na mamilioni wengine kuyakimbia makaazi yao yakiendelea, Lavrov amesema pande hizo zimejadiliana kuhusu masuala ya kuvutia, huku Kerry akisema wanatafuta njia nyingine mpya ya amani na kuangalia namna ya kuyafufua tena makubaliano ya kusitisha mapigano. Kerry amesema wamekubaliana kuendelea kwa mazungumzo ya ngazi ya juu.

Masuala muhimu ambayo bado hayajafikiwa ni pamoja na kuyashawishi makundi mengi yenye silaha kuheshimiwa kwa mpango wa kusitisha mapigano, kuwatenganisha waasi wanaoungwa mkono na mataifa ya Magharibi, Ghuba na Uturuki kutoka kwenye makundi yanayotambuliwa kama ya kigaidi, kufungua njia ili kuruhusu misaada ya kibinadamu kufika kwenye maeneo yaliyozingirwa na kukubaliana kuhusu mpango utakaosaidia kupatikana kwa suluhisho la kisiasa ambao jumuiya ya kimataifa na mataifa yenye nguvu ya kikanda yana mitazamo tofauti kuhusu nafasi ya Rais wa Syria, Bashar al-Assad na mustakabali wa nchi hiyo.

Makubaliano kuhusu mapambano na IS

Suala pekee ambalo wajumbe hao wanaonekana kukubaliana, ni kuwarejesha nyuma na kuwasambaratisha wapiganaji wa kundi la Dola la Kiislamu-IS, ambao wanaendesha mashambulizi Syria na Iraq. Kuvunjika kwa mpango wa kusitisha mapigano uliofikiwa kati ya Marekani na Urusi, kumefatiwa na ghasia kubwa mjini Aleppo, ambako vikosi vya Syria vikiungwa mkono na wapiganaji wa Iran na ndege za kivita za Urusi, wanaendesha mashambulizi kwa lengo la kuukomboa mji huo wa mashariki kutoka kwa waasi waliofanikiwa kuuzingira na kuwafanya kiasi ya raia 250,000 kukwama.

Kukombolewa kwa Aleppo, mji uliokuwa na wakaazi wengi nchini Syria kabla ya kuzuka kwa vita na ambao umeharibiwa vibaya, kutakuwa ni ushindi utakaosababisha wahanga wengi. Katika hatua hiyo, Marekani, mataifa ya Ghuba na Uturuki zitabidi kuamua iwapo zinataka kuwasaidia zaidi waasi wenye itikadi kali, wakiwemo wenye mafungamano na mtandao wa kigaidi wa Al-Qaeda
Uturuki kwa upande mmoja imelegeza msimamo wake kuhusu mustakabali wa Assad na kupatana na Urusi wakati ikijikita zaidi katika mapambano dhidi ya IS na kuwazuia matarajio ya Wakurdi wa Syria, ambao walivamia kaskazini mwa Syria mwezi Agosti.

Tangu kuanza kwa vuguvugu la maandamano ya kupigania demokrasia kwenye nchi za Kiarabu mwaka 2011, mzozo wa Syria umetumbukia katika pande mbalimbali na kusababisha kuibuka kwa maeneo mengi ya mapambano, hivyo kuchangia kuwepo makundi kadhaa ya waasi yakiwemo yale yenye wapiganaji ambao ni raia wa Syria na wageni, mahasimu wa kikanda na mataifa yenye nguvu duniani. DW
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com