Makundi
ya upinzani katika Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yameitisha
maandamano mengine leo ya kumpinga Rais Joseph Kabila, siku moja baada
ya makabiliano yanayodaiwa kusababisha vifo vya watu 50.
Hali
imeendelea kuwa tete nchini Kongo. Usiku wa kuamkia leo, makao makuu ya
vyama vitatu vya upinzani yameteketezwa kwa moto. Maiti tatu zilizoungua
kabisa kiasi cha kutoweza kutambulika zilitolewa katika jengo la chama
kikuu cha upinzani cha Union for Democracy and Social Progress, UDPS,
huku watu wengine wawili wakiteketezwa moto wakiwa hai na mwengine mmoja
kujeruhiwa.
Mashambulizi
hayo ya moto yanatokea baada ya makabiliano ya jana kati ya polisi na
waandamanaji katika mji mkuu, Kinshasa. Kwa mujibu wa ripoti za
serikali, miongoni mwa waliopoteza maisha kufuatia maandamano hayo ni
pamoja na maafisa wanne wa usalama.
Walinda usalama wakikabiliana na waandamanaji mji wa Kinshasa
Viongozi
wa upinzani wanamtaka Rais Kabila, ambaye ameongoza Kongo tangu mwaka
2001,kujiuzulu, wakisema analenga kuongeza muhula mwengine kinyume na
katiba. Makabiliano hayo ya jana yametajwa kuwa mabaya zaidi kutokeoa
mjini Kinshasa tangu Januari mwaka 2015, baada ya polisi kuyavunja
maandamano mengine ya upinzani yaliyosababisha vifo vya watu kadhaa.
Waziri wa Usalama wa Ndani, Evariste Boshab, ameyataja maandamano hayo
yanayofanywa na upinzani kama maasi na kusema serikali haitayavumilia
Japo Rais
Kabila amezuiwa na katiba kugombea muhula mwingine, hajachukua hatua
zozote kutoa ratiba ya kufanyika uchaguzi mkuu, hali iliyozua wasiwasi
kuwa huenda akaendelea kukaa madarakani, hata baada ya muda wake
kukamilika tarehe 20 mwezi Disemba mwaka huu. Mwandamanaji mmoja alisema
hawatamkubalia Rais Kabila tena "Sisi tunazingatia Kifungu cha 64 cha
Katiba. Muda wa kuhudumu Kabila umemalizika. Iwapo anataka kutuuwa,
Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC, itamshughulikia. Hatumtaki tena.
Anapaswa kuondoka ofisini. Muda wake wa kuhudumu umekamilika. Anapaswa
kuondoka."
Rais wa DR Kongo Joseph Kabila (Katikati) katika sherehe za kuadhimisha uhuru wa Kongo, eneo la Kindu
0 comments:
Post a Comment